2012-11-03 08:45:55

Wakenya simameni kidete kulinda, kutetea na kudumisha misingi ya haki, amani na mshikamano wakati wa uchaguzi mkuu 2013


Askofu mkuu Alain Paul Lebeaupin, aliyekuwa Balozi wa Vatican nchini Kenya ambaye hivi karibuni aliteuliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kuwa Balozi wa Vatican kwenye Umoja wa Nchi za Ulaya wenye makao yake makuu mjini Brussels, Ubelgiji, anawataka wananchi wa Kenya kuhakikisha kwamba, uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika nchini humo hapo tahere 4 Machi, unakuwa, huru, wa haki kwa kuzingatia pia misingi ya amani, umoja na mshikamano wa kitaifa.

Askofu mkuu Lebeaupin anawataka wananchi wa Kenya kwa namna ya pekee kuhakikisha kwamba, madhara makubwa yaliyojitokeza kwa watu na mali zao mara baada ya kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka 2007 hayajirudii tena katika historia ya wananchi wa Kenya.

Askofu mkuu Lebeaupin anasema, alifika nchini Kenya kunako mwaka 2005 na katika kipindi chote hiki ameshuhudia mabadiliko makubwa katika maisha ya watu wa Kenya. Anakumbuka kwa namna ya pekee, Kura ya Maoni iliyopelekea kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa, ambayo imesaidia kujenga umoja wa kitaifa, ingawa bado inakabiliwa na changamoto nyingi.

Askofu mkuu Lebeaupin ameyasema hayo katika dhifa iliyoandaliwa kwa niaba yake, hivi karibuni kwa ajili ya kumuaga, baada ya kuhitimisha utume wake nchini Kenya kama Balozi wa Vatican. Anasema kwamba, anaondoka nchini Kenya akiwa na kumbu kumbu hai kabisa ya maisha na utume wake nchini humo, baada ya kuihudumia Familia ya Mungu kwa takribani miaka saba.

Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, amemtakia kheri na baraka pamoja na kupona haraka kutokana na ajali iliyomfika Mwezi Mei, 2012, akiwa mjini Roma. Amempongeza kwa utume wake uliopelekea utekelezaji wa mikakati mingi ya maendeleo: kiroho na kimwili kwa ajili ya maisha ya Kanisa na ustawi wa wananchi wa Kenya katika ujumla wao.









All the contents on this site are copyrighted ©.