2012-11-08 15:24:49

Kuna umuhimu wa kuendeleza majadiliano na ushirikiano kati ya sayansi na imani, ili kujenga utamaduni unaomheshimu binadamu, utu na uhuru wake!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Alhamisi tarehe 7 Novemba 2012 amekutana na kuzungumza na Wajumbe wa Taasisi ya Kipapa ya Sayansi waliokuwa wanafanya mkutano wao wa mwaka hapa mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi 7 Novemba 2012.

Anasema, kuna ugumu na uwiano mkubwa katika sayansi kuhusiana na: nadharia, mbinu na mwelekeo wake wa uandishi, mambo yanayogusa kwa namna ya pekee kabisa umoja katika masuala ya kisayansi.

Katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwepo na maendeleo makubwa ya sayansi na teknolojia, mambo ambayo yamemwezesha mwanadamu kupata ufahamu mkubwa zaidi kuhusu asili na maumbile, changamoto ya kuangalia nafasi ya mwanadamu katika Fumbo la Uumbaji kama sehemu ya mchakato wa kutumia vyema ujuzi na maarifa yake kwa ajili ya kutunza mazingira.

Mwanadamu amekirimiwa na Mwenyezi Mungu akili na uhuru wa kuufahamu ulimwengu, changamoto ya kutumia chenzo hizi ili kupenda, kuishi na kufanya kazi. Leo hii kuna vifaa vinavyomwezesha mwanadamu kufanya majaribio makubwa, lakini daima akumbuke kwamba, kuna haja ya kuwa na umoja katika mchakato wa tafiti za kisayansi ili kufahamu nguvu asilia.

Watafiti na wanasayansi waendelee kurahisisha mafanikio haya kwa ajili ya mafao ya wengi na kwamba, akili na hekima ya kikristo inayopata chimbuko lake katika taalimungu na falsafa inaweza kuleta uwiano bora zaidi kwa kutambua kwamba, mwanadamu anashiriki kwa namna ya pekee kabisa ile kazi ya uumbaji ambayo bado inahitaji kufanyia utafiti wa kina na wanasayansi.

Falsafa na Taalimungu iwasaidie kuwa na uelewa mpana zaidi kuhusu kweli asilia na kazi ya uumbaji, kama changamoto kwa mwanadamu kuinua macho yake, ili kutafakari ukuu wa Mungu ambaye kwa uwamo wake, viumbe vinashiriki ukuu wa Mungu. Kwa njia hii, wanasayansi wataendelea kufanya tafakari ya kina ili kugundua Fumbo la maisha ya mwanadamu na ulimwengu katika ujumla wake.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema kwamba, kuna umuhimu wa kuendeleza majadiliano na ushirikiano kati ya ulimwengu wa sayansi na imani, ili kujenga utamaduni unaomheshimu binadamu, utu na uhuru wake kwa ajili ya mafao ya Familia ya binadamu na maendeleo endelevu hapa duniani.

Bila mwingiliano huu anasema Baba Mtakatifu, mwanadamu atajikuta kwamba, anapoteza mwelekeo wa akili na ukweli na hatimaye, kutekwa na vionjo; mambo ambayo ni hatari kubwa kwa binadamu, amani na mustakabali wake.

Baba Mtakatifu anahitimisha hotuba yake kwa wajumbe wa Taasisi ya Kipapa ya Sayansi, kwa kuwakumbusha kwamba, Mama Kanisa anaendelea kuadhimisha Mwaka wa Imani, kama sehemu ya kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.

Ni matumaini yake kwamba, Taasisi hii itaendelea kuchangia kuboresha na kuimarisha uhusiano uliopo kati ya akili na imani na kwamba, yuko pamoja nao katika sala.








All the contents on this site are copyrighted ©.