2012-11-08 11:33:58

Matumizi ya maendeleo na sayansi katika njia za mawasiliano Maaskofu Wanapofundisha, Ongoza na Kuwatakatifuza Watu wa Mungu


Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani linajipanga kikamilifu kutekeleza wajibu wake wa kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza Watu wa Mungu katika ulimwengu wa Utandawazi na Maendeleo ya Sayansi na teknolojia kwa njia mpya za mawasiliano ya kijamii, kama changamoto inayoendelea kujitokeza katika Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo sanjari na Uinjilishaji Mpya.

Maaskofu wanategemea kujadili kwa kina na mapana kuhusu matumizi ya njia za mawasiliano ya jamii, katika mkutano wao wa Mwaka utakaofanyika kuanzia tarehe 12 hadi 15 Novemba 2012 huko Baltimore.

Kardinali Donald Wuerl, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani atazungumzia changamoto zinazojitokeza katika Ulimwengu mamboleo na fursa zilizopo katika utekelezaji wa utume wa Maaskofu katika kufundisha: Imani, Maadili na Utu wema. Maendeleo ya matumizi ya njia za mawasiliano na mitandao ya kijamii imeboresha maradufu mawasiliano. Hii ni changamoto kwa Maaskofu kujibu mara moja shutuma au pale ambapo Mafundisho Tanzu ya Kanisa yanapotoshwa au kutafsiriwa vibaya.

Leo hii kuna sauti nyingi zinazoendelea kusikika katika mitandao ya kijamii, Maaskofu wanajiuliza, Je, umefika wakati hata kwa wao pia kuingiza sauti zao katika mitandao hii? Jambo hili linahitaji kwanza kabisa, Maaskofu kufafanua dhamana na wajibu wao katika kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza watu wa Mungu. Njia za mawasiliano ya kijamii ni sawa na upanga wenye makali kuwili, kumbe, zinapaswa kutumiwa kwa umaskini na uangalifu mkubwa zaidi, vinginevyo zinaweza kusababisha ugumu na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao kama Maaskofu mahalia.

Itakumbukwa kwamba, hii ni fursa mpya kwa Maaskofu na viongozi wengine wa Kanisa kuweza kuwasiliana na Waamini wao kwa haraka zaidi, ikilinganishwa na njia ambazo Mama Kanisa amekuwa akitumia kwa takribani miaka elfu mbili iliyopita.








All the contents on this site are copyrighted ©.