2012-11-12 08:48:18

Ujumbe na matashi mema kwa Askofu mkuu mteule Justin Welby, Kiongozi mkuu wa Jumuiya ya Waanglikani Duniani


Kardinali Kurt Koch, Rais wa Baraza la Kipapa la uhamasishaji wa umoja miongoni mwa Wakristo, kwa niaba ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amemtumia ujumbe wa matashi mema, kheri na baraka, Askofu mkuu mteule Justin Welby wa Jimbo la Durham ambaye hivi karibuni ameteuliwa na kuthibitishwa na Malkia wa Uingereza kuwa Askofu mkuu mteule wa Jimbo kuu la Cantebury, Uingereza na Kiongozi mkuu wa Jumuiya wa Anglikani Duniani.

Kardinali Koch anasema, uhusiano kati ya Kanisa Anglikani na Kanisa Katoliki ni muhimu sana katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene, changamoto kwa wakristo kuendelea kuwa waaminifu kwa Kristo anayewataka wafuasi wake kuwa wamoja kama ambavyo anabainisha katika ile sala ya kikuhani.

Kwa takribani miaka hamsini iliyopita, Makanisa haya mawili yameendelea kujikita katika majadiliano ya kiekumene katika ngazi ya kitaalimungu, kwa kutafuta muafaka unaopania kuwasaidia waamini wa Makanisa haya kufahamiana kwa karibu zaidi.

Katika kipindi hiki chote, Mapapa na Wakuu wa Kanisa Anglikani wamekutana na kuzungumza mara kwa mara, kwa pamoja wamekazia urafiki wao katika maisha ya kiroho na kiutu pamoja n akutambua changamoto iliyoko mbele yao ya kutaka kutolea kwa pamoja ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake na huduma kwa Jamii inayowazunguka.

Ni matumaini ya Kardinali Koch kwamba, urafiki huu utaendelezwa na kwamba, kwa wakati muafaka atajitahidi kutafuta nafasi ya kuweza kukutana naye ana kwa ana kwa ajili ya majadiliano ya pamoja yanayopania kudumisha umoja wa kikristo, ili ulimwengu uweze kuamini. Anapenda pia kumhakikishia sala zake anapotekeleza wajibu na dhamana aliyokabidhiwa kwa Kanisa Anglikani.







All the contents on this site are copyrighted ©.