2012-11-10 11:05:58

Watoto wana haki ya kuwa na Baba na Mama katika Familia!


Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican katika tahariri yake anabainisha kwamba, kwa siku za hivi karibuni kumekuwepo na matukio makuu matatu yanayojikita katika suala zima la ndoa. Mahakama kuu nchini Hispania imetupilia mbali rufaa iliyokuwa inataka sheria kutambua kwamba ndoa inaundwa na uhusiano kati ya mume na mke, badala ya kuachia mahusiano haya kuwa ni kati ya watu wawili.

Nchini Ufaransa, Serikali imepeleka muswada unaowataka wabunge kujadili na hatimaye kubadili sheria kuhusu ndoa ili kuwashirikisha pia watu wa jinsia moja wanaotaka kuishi pamoja kama Bwana na Bibi. Nchini Marekani, kuna baadhi ya sheria ambazo zimefanyiwa marekebisho wakati wa pilika pilika za uchaguzi mkuu nchini humo uliohitimishwa hivi karibuni ili kutoa mwanya kwa watu wa jinsia moja kuungana pamoja kama Bwana na Bibi.

Padre Lombardi anasema kwamba, hii kimsingi si habari, kwani tangu mwanzo, watu wenye mapenzi mema walitambua mwelekeo kama huu, lakini jambo la msingi ambalo watu wanapaswa kujiuliza, Je, mabadiliko yote haya yanamlenga nani? Je, ni kwa ajili ya mafao ya wengi ndani ya Jamii? Huu si msimamo wa Kanisa Katoliki peke yake, hata Rabi mkuu wa Ufaransa ameonesha kusikitishwa sana na mwelekeo huu. Hili si swala la ubaguzi wa kijinsia.

Hapa ni kutambua kwamba, mtoto anayezaliwa anayo haki ya kuwamfahamu Baba na Mama yake, ili kuwa kweli na mwono chanya kuhusu maisha ya mwanadamu, utu na heshima yake, bila kusahau mahusiano yake ndani ya Jamii. Ndoa ya watu wa jinsia moja, anasema Padre Lombardi si utamaduni unaopaswa kupigiwa debe! Kuna mifumo mbali mbali ya ndoa ambayo pia si sahihi kwa mfano ndoa za wake wengi.

Kanisa litaendelea kusimama kidete kulinda na kutetea ndoa kati ya mwanaume na mwanamke kadiri ya mpango wa Mungu kwa mwanadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.