2012-11-09 08:49:37

Mshikamano wa Papa na wananchi wa Guatemala waliokumbwa na tetemeko la ardhi


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amemtumia ujumbe wa upendo na mshikamano Askofu Rodolfo Valenzuela Nunes wa Jimbo la Vera Paz, Guatemala kutokana na tetemeko la ardhi lililotokea tarehe 8 Novemba 2012 na kusababisha watu zaidi ya 50 kupoteza maisha yao na wengine zaidi ya mia moja na sabini kupata majeraha. Zaidi ya wanajeshi elfu mbili wanaendelea na jitihada za kuokoa maisha ya watu waliofukiwa na kifusi baada ya tetemeko hilo.

Baba Mtakatifu anasema, amepokea habari hizi kwa majonzi na masikitiko makubwa, anapenda kuwahakikishia wananchi wa Guatemala walioguswa kwa namna ya pekee na maafa haya uwepo wake wa karibu kwa njia ya sala. Anawakumbuka na kuwaombea wote waliopoteza maisha yao kutokana na tetemeko waweze kupata pumziko la milele na majeruhi waweze kupona haraka na hatimaye, kuendelea na shughuli zao za kila siku.

Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, waathirika wa tetemeko hili wataweza kuonjeshwa upendo na mshikamano wa kweli. Anawataka waamini pamoja na mashirika ya misaada ya Kanisa Katoliki kuunganisha nguvu zake ili kuwasaidia waathirika wa tetemeko hili nchini Guatemala.







All the contents on this site are copyrighted ©.