2012-11-12 08:31:01

Baa la njaa linawanyemelea watu zaidi ya millioni mbili nchini Angola


Serikali ya Angola hivi karibuni ilitangaza hali ya hatari kutokana na kuongezeka kwa baa la njaa nchini humo linalowasibu zaidi ya watu millioni mbili na kati yao kuna watoto laki tano wanaoendelea kusumbuliwa na utapiamlo wa kutisha. Hii ni kutokana na kukithiri kwa ukame na kwamba, kati ya majimbo kumi na nane nchini humo, majimbo kumi yanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula unaotishia maisha ya watoto zaidi ya laki tano.

Serikali ya Angola kwa kushirikiana na wadau mbali mbali ndani na nje ya nchi wamezindua kampeni maalum inayopania kupambana na utapiamlo wa kutisha miongoni mwa watoto. Mpango huu, unatarajiwa kuwahudumia watoto wanaoishi kwenye Majimbo ya Zaire, Bie, Huambo, Kwanza-sul, Cunene, Huila, Bengo, Bengula, Moxico na Namibe. Mpango huu pamoja na mambo mengina utajenga vituo vya afya pamoja na kuwapatia mafunzo wahudumu wa sekta ya afya wapatao elfu mbili, ili kusaidia jitihada za kupambana na utapiamlo nchini Angola.

Ukame wa kutisha kutokana na mvua kutonyeesha kwa muda mrefu, imepelekea kushuka kwa uzalishaji katika sekta ya kilimo, ikilinganishwa na msimu uliopita, kiasi kwamba, usalama wa uhakika wa chakula uko mashakani kwa zaidi ya watu millioni moja na laki nane. Licha ya utajiri mkubwa wa mafuta unaopatikana nchini Angola yenye idadi ya watu millioni ishirini, lakini bado baa la njaa, umaskini na ujinga vinawaandama wananchi wa Angola kwa kiasi kikubwa.







All the contents on this site are copyrighted ©.