2012-11-07 08:42:12

Changamoto ya kuwa na utambulisho mpya wa Kanisa katika ulimwengu mamboleo!


Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, karibu tena katika kipindi chetu cha Uinjilishaji wa kina ambapo bado tunaendelea na uchambuzi juu ya Lineamenta ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji mpya. Juma lililopita tuliachana na mawazo juu ya mazingira wanayojikuta wanafamilia ya Mungu katika kumshuhudia Kristo katika ulimwengu wa leo. RealAudioMP3

Juma hili tuungane na Baba Mtakatifu Benedikto XVI anapoendelea kuwaasa Maaskofu wa Sinodi juu ya namna mpya ya kuwa Kanisa katika millennia ya tatu.

Baba Mtakatifu Benedikto XVI anabainisha kuwa mazingira ya sasa na mabadiliko makubwa kiutamaduni na kijamii yanapelekea uhitaji na mtazamo mpya kiunjilishaji. Anataja kwa mfano, mfumo wa tangu zamani uliozoeleka hadi leo wa kuligawa Kanisa katika nchi za Kikristu na nchi za Missioni umepitwa na wakati wala hautoi tena picha halisi ya Kanisa la Kiulimwengu lenye utume mmoja wa kumtangaza Kristo kwa Mataifa yote. Badala yake anapendekeza kufanyike mabadiliko mbadala kifikra na kimtazamo katika Kanisa kwa kuzingatia maisha ya Kanisa na Imani bila kuathiri utume msingi wa Kanisa yaani Uinjilishaji.

Kanisa kwa namna zake zote lazima libaki daima kama Kanisa mahalia na familia ya watu wa Mungu anasisitiza Baba Mtakatifu Benedikto XVI. Hata katika mazingira magumu ya kuhujumiwa Kanisa lazima lisipoteze ujumbe wake wa upendo wa Mungu kwa watu wake kwa kuwa daima karibu na watoto wake katika maisha yao ya kila siku likimpeleka Kristu aliyeteseka miongoni mwa waumini. Kanisa linaalikwa kuwaendea watu wa Mungu mahali na mazingira yoyote walipo na kutoa majibu kwa maswali makuu ya maisha na kurudisha tumaini kwa waliolikosa na kurudisha tena furaha ya watu hawa hata katika mahangaiko yao.

Baba Mtakatifu kwa namna ya pekee amelitaka Kanisa katika nchi za magharibi kujikita zaidi katika uinjilishaji mpya kwani ndio eneo hasa ambalo hapo mwanzo lilipokea imani na kushamiri na kuwa sababu ya kuwepo kwa imani hiyo maeneo mengi ulimwenguni kupitia makundi makubwa ya wamissionari kutoka eneo hilo. Leo hii hali imebadilika kinyume chake.

Imani ya Kristo imepoteza ladha kwa kiwango kikubwa au imekuwa sababu ya migogoro na chuki miongoni mwa wanajamii. Kumbe iko haja ya kuinjilisha upya ili kufufua tena ile imani iliyopandwa hapo zamani kwa sala na sadaka kubwa. Kuna haja ya kubuni mbinu ya kuwepo kwa Kanisa hata katika mazingira yaliyopoteza uchaji wa Mungu na hivyo dini kukosa nafasi katika maisha ya mtu.

Baba Mtakatifu anaendelea kubainisha zaidi tema ya Uinjilishaji Mpya akizingatia utume msingi wa Kanisa ambao anasema utabaki vilevile miaka nenda rudi, Unjilishaji wa Mataifa yote kuwa wanafunzi wa Yesu. Tunapozungumazia uinjilishaji mpya anasema Baba Mtakatifu inamaanisha tu kuwa haiwezekani kwa mfano nchi za Kikristo kuendelea kuinjilisha nchi zingine zikisahau makundi makubwa ya wasio wakristu nyumbani.

Kumbe, nyakati hizi ni zama za kurudi nyuma na kuimarisha wale walio nyumbani. Kwa uinjilishaji mpya Kanisa linaingia katika kipindi kipya chenye changamoto mpya ma mtindo mpya wa uinjilishaji ambapo ujumbe unabaki ule ule kwani Kristo ni Yule Yule: Jana, Leo na hata Milele.

Uinjilishaji mpya anendelea kubainisha Baba Mtakatifu, ni jina linalotajwa kuonesha utume wa Kanisa katika mtindo mpya katika mazingira mapya ya sasa. Uinjilishaji mpya unaligusa Kanisa zima linaporudi mahali lilipo na kuthathmini hali halisi ya ushuhuda wa imani miongoni mwa watu wake bila kuangalia maeneo fulani tu ya kuinjilisha. Kanisa mahalia sasa linaalikwa kujikita zaidi na uimarishaji wa imani nyumbani au mahali pale lilipo.

Uinjilishaji mpya unalenga kumpeleka Kristo ulimwenguni kumbe Kanisa zima linahusika: Kanisa katika nchi za Kikristo liendelee kupambana na tatizo la uasi dini miongoni mwa waumini wake wakati katika nchi za kimissionari, Kanisa liendelee na utamadunisho ili mradi Imani iendelee kutoa mwanga, na mwelekeo sahihi na uzima kwa watu wa Mungu popote pale walipo.

Mpendwa msikilizaji kufikia hapo tumefikia mwisho wa kipindi chetu kwa siku ya leo. Tuendelee kuwa wasikivu na macho kusikiliza na kusoma yale tunayoalikwa kuyatekeleza kutoka katika Sinodi ya Uinjilishaji Mpya. Mungu akubariki sana, nikikuaga kutoka Studio za Radio Vatican, ni mimi mtayarishaji na msimulizi wako Padre George wa Bodyo.











All the contents on this site are copyrighted ©.