2012-11-09 09:29:20

Kanisa kumtangaza mtumishi wa Mungu Maria Luisa Prosperi kuwa Mwenyeheri


Mtumishi wa Mungu Maria Luisa Prosperi alizaliwa tarehe 19 Agosti 1799, huko Folignano, Kaskazini Mashariki mwa Italia, akajiunga na Monasteri ya Santa Lucia in Trevi, hapo tarehe 4 Mei 1820 na kupewa jina la Maria Luisa Angelica wa Moyo Mtakatifu wa Yesu.

Kwa mfano wa maisha yake matakatifu, alichaguliwa kuwa Mama mkuu wa Monasteri tangu tarehe Mosi Oktoba 1837, kwa vipindi vinne mfululizo, hadi mauti yalipomfika hapo tarehe 12 Septemba 1847 baada ya kuugua kwa muda mrefu, huku akiyapokea mateso na mahangaiko yake kwa imani na matumaini; anatarajiwa kutangazwa kuwa Mwenyeheri Jumamosi tarehe 10 Novemba, 2012 Jimboni Spoletto, Italia.

Tukio hili la kihistoria katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, linafuatia tukio jingine la aina hii la Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kumtangaza Mtakatifu Ildegarda wa Bingen, kuwa Mwalimu wa Kanisa. Watakatifu hawa ni mfano na kielelezo cha kuigwa katika maisha na utume wa Kanisa, wakati huu Mama Kanisa anapojitahidi kukuza na kuendeleza ari na moto wa Uinjilishaji Mpya kwa njia ya ushuhuda wa maisha. Ni mchango unaotolewa na Familia ya Shirika la Wabenediktini, kwa ajili ya utamaduni na utakatifu wa maisha ya Kanisa.

Ni maneno ya Kardinali Angelo Amato, Rais wa Baraza la Kipapa lenye dhamana ya kuwatangaza wenyeheri na watakatifu, anapoelezea wasifu wa Mtumishi wa Mungu Maria Luisa Prosperi. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika barua yake ya kichungaji, anamwelezea mtumishi huyu wa Mungu kuwa kweli ni mtawa aliyekuwa na Ibada ya pekee katika kuabudu Ekaristi Takatifu pamoja na kukumbatia Fumbo la Msalaba, kielelezo cha huruma na upendo wa Mungu unaokomboa.

Ni mtawa aliyebahatika kuwa na karama mbali mbali alizozitumia kwa ajili ya maisha na ustawi wa Shirika lake na Kanisa kwa ujumla. Ni mwamini aliyekuwa na imani hai ambayo kamwe haikuweza kuterereka hata wakati wa ugonjwa wake. Ni imani iliyokuwa inabubujika kama zawadi safi kutoka kwa Roho Mtakatifu, ikaugusa moyo wake ambao ulisheheni upendo wa Kimungu kwa jirani zake, kiasi cha kuutolea ushuhuda makini na wenye nguvu na mvuto wa pekee. Ni mtawa aliyekuwa na kiu ya kutaka kuonana na Mwenyezi Mungu, asili ya imani yake.

Kardinali Angelo Amato anasema, leo hii Kanisa na Ulimwengu katika ujumla wake, linawahitaji waamini walei, watawa na makleri waweze kushuhudia imani yao, katika hali ya amani na utulivu wa ndani hata wakati wanapokumbana na dhoruba katika maisha yao.







All the contents on this site are copyrighted ©.