2012-11-06 07:33:05

Kumbu kumbu ya miaka 125 ya Kampeni ya Kardinali Lavigerie dhidi ya biashara haramu ya utumwa Barani Afrika


Wamisionari wa Afrika (White Fathers) na Masista Wamisionari wa Mama yetu Malkia wa Afrika (White Sisters) watasherehekea kumbukumbu ya miaka 125 ya kampeni ya mwanzilishi wao, Kardinali Lavigerie Charles, ya kupambana na Biashara haramu ya Utumwa Barani Afrika. RealAudioMP3

Kumbukumbu hii itazinduliwa tarehe 11 Novemba 2012 katika Kanisa la Gesù, lililoko mjini Roma kwa Ibada ya Misa Takatifu itakayoongozwa na Askofu mkuu Michael Fitzgerald, Balozi wa Vatican nchini Misri na itafungwa hapo tarehe 8 septemba, 2013, mjini Ouagadougou, Burkina Faso. Kauli mbiu inayoongoza maadhimisho haya kwa mwaka huu ni: "Mimi ni mwanadamu na hakuna chochote cha kibinadamu kilicho kigeni kwangu."

Sababu za kuadhimisha kumbukumbu hii:

Kwanza kabisa ni kutoa shukrani kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya mafanikio ya kampeni hii. Licha kufutwa kwa biashara haramu ya binadamu, lakini bado kuna uwepo na ongezeko la aina mpya za utumwa mamboleo katika jamii nyingi duniani. Ni vitendo vinavyodhalilisha utu na heshima ya binadamu, kama ilivyokuwa wakati wa biashara haramu ya utumwa, miaka mia moja na ishirini na mitano iliyopita.

Hii ni changamoto ya kuimarisha tafakari na dhamira zetu kuhusu kusimama kidete kulinda na kutetea haki na amani, hasa katika mapambano dhidi ya utumwa mamboleo, tukifuata nyayo za Mwanzilishi wetu. Zaidi ya hayo, tutafanya kumbukumbu hii pamoja na Kanisa zima ambalo lilimkabidhi Kardinali Lavigerie utume huu, kupitia kwa Baba Mtakatifu Leo XIII hapo tarehe 21 Mei 1888.

Kampeni ya Kardinali Lavigerie ya kupambana na utumwa Barani Afrika
Kabla ya uzinduzi wa kampeni hii:

Kardinali Lavigerie alikutana na waathirika wa mauaji ya kinyama nchini Lebanon na Syria yaliyotokea kunako mwaka 1860. Alifanikiwa kukutana na waathirika wa baa la njaa nchini Algeria kunako mwaka 1868. Aliguswa kwa namna ya pekee na waathirika wa biashara ya utumwa iliyokuwa inatendeka Kusini mwa Algeria, kwa mfano Laghouat na Ouargla. Kuanzia mwaka 1872 na kuendelea na Afrika ya Masharaki kupitia kwa shuhuda za wamisionari wake, kuanzia mwaka 1879 na kuendelea.

Baada ya kusikia kwa kina na mapana, kuna haja ya kutekeleza mambo yafuatayo kwa ajili ya kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Watu wawaonjeshe jirani zao moyo wa huruma kwa njia ya huduma kwa waathirika. Kuna haja ya kuendeleza juhudi za kuwakomboa watu kutoka katika utumwa mamboleo, hasa miongoni mwa watoto, wanawake na vijana kwa kutoa elimu makini.

Neno huruma lilikuwa ni kati ya maneno aliyoyatumia kwenye Nembo yake. Ni Kiongozi aliyeguswa na mahangaiko ya watu kiasi kwamba, utume wake mzima, ulikereka na vitendo vya kunyanyasa utu na heshima ya binadamu. Kardinali Lavigerie alitambua kwamba, huruma peke yake ilikuwa haitoshi kuliokoa Bara la Afrika kutoka katika biashara haramu ya utumwa. Ndiyo maana kwa busara ya kichungaji alipenda kuunganisha upendo na huduma kama sehemu ya mchakato wa kupambana na hatimaye, kung’oa kabisa mizizi iliyopelekea uwepo wa biashara haramu ya utumwa.

2. Kampeni yake: 1888-1892

Katika mpango wake wa 'Uinjilishaji wa Afrika" miaka kumi kabla ya kampeni hii, Lavigerie alikuwa tayari amependekeza "kukomesha biashara ya watumwa" kama moja ya njia za uinjilishaji huo. Alitumia fursa ya kukomeshwa kwa biashara ya utumwa nchini Brazil kwa kumwomba Baba Mtakatifu Leo XIII, ashutumu vikali biashara haramu ya watumwa Barani Afrika, katika Waraka wake wa kichungaji ”In Plurimis” aliouandika kwa ajili ya tukio hilo hapo tarehe 5, Mei, 1888. Baba Mtakatifu akamkabidhi dhamana ya kupambana na biashara haramu ya utumwa Barani Ulaya, kuanzia tarehe 21 Mei, 1888.

Lengo la kampeni hii, lilikuwa ni kukomeshwa biashara ya watumwa Kusini mwa Jangwa na Sahara. Ili kufanikiwa ilimbidi kuwajengea watu uwezo kwa njia ya Kampeni kwa watu wanaoishi Barani Ulaya kwa ajili ya watu wa Afrika. Aliwataka wananchi wa Bara la Ulaya kuzishirikisha Serikali zao kwa kuonesha madhara ya biashara haramu ya utumwa, ili kuchukua hatua za kisheria dhidi ya nyanyaso hizi kwa utu na heshima ya binadamu pamoja na kuhakikisha kwamba, sheria hizi baada ya kutungwa, zinatekelezwa.

Kardinali Lavigerie alipata msukumo wa pekee kupambana na biashara haramu ya binadamu kwa kuzingatia sheria asilia na sheria za Kimungu, akajitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kupambana na madhulumu haya, akisukumwa na ubinadamu na uelewa wake katika masuala ya kidini. Utumwa unapingana na kweli za Kiinjili, sheria asilia na sheria za Kimungu. Haya ni masuala yanayogusa imani, akili, haki, heshima, upendo na uhuru wa mtu.

Alithamini ubinadamu wake na kwake, hakuna chochote cha kibinadamu ambacho kilikuwa ni kigeni kwake. Uonevu huu ulikuwa unatia kasoro katika asili ya maisha yake. Angependa watu kumpatia uhuru, heshima kwa kuthamini pia utakatifu wa maisha ya Familia.

Alitamani kuona kwamba, watu waliokombolewa kutoka utumwani wanarejeshewa furaha, thamani ya familia, heshima na uhuru wao. Kardinali Lavigerie anatambua Sheria ya kiungu kwamba: Mungu ni Muumba na Mkombozi wa watu wote. Binadamu wameumbwa kwa mfano wake na sura yake, huu ndio msingi wa heshima, utu na haki ya binadamu inayokiukwa na biashara haramu ya utumwa.

Mbinu alizotumia katika kufanikisha kampeni yake ni pamoja na mikutano ya kitaifa na kimataifa. Akaandika: barua, makala na taarifa kwa ajili ya kusambaza kwenye vyombo vya habari, ili kuwafikia watu wengi zaidi. Alisimamia uanzishwaji wa vyama vya kupambana na biashara haramu ya utumwa Barani Ulaya. Alianzisha huduma za kijamii hasa elimu na afya kwa afya kwa watoto waliokombolewa kutoka utumwani.

Aliendelea kutegemea sana Sala kama moja ya nyenzo muhimu katika Kampeni hii. Kwake, Uinjilishaji Barani Afrika ulikuwa unakwenda sanjari na utoaji wa elimu pamoja na kuwashirikisha wanawake katika kampeni hii, jambo ambalo halikuwa rahisi sana kwa wakati huo, kutokana na mfumo dume kuendelea kutawala.

3. UTUMWA MAMBOLEO

Kwa ujumla, tunaweza tukasema kwamba, kitu au jambo lolote linalodhalilisha na kukiuka: heshima, hadhi na haki msingi za binadamu ni utumwa, bila kujali: jinsia, rangi, imani au dini ya mtu. Orodha ya utumwa mamboleo ni kubwa sana, kwani inazihusisha pia taasisi ambazo zinajikuta zinawatumbukiza watu katika utumwa: hizi ni pamoja na kazi za suluba, madeni makubwa, biashara haramu ya binadamu, utumwa ndani ya familia pamoja na kambi za kazi za suluba Na ndani ya makundi hayo tunaweza kuorodhesa vitendo vya utumwa kama vile ajira ya watoto wadogo, biashara haramu ya ngono pamoja na ndoa za shuruti.

4. Mapambano na aina mpya za utumwa: Msukumo kutoka Kardinali Lavigerie

Tunapenda kufuata nyayo za Kardinali Lavigerie katika kupambana na utumwa mamboleo katika mikakati na mipango yetu ya kichungaji, kwa kuzingatia kwanza kabisa maisha ya sala kama chemchemi ya kuzuia, ili hatimaye kung’oa mizizi ya biashara haramu ya utumwa; kuweka mikakati ya kuzuia kwa kuwawezesha watu: kiakili na kiimani. Ni jukumu la wadau mbali mbali kuhakikisha kuna utekelezaji na sheria zinatekelezeka.

Waathirika wapewe ulinzi pamoja na kujengewa uwezo wa kujitegemea, ili kuheshimu hadhi na utu wao kama binadamu. Ili kufanikisha mapambano haya anasema kardinali Lavigerie, kuna haja ya kujenga umoja na mshikamano wa dhati na wadau mbali mbali, kwani vitendo hivi ni kinyume kabisa cha utu na heshima ya binadamu; ni kinyume cha sheria asili inayowagusa watu wote bila ubaguzi wowote ule. Mshikamano huu unajikita si tu katika mambo ya imani, akili, bali unagusa kwa namna ya pekee, haki, heshima, upendo na uhuru wa mtu.

5. Dhamira zakuzingatia wakati wa mwaka huu (2012-2013)

Katika mwaka huu 2012 hadi 2013: Kumbukumbu na tafakari yetu itazingatia masuala yafuatayo: Utumwa wa watoto, Haki za Binadamu Barani Afrika, Biashara haramu ya binadamu, Upokonyaji wa ardhi, Uhamiaji na Umaskini.

6. Kalenda

Maadhimisho haya yatafuata Kalenda ya Shirika katika Makanisa mahalia, yaani kadiri ya mipango ya Kanda za Wamissionari wa Afrika na Masista Wamissionari wa Mama Yetu Malkia wa Afrika sanjari na kuihusisha sekta ya watu binafsi pamoja na waamini walei na vyama vya kitume. Tutakuwa na siku tatu tu za kuzingatiwa na wanachama wote wa Wamisionari wa Afrika na Masista Wamisionari wa Mama yetu Malkia wa Afrika. Siku hizi ni:

11 Novemba 2012: Missa Takatifu ya uzinduzi wa shughuli za mwaka. Mjini Roma tukio hili litaambatana na:Maonesho ya picha za Kampeni ya Kardinali Lavigerie pamoja na picha zinazoonesha utumwa mamboleo. Kutafanyika mkutano kuhusu Kampeni hii pamoja na kuonesha madhara ya biashara haramu ya binadamu.

Tarehe 30 Aprili 2013: Sikukuu ya Mama yetu wa Afrika:Itakuwa ni Siku ya Mafungo itakayoongozwa na dhamiri juu ya ukombozi. Tarehe 8 Septemba, 2013: Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bikira Maria. Maadhimisho ya hitimisho la Kumbukumbu ya miaka mia moja na ishirini na mitano tangu kampeni ya kupinga biashara haramu ya binadamu ilipoanzishwa yatakuwa huko mjini Ouagadougou, Burkina Faso.

Imetafsiriwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.