Waraka kuhusu Mahubiri ya Fumbo la Imani unajadiliwa na Baraza la Maaskofu Katoliki
Marekani
Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani litakuwa na mkutano wake kuanzia tarehe 12 hadi
15, Novemba 2012, huko Baltimore, pamoja na mambo mengine yanayogusa maisha na utume
wa Kanisa nchini Marekani, wanatarajiwa kupigia kura Waraka kuhusu Mahubiri ya Fumbo
la Imani, utakaotolewa na Kamati ya Makleri, Watawa na Miito ya Baraza la Maaskofu
Katoliki Marekani.
Walengwa wakuu wa Waraka huu ni: Makleri na walezi wa Majando
kasisi, ili waweze kutekeleza vyema wajibu wao wa kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza
watu wa Mungu kwa njia ya mahubiri yaliyoandaliwa barabara, yenye kuleta mvuto na
mguso; yanayotangaza na kurithisha imani ya Kristo na Kanisa lake. Waraka huu unasema,
kiini cha utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu ni Kristo, aliyeteswa, akafa na kufufuka
kutoka katika wafu, atakayerudi kuwahukumu wazima na wafu na wala ufalme wake hautakuwa
na mwisho.
Wahubiri wanachangamotishwa na Mama Kanisa kwa namna ya pekee kuhakikisha
kwamba mahubiri yao yanagusa uhalisia wa maisha na kamwe yasiwe ni mahubiri yanayoelea
katika ombwe na hivyo kuwaacha waamini wakavu na mahangaiko makubwa katika undani
wa maisha yao ya kiroho.
Ni mahubiri yanayopaswa kutambua tofauti za kitamaduni
na mwingiliano wa watu, kuliko ilivyokuwa miaka kadhaa iliyopita. Ni umati ambao unaguswa
kwa namna ya pekee na maendeleo ya sayansi na teknolojia bila kusahau tabia ya ukanimungu
inayojengeka kwa kasi miongoni mwa Jamii katika nchi zilizoendelea zaidi duniani.
Ni waamini ambao kwa kiasi kikubwa hawakubahatika kupata Katekesi ya kina kuhusu mafumbo
ya Imani ya Kanisa.
Wahubiri wanapaswa kutambua kwamba, mahubiri yao ni sehemu
muhimu sana katika maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa na wala si kiraka katika Ibada
zinazoendeshwa na Kanisa, kumbe, kuna haja ya kujiandaa kikamilifu, ili kufikisha
ujumbe unaokusudiwa, yaani kuwalisha watu Neno la Mungu, lililoandaliwa vyema, baada
ya tafakari ya kina.
Mahibiri yawaguse waamini, ili kuchochea hamu ya kutaka
kukutana na Kristo, hamu ya kutaka kumfahamu, kumpenda na kumtumikia Mwana wa Mungu
aliyejitoa bila ya kujibakiza kwa jili ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi
la dhambi na mauti na hivyo kumshikirisha ile hadhi ya kuitwa tena mwana mteule wa
Mungu.
Mahubiri yaanzishe mchakato wa majadiliano ya kina kati ya Neno la Mungu
na maisha ya mwamini, ili kujenga urafiki wa kweli na Yesu Kristo pamoja na jirani.
Wahubiri wawasaidie waamini kuelewa vifungu vya Maandiko Matakatifu mintarafu utamaduni
wao, ili kuwajengea uwezo wa kuchuchumilia utakatifu wa maisha, wanapojitahidi kumwilisha
Injili ya Kristo katika uhalisia wa maisha yao.
Maendeleo ya sayansi na teknolojia
ya mawasiliano yawawezeshe waamini pia kuhakikisha kwamba, wanajitahidi kuwa na Neno
la Mungu wanaposafiri, sehemu zao za kazi lakini zaidi katika familia, ili kweli Neno
la Mungu liweze kuwa ni dira na mwongozo wa maisha ya wafuasi wa Kristo. Wahubiri
wajitahidi kuwafahamu vyema waamini wao, ili hata mahubiri yao yaweze kuleta maana
na mguso wa kweli, vinginevyo ni sawa na kumpigia mbuzi gitaa!
Mahubiri yasiwe
ni mahali pa Makleri kuonesha umwamba wao katika taalimungu na kwamba, daima wajitahidi
kutangaza kile ambacho Mama Kanisa anawataka na wala mahubiri isiwe ni mahali pa kutolea
mawazo binafsi. Watambue kwamba, kuna waamini ambao wanashiriki Ibada ya Misa Takatifu
hasa zaidi wakati wa Siku kuu ya Noeli, Pasaka, Mazishi, Ndoa na Sakramenti mbali
mbali, uwe ni wakati muafaka wa kuwakaribisha tena ili waweze kujisikia kuwa hata
wao ni sehemu ya maisha na utume wa Kanisa na kamwe usiwe ni muda wa kuwakejeli na
kuwadhalilisha.