2012-11-09 09:50:26

Vyombo vya mawasiliano ya Jamii vina mchango mkubwa katika azma ya Uinjilishaji Mpya


Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican, hivi karibuni ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya wafadhili wa Radio Maria Poland, waliokuwa wanafanya hija ya maisha yao ya kiroho hapa mjini Roma. Mahujaji hao walifika Roma ili kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa uwepo wa utume wa Radio Maria nchini Poland kwa takribani miaka ishirini, radio ambayo kwa hakika imekuwa ni chombo kikuu cha Uinjilishaji Mpya.

Ilikuwa ni fursa ya kuweza kujifunza kutoka kwa Watakatifu mbali mbali, lakini kwa namna ya pekee, Mtakatifu Petro na Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, ambaye ameitangaza Injili ya Kristo kwa njia ya ushuhuda wa maisha yake.

Kardinali Bertone aliwakaribisha mahujaji hawa kwa niaba ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, aliyewachangamotisha kuhakikisha kwamba, maadhimisho ya miaka ishirini ya Radio Maria nchini Poland, inakuwa ni fursa ya kujiimaarisha kiroho, kwa kufanya hija mjini Vatican na katika Nchi Takatifu. Mahujaji hawa ni kielelezo cha imani ya mtu binafsi na Kanisa katika ujumla wake; ni mashahidi wa upendo wa Mungu kwa waja wake na alama ya matumaini kwa maisha ya uzima wa milele, daima wakijitahidi kuongozwa na huruma ya Mungu katika hija ya maisha yao kuelekea mbinguni.

Kardinali Bertone anabainisha kwamba, imani kimsingi ni tukio ambalo linamwezesha mwamini kukutana na Yesu Kristo Mkombozi wa dunia, ambaye kimsingi ni njia, ukweli na uzima. Vyombo vya mawasiliano ya Jamii vina mchango mkubwa katika dhamana ya Uinjilishaji Mpya. Ameushukuru uongozi wa radio Maria kwa huduma yake makini katika kipindi cha miaka ishirini ya uwepo wake nchini Poland na kwamba, kimesaidia kupandikiza mbegu ya imani, matumaini na mapendo mioyoni mwa watu.

Ni Radio ambayo imekuwa mstari wa mbele katika kukoleza: Moyo na Maisha ya Sala, Katekesi makini, Utangazaji wa Injili, bila kusahau utoaji wa habari kuhusu maisha na utume wa Kanisa pamoja na kurusha matangazo ya maadhimisho ya Ibada mbali mbali zinazoendeshwa na Baba Mtakatifu. Ameitaka radio Maria kuendeleza utume huu makini ndani ya Kanisa kwa kumtumainia Roho Mtakatifu.

Kardinali Tarcisio Bertone, amehitimisha mahubiri yake kwa kuwaweka mahujaji hawa chini ya maombezi ya Bikira Maria nyota ya Uinjilishaji Mpya na ya Mtakatifu Petro, ili Radio Maria poland iweze kuendeleza utume wake kwa ajili ya mafao ya wengi ndani ya Jamii na kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la kiulimwengu.







All the contents on this site are copyrighted ©.