2012-11-12 08:56:47

Elimu inayotolewa na taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu inapaswa kujikita katika kufundisha, kutafiti na huduma kwa jamii


Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mwenge, MWUCE, kinachomilikiwa na kuendeshwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, hivi karibuni, kilisherehekea mahafali yake ya tano kwa kutoa Shahada ya kwanza ya ualimu kwa wanafunzi 591 na wengine 12 walipokea cheti katika masomo ya sayansi ya Computer kutoka Chuoni hapo.

Katika mahafali yao, Askofu John Ndimbo, mwenyekiti wa Idara ya Elimu Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, alisema kuna haja kwa taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu nchini Tanzania kujikita zaidi katika maboresho katika ufundishaji, tafiti na huduma za kijamii, ili wahitimu hao wanapotoka vyuoni waweze kuwa wamepikwa barabara kwa ajili ya maendeleo ya Jamii inayowazunguka.

Ni jukumu la Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mwenge kuwaelimisha wanachuo wake, ili watambue malengo ya elimu inayotolewa hapo Chuoni. Kanisa na Jamii inawekeza ili kuhakikisha kuwa wanafunzi hao wanapohitimu waweze kutoa huduma bora zaidi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watanzania wote.

Askofu Ndimbo amewataka wahitimu hao kuhakikisha kwamba, wanajikita katika tafiti za kisayansi, ili kuweza kumwendeleza mtu mzima na kwamba, mwelekeo huu utaiwezesha Tanzania kuendelea kucharuka katika sekta ya elimu. Amewakumbusha kwamba, tafiti za kisayansi zina madai yake, zinahitaji nidhamu, uwajibikaji na majitoleo; inawahitaji watu wenye uwepo mpana na wenye mang’amuzi katika kupembua na kuainisha mambo, ili kweli tafiti hizi zinazofanywa na wasomi hao ziweze kuleta manufaa kwa Jamii ya watanzania na katika mfumo mzima wa elimu.

Kwa upande wake, Askofu Isaac Amani, Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo Kikuu Kishiriki cha Mwenge, Moshi katika hotuba yake, amewataka wahitimu kukuza na kuendeleza kipaji cha ugunduzi wanapotekeleza majukumu yao kama wasomi na kundi muhimu sana katika maendeleo na ustawi wa Jamii. Anasema, Chuo Kikuu Kishiriki cha Mwenge kitaendelea kutoa elimu kwa kuzingatia ubora na viwango vinavyotakiwa na Mama Kanisa pamoja na Chuo Mama cha Mtakatifu Augustino cha Tanzania, SAUT.

Askofu Amani ameiomba Serikali ya Tanzania, kuendelea kushirikiana kwa karibu zaidi na Chuo Kikuu Kishiriki Mwenge katika mchakato unaopania kuhakikisha kuwa kuna idadi kubwa zaidi ya wanafunzi wanaojiunga na kuendelea na masomo yao ili kuleta maboresjho makubwa zaidi katika sekta ya elimu, changamoto inayoikabili Tanzania kwa sasa.

Ameiomba Serikali kwa kushirikiana na wadau mbali mbali, kuhamasisha wanafunzi kupenda masomo ya sayansi kwa ajili ya maendeleo ya nchi, kuliko mwelekeo uliopo sasa ambao unawafanya wanafunzi wengi kuogopa masomo ya sayansi, jambo ambalo ni hatari kubwa kwa jamii kwa sasa na kwa siku za usoni.

Askofu Amani anasema, elimu itakuwa na mafunaa pale tu, itakapozingatia ubora na viwango vya kitaifa na kimataifa. Ni jukumu kwa wahitimu kutambua dhamana na wajibu pamoja na kukidhi mategemeo ya jamii inayoendelea kuwekeza kwa vijana wake kwa ajili ya maendeleo ya nchi. Jamii ya watanzania katika ujumla wake, ina imani na matumaini makubwa kwamba, baada ya masomo yao wataweza kutekeleza majukumu yaliyoko mbele yao kwa nidhamu na majitoleo makubwa.

Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Kishiriki Mwenge Dr. Philbert Vumilia, amesema, mfumo wa kuwapima wanafunzi unaotolewa na Chuo hiki unawawezesha wanafunzi kujijengea uwezo na hali ya kujiamini katika utekelezaji wa majukumu yao kama wataalam katika sekta ya elimu.

Amewataka wahitimu kuwa na upeo mpana zaidi katika ulimwengu huu wa maendeleo ya sayansi na teknolojia na kutumia kwa busara zaidi kila fursa inayojitokeza katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwa ajili ya maendeleo yao binafsi na Jamii kwa ujumla wake.

Chuo Kikuu Kishiriki Mwenge ni mahali ambapo wanafunzi wanafurahi kusoma kutokana na juhudi, bidii, maarifa na majitoleo yanayojionesha miongoni mwa wakufunzi na wanafunzi katika ujumla wao. Kwa mwanafunzi anayetaka kusoma, Chuo Kikuu KishirikiMwenge ni mahali pake kabisa. Chuo kitaendelea kuwekeza katika maboresho ya miundo na programme za masomo ili kuinua kiwango cha elimu nchini Tanzania.

Kwa namna ya pekee, upendeleo unatolewa kwa wanawake na wasichana wanaotaka kujikita katika maboresho ya maisha na familia zao, ili kupata watu ambao watakuwa wameiva kitaaluma, kimaadili na kiutu, tayari kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya maendeleo endelevu ya Jamii ya watanzania. Kwa pamoja, Mwenge inapania kuhakikisha kwamba, kweli wanakuwa ni mwanga na nuru ya ulimwengu.

Mgeni rasmi katika mahafali haya alikuwa ni Mheshimiwa Philip Mulugo, Naibu Waziri wa elimu na mafunzo, ambaye amepongeza juhudi na mchango unaotolewa na Chuo Kikuu Kishiriki Mwenge katika sekta ya elimu








All the contents on this site are copyrighted ©.