2012-11-07 14:39:37

Kardinali Robert Sarah kumwakilisha Papa nchini Syria kama alama ya mshikamano na wananchi wa Syria katika kipindi hiki kigumu


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, mara baada ya Katekesi yake, Jumatano tarehe 7 Novemba 2012 amesema kwamba, anaendelea kufuatilia kwa karibu zaidi hali ya machafuko na vita vinavyoendelea kurindima nchini Syria kwa hofu kubwa, kutokana na idadi ya waathirika kuendelea kuongezeka siku hadi siku na hivyo kusababisha mateso na mahangaiko kwa watu wasiokuwa na hatia, ambao wengi wao tayari wameyakimbia makazi yao wakihofia usalama wa maisha yao.

Baba Mtakatifu anasema, kama alama ya mshikamano wake na Kanisa zima kwa wananchi wa Syria pamoja na Jumuiya za Wakristo nchini Syria, alitamani kutuma ujumbe wa Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya, lakini haikuwezekana.

Sasa ameamua kwamba, kuanzia tarehe 10 Novemba 2012, Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki atakwenda nchini Lebanon, ambako anatarajiwa kukutana na viongozi wa Kanisa pamoja na waamini katika ujumla wao. Atatembelea kambi za wakimbizi pamoja na kuzungumza na Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki, ili kuratibu kwa pamoja misaada inayotolewa na Kanisa kwa ajili ya wananchi wa Syria wanaokabiliana na hali ngumu ya maisha.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anachukua fursa hii kuzitaka pande zote mbili zinazoendelea kusigana pamoja na watu wenye mapenzi mema kwa nchi ya Syria, kuunganisha nguvu zao, ili amani iweze kupatikana kwa njia ya majadiliano na utulivu miongoni mwa wananchi wa Syria, ili hatimaye, suluhu ya kisiasa iweze kupatikana.







All the contents on this site are copyrighted ©.