2012-11-08 09:14:18

"Mwenyezi Mungu asili ya maisha, akuongoze katika haki na amani Rais Obama"


Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, amemtumia salam za pongezi na matashi mema Rais Barack Obama wa Marekani kutokana na kuchaguliwa kwake kwa kishindo, kuwaongoza Wamarekani kwa kipindi kingine cha miaka minne. Anamtakia baraka na neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu anapoendelea kutekeleza wajibu na majukumu yake kama Rais wa Marekani.

Anasema, Baraza la Makanisa litaendelea kutolea sala zake kwa ajili ya Rais Obama na viongozi wenzake. Akigusia kwa namna ya pekee, mkutano mkuu wa kumi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, utakaongozwa na kauli mbiu "Mungu asili ya maisha, anatuongoza katika haki na amani", amemwalika Rais Obama kuhakikisha kwamba, anatumia ushawishi wake kama Rais wa Marekani katika harakati za kukuza na kudumisha haki na amani, sehemu mbali mbali za dunia.

Ni matumaini ya Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwamba, Rais Obama ataendelea kuwa ni kiongozi na mfano wa kuigwa katika Jumuiya ya Kimataifa, katika mchakato unaopania kutafuta, kulinda na kudumisha misingi ya haki na maelewano hususan kati ya Israel na Palestina.







All the contents on this site are copyrighted ©.