2012-11-10 15:46:48

"Padre Quadrio alikumbatia ukweli na upendo ili kupata ukweli wa upendo"


Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican, Jumamosi tarehe 10 Novemba 2012, ameshiriki katika maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 75 tangu Kitivo cha Taalimungu, Chuo Kikuu cha Torino, kilipoanzishwa na kumbu kumbukumbu ya miaka 50 tangu alipofariki dunia Mheshimiwa Padre Quadrio, aliyezaliwa tarehe 28 Novemba 1921. Ni mtu ambaye maisha yake yalitajirishwa na tafakari ya Neno la Mungu, Maisha ya Kisarkamenti na matendo ya toba, kama sehemu ya mchakato wa hija ya maisha yake kutaka hata yeye siku moja aweze kuwa kati ya Watakatifu wa Mungu.

Ni Padre aliyekuwa na Ibada ya pekee kwa Bikira Maria aliyepalizwa mbinguni mwili na roho, akajitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya majiundo ya wanafunzi wake katika Mafundisho tanzu ya Kanisa. Alikuwa ni Padre aliyetoa mchango mkubwa katika tafakari za Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, hususan kuhusu mwaliko wa waamini wote kuchuchumilia utakatifu wa maisha. Alipokea mateso na ugonjwa wake kwa imani na matumaini makubwa, daima akiendelea kujikita katika sala.

Kardinali Bertone anasema kwamba, Padre Quadrio alikuwa ni Jaalimu aliyesimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Maisha kwa njia ya ushuhuda wake uliojengeka katika maahusiano mazuri na watu, kiasi kwamba, akapewa dhamana ya kufanya utume na shughuli za kichungaji miongoni mwa vijana. Akakuza uhusiano huu katika misingi ya urafiki, kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu ni rafiki wa wote.

Alikuwa mtu mwema na mwenye moyo mzuri kwa wote waliokuwa wanateseka katika umaskini na upweke; akaguswa na mahangaiko yao; akawasikiliza kwa umakini mkubwa na kuwapokea jinsi walivyo, akijitahidi kuwasaidia kadiri ya uwezo wake. Alipenda pia kutekeleza Mapenzi ya Mungu katika maisha yake na daima alionesha imani kubwa, kwa hakika anasema Kardinali Bertone, huyu alikuwa ni Padre na mfano wa kuigwa katika maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, chanzo na kilele cha maisha na utume wa Kanisa.

Aliliadhimisha Fumbo hili kwa Ibada na uchaji; akalitafakari na hatimaye kulimwilisha Neno la Mungu katika maisha na utume wake. Injili ilikuwa ni dira na mwongozo wake, kiasi kwamba, alitambulika kuwa kweli ni mtangazaji wa Habari Njema ya Wokovu na Jalimu mahiri la Maandiko Matakatifu na kielelezo cha utakatifu wa maisha.

Kardinali Tarcisio Bertone anasema kwamba, dhamana ya Uinjilishaji Mpya inayofanyiwa kazi na Mama Kanisa kwa sasa lazima iende sanjari na maisha ya: Sala, tafakari ya kina pamoja na kujenga umoja na mshikamano miongoni mwa Familia ya Mungu kwa kutambua kwamba, Kanisa hapa duniani linasafiri kuelekea Yerusalemu ya mbinguni, changamoto ya kuwa kweli ni watu wa Mungu, kwa kukumbatia upendo na ukweli ili kupata ukweli wa upendo







All the contents on this site are copyrighted ©.