2012-11-07 07:26:58

"Msitumie vyandarua kufugia kuku na kutegea samaki"


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amewaelekeza Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kuhakikisha kuwa shule zote za sekondari za kata nchini zinakuwa na vyumba vitatu vya maabara katika muda wa miaka miwili kuanzia Jumatatu, Novemba 5, 2012.

Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali yake inajiandaa kufanya ajira nyingine kubwa ya walimu katika muda mfupi ujao, ili kuzidi kukabiliana na upungufu wa walimu katika shule mbali mbali nchini. Amewataka baadhi ya wananchi wanaotumia vyandarua vya kupambana na ugonjwa wa malaria na vilivyogawiwa bure na Serikali kufugia kuku kuacha mara moja tabia hiyo.

Rais Kikwete ametoa agizo hilo kwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wakati alipozindua na kufungua miradi miwili mikubwa ya ujenzi wa barabara katika Mkoa wa Singida ambako jioni ya leo amemaliza ziara ya siku mbili ya kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo katika Mkoa huo. Miradi hiyo miwili ni uwekaji wa jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya na ufunguzi wa Barabara ya Issuna-Manyoni ambayo ujenzi wake umekamilika.

Akizungumza kabla ya kuweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Barabara ya Manyoni hadi Chaya kupitia Itigi nje kidogo ya mji wa Itigi, Mkoani Singida, Rais Kikwete amesema kuwa ni lazima sasa kukabiliana na kumaliza matatizo yanayokabili sekta ya elimu ukiwemo ukosefu wa maabara ambazo ndizo zitajenga msingi kwa wanafunzi wa Tanzania kuwa wanasayansi.

Rais Kikwete amewambia mamia kwa mamia ya wananchi waliohudhuria sherehe ya uwekaji wa jiwe hilo la msingi: “Sasa nawaagiza viongozi wenzangu- Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya, kila Mkuu wa Mkoa na kila Mkuu wa Wilaya, kusimamia ujenzi wa vyumba vitatu vya maabara, yaani maabara ya fizikia, kemia na baiolojia kwenye kila shule ya sekondari ya kata nchini. Kazi hii nataka ikamilike katika miaka miwili kuanzia leo. Kwa upande wake, Serikali kuu itahangaika kutafuta vifaa vya kufunga katika vyumba hivyo.”

Akiendelea kuwaeleza wananchi kuhusu hatua ambazo Serikali inazichukua kukabiliana na changamoto zinazokabili elimu nchini ambayo imepanuka sana katika miaka saba iliyopita, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali inakamilisha taratibu za kuajiri maelfu ya walimu katika muda mfupi ujao.

“Wakati tunaingia madarakani mwaka 2005, nchi yetu ilikuwa inafundisha na kutoa walimu 500 kwa mwaka. Mwaka jana, idadi hiyo ilifikia walimu 12,000 na sasa tunajiandaa kugawa walimu wengine waliohitimu. Nadhani kwenye Januari, mwakani, kila shule nchini itaongezewa walimu. Tunadhamiria kuwa katika miaka miwili ama mitatu ijayo, tatizo la upungufu wa walimu nchini liwe ni historia,” amesema Rais Kikwete.

Rais pia amewaeleza wananchi kuhusu jitihada zinazofanywa kukabiliana na changamoto katika sekta ya afya ikiwa ni pamoja na kupambana na magonjwa yanayoua watu kwa wingi nchini ikiwamo malaria na ukimwi. Hata hivyo, Rais ameeleza kusikitishwa kwake na tabia ya baadhi ya watu ambao wanatumia vyandarua ambavyo vimegawiwa bure na Serikali kwa kila kaya nchini kufugia kuku ama kuvulia samaki. “Watu wetu wa ajabu sana. Tumegawa vyandarua bure ili sote tuondokane na tatizo la malaria. Lakini nasikia wengine wanavitumia kufugia kuku. Kweli Tanzania inahitaji ubunifu, lakini siyo ubunifu wa namna hii wa ovyo. Tuache kutumia vyandau kufugia kuku, tuvitumie kama ilivyokusudiwa.”









All the contents on this site are copyrighted ©.