Ujumbe wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku kuu ya Deepval kwa Mwaka
2012
Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini limetuma ujumbe na matashi mema kwa waamini
wa dini ya Kihindu katika maadhimisho ya Siku kuu ya Deepval, ujumbe ambao kwa Mwaka
2012 unaongozwa na kauli mbiu "Wakristo na Wahindu wawaandae Vijana wa kizazi kipya
ili waweze kuwa ni wajenzi wa amani".
Katika ujumbe huu, Baraza la Kipapa
la Majadiliano ya Kidini linasema kwamba, mwanadamu nyakati hizi anakabiliwa na nguvu
hasi zinazotishia amani na maelewano kati ya watu, ndiyo maana wanaona inafaa sana
kwa waamini wa dini ya Kihindu na Kikristo kushikamana kwa pamoja ili kusaidia majiundo
ya vijana wa kizazi kipya, ili hatimaye, waweze kuwa ni wajenzi wa amani.
Ikumbukwe
kwamba, amani si kutokuwepo kwa kinzani, migogoro wala vita, lakini ni matunda ya
upendo. Wadau mbali mbali wanahamasishwa kushiriki kikamilifu katika kutafuta, kulinda
na kudumisha misingi ya amani, kama kiini cha malezi ya vijana wa kizazi kipya, kwa
ajili ya mafao ya wengi. Ili amani hii iweze kuwa dumifu, kuna haja ya kuhakikisha
kwamba, inajengeka katika misingi ya ukweli, haki, upendo na uhuru.
Vijana
wa kizazi kipya wanapaswa kuelimishwa katika ukweli, haki, upendo na uhuru. Wadau
mbali mbali wanapotekeleza wajibu na dhamana hii, wanapaswa kukazia kwamba, tofauti
za kidini zinazojitokeza miongoni mwa wananchi ni utajiri mkubwa ambao wanapaswa kuulinda
na kuutunza badala ya kuonekana kana kwamba, ni jambo la hatari.
Ikumbukwe
kwamba, Familia ni shule ya kwanza ya amani na wazazi ni walezi wa kwanza wa amani,
dhamana inayojionesha kwa njia ya mifano bora ya maisha na mafundisho yao; ni watu
wenye dhamana ya kurithisha tunu msingi za maisha ya kijamii, zitakazoiwezesha Jamii
kuweza: kuthaminiana, kuheshimiana, kufahamiana, kusikilizana, kushirikishana, kusaidiana
na kusameheana.
Shule, taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu ni mahali ambapo
vijana wa kizazi kipya wanashirikishana, wanasoma na kufanya kazi kwa pamoja kutoka
katika dini na tamaduni tofauti tofauti, hivyo basi, walimu na walezi katika majiundo
yao wanadhama kubwa ya kuhakikisha kwamba, elimu inayotolewa inaheshimu, inalinda
na kudumisha utu na heshima ya mwanadamu; kwa kukazia urafiki, haki, amani, ushirikiano
na maendeleo endelevu yanayomgusa mtu mzima: kiroho na kimwili.
Tunu msingi
za kimaadili na kiroho hazina budi kuwa ni nguzo thabiti katika utoaji wa elimu pamoja
na kuwajengea wanafunzi uwezo wa kuwa na mang'amuzi ya kina kuhusu siasa na sera ambazo
zinaweza kusababisha kinzani na migawanyiko ndani ya Jamii. Serikali na viongozi mbali
mbali katika maisha ya Kijamii, Kisiasa na Kitamaduni pamoja na sekta nyingine za
maisha, wanao wajibu na dhamana wanayopaswa kutekeleza katika kuimarisha elimu miongoni
mwa vijana wa kizazi kipya.
Viongozi wa dini kutokana na dhamana yao ya maisha
ya kiroho na kimaadili wanapaswa kuendelea kuwahimiza vijana kutembea katika njia
ya amani, ili hatimaye, waweze kuwa kweli ni wajenzi wa amani. Njia za mawasiliano
ya Jamii zinamchango wake katika mchakato mzima wa kumuunda kijana wa kizazi kipya
katika mawazo, vionjo na matendo yake.
Hivyo basi, wadau wa sekta ya mawasiliano
ya jamii hawana budi kuhakikisha kwamba, wanasaidia kutoa mawazo yatakayokoleza mifano
bora ya maisha, kwa kuwajibika barabara wanapotumia uhuru wao katika shughuli za upashanaji
habari sanjari na kuhakikisha kwamba, wanajikita katika ujenzi wa utamaduni wa amani.
Kwa njia hii, Jamii itaweza kujenga utamaduni wa udugu na mshikamano, kwa kutambua
na kumheshimu kila mtu.
Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini linahitimisha
ujumbe wake kwa ajili ya maadhimisho ya Siku kuu ya Deepvali kwa Mwaka 2012 kwa kusema
kwamba, kila mtu anawajibika kutafuta na kujishikamanisha na tunu msingi za kimaadili
na kidini, ili kuwawezesha vijana wa kizazi kipya kuwa kweli ni wajenzi wa amani.
Ujumbe huu umetolewa na Kardinali Jean Lous Tauran, Rais pamoja na Padre Miguel Angel
Ayuso Guixot, Katibu wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini.