2012-11-12 07:54:38

Askofu Beatus Kinyaiya asema vyombo vya habari vina mchango mkubwa katika Uinjilishaji Mpya na wa kina Barani Afrika


Mababa wa Kanisa wanabainisha kwamba, vyombo vya mawasiliano ya jamii ni ulimwengu unaopaswa kuinjilishwa, ili viweze kuleta msukumo mkubwa zaidi katika jitihada za Bara la Afrika kujitafutia maendeleo endelevu. Vyombo vya habari vina mchango mkubwa katika kukuza na kuimarisha umoja na mshikamano kati ya Familia ya binadamu daima wakipania kutafuta mafao ya wengi. RealAudioMP3

Teknolojia ya habari na mawasiliano ilenge pia kukuza na kudumisha haki, amani, umoja na mshikamano wa kweli. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika Waraka wake wa kichungaji Dhamana ya Afrika anabainisha kwamba, kuna haja ya vyombo vya habari kutumika katika dhamana ya Uinjilishaji, sanjari na kusaidia juhudi za Kanisa Barani Afrika katika mchakato unaopania kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho.

Tangu baada ya maadhimisho ya Sinodi ya kwanza ya Maaskofu Barani Afrika, Majimbo na Mashirika mbali mbali yameanzisha Radio ili kuimarisha juhudi za Uinjilishaji wa kina. Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Askofu Beatus Kinyaiya wa Jimbo Katoliki Mbulu, Tanzania anasema, Radio Habari Njema inayomilikiwa na kuendeshwa na Jimbo Katoliki Mbulu, ina mchango mkubwa katika azma ya Uinjilishaji mpya na wa kina, kwa sababu inaburudisha, inahabarisha, inafundisha, inaonya na kukemea.

Ikumbukwe kwamba, upashanaji habari ni wito unaopania kuwamegea wengine ile furaha ya Habari Njema inayobubujika kutoka katika maisha na utume wa Kanisa. Katika utume huu, Kanisa linatekeleza wajibu huu nyeti likikabiliwa na changamoto mbali mbali, ikiwemo uhaba wa rasilimali fedha na rasilimali watu, kiasi kwamba, wakati mwingine haliwezi kukidhi ndoto za wafanyakazi wake za kupata mishahara minono na marupurupu kibao! Wafanyakazi hawa wanapaswa kutambua kwamba, Kanisa linathamini sana mchango wao katika Uinjilishaji.

Askofu Beatus Kinyaiya anawaalika wasikilizaji kwa namna ya pekee, kuhakikisha kwamba, wanajenga utamaduni wa kusikiliza kwa makini na kuacha mtindo wa kubagua vipindi, kwani vyote vimepangwa kwa ajili ya majiundo ya mzima: kiroho na kimwili. Anawapongeza wamiliki wa vyombo vya upashanaji habari ambavyo vinaendelea kuongezeka nchini Tanzania kwa kuthubutu kuwekeza katika sekta hii nyeti, yenye madai ya rasilimali watu, fedha na muda.

Anasema, changamoto na ugumu wanaokutana nao visiwakatishe tamaa, bali wasonge mbele wakipania kuboresha huduma yaokwa jamii, kwa kuzingatia mafao ya wengi, misingi ya haki, amani, utu na maadili mema. Matatizo na changamoto zinapojitokeza zitafutiwe dawa ili vyombo hivi viendelee kutoa huduma kwa Jamii husika.







All the contents on this site are copyrighted ©.