Waimbaji wanayo dhamana ya kutangaza Imani na kushiriki kikamilifu katika mchakato
wa Uinjilishaji Mpya kwa njia ya karama na vipaji vyao!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumamosi tarehe 10 Novemba 2012 alikutana
na kufanya mazungumzo na Wanachama wa Chama cha Kitume cha Mtakatifu Cecilia kinachojikita
zaidi katika nyimbo zinazohamasisha ushiriki mkamilifu katika Liturujia, wakati wa
Kongamano lao kitaifa, kama sehemu ya kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso
Mkuu wa Pili wa Vatican.
Ni chama ambacho, kimekuwa mstari wa mbele kufundisha
kwa namna ya pekee, Katiba ya Liturujia ya Kanisa mintarafu Mafundisho ya Mtaguso
wa Pili wa Vatican. Baba Mtakatifu anasema kwamba, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani yanapania
kwa namna ya pekee kabisa, kuhakikisha kwamba, waamini wanaifahamu fika imani yao
kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya na kwamba, Muziki Mtakatifu una sehemu
kubwa katika kuimarisha na kuhamasisha shughuli za Uinjilishaji Mpya.
Baba
Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika hotuba yake kwa wanachama hawa, amegusia
mchango wa Mtakatifu Agostino, Askofu na Mwalimu wa Kanisa, aliyeshiriki kwa kipindi
kirefu maadhimisho ya Liturujia yaliyokuwa yanaongozwa na Mtakatifu Ambrose, kwa kusema
kwamba, imani kimsingi inazaliwa kutokana na kusikiliza Neno la Mungu katika mapana
yake. Kutokana na ukweli huu, nyimbo ambazo zinachota utajiri wake kutoka katika Zaburi
na Maandiko Matakatifu kwa ujumla, zina uwezo mkubwa wa kutangaza imani pamoja na
kusaidia juhudi za Uinjilishaji, kama anavyoshuhudia Mtakatifu Agostino.
Itakumbukwa
kwamba, anayeimba vizuri huyo anasali mara mbili, ndiyo maana Mtakatifu Ambrose alitoa
kipaumbele cha kwanza kwa kukuza na kuimarisha muziki mtakatifu wakati wa maadhimisho
ya Liturujia ya Kanisa. Ushuhuda wa Mtakatifu Agostino anasema Baba Mtakatifu uwe
ni ushuhuda makini katika harakati za Mama Kanisa kwamba, Muziki mtakatifu, ukiambatana
na maneno ni sehemu ya Liturujia ya Kanisa, inayoweza kuboresha imani na hivyo kumwimbia
Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani; hatima yake, ni kwa ajili ya kuwatakatifuza
Watu wa Mungu.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa namna ya pekee,
anawashukuru na kuwapongeza Wanakwaya wanaotumia vyema vipaji na karama zao kwa ajili
ya kuhamasisha Liturujia ya Kanisa, ili waamini wanaposhiriki katika ujumla wao, waweze
kumtolea Mwenyezi Mungu sifa na heshima; wakitambua daima kwamba, kwa kuimba wanasali
na kuwafanya wengine kushiriki katika sala hii, ili kwa pamoja Mwenyezi Mungu aweze
kupewa sifa anayostahili.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, kuna uhusiano wa
dhati kati ya Nyimbo na Uinjilishaji Mpya; changamoto ya kuthamini na kuenzi nyimbo
mbali mbali zinazotungwa hata katika Makanisa machanga duniani. Kwa njia ya nyimbo
watu wanaweza kugundua uwepo wa Mungu katika hija ya maisha yao, wanaweza kutubu na
kuongoka pamoja na kuimarisha imani yao.
Nyimbo zilizotungwa kwa ufasaha na
ustadi mkubwa zina mvuto na mguso katika akili na mioyo ya watu, changamoto kwa watunzi,
wanamuziki na waimbaji wenyewe kutambua dhamana na mchango wao katika maboresho ya
Liturujia, bila kusahau kuthaminisha utajiri wa nyimbo za Kanisa kama ambavyo Mababa
wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican wanaendelea kuhimiza.
Mwishoni, Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita, anawahimiza waimbaji kuhakikisha kwamba, wanawashirikisha
Watu wa Mungu katika Liturujia kwa kusikiliza na kushiriki kikamilifu, ili kwa njia
ya vipaji na karama zao, waiwezeshe mioyo ya waamini kuimba wakati wa maadhimisho
ya Liturujia ya Kanisa.