2012-11-03 07:59:04

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani na changamoto zake kwa waamini


Askofu mkuu Rino Fisichella, Rais wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji mpya anabainisha kwamba, Mwaka wa Imani uliofunguliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi ni sita mjini Vatican kwa Ibada ya Misa Takatifu, Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya Uinjilishaji mpya sanjari na kumbu kumbu ya Jubilee ya miaka hamsini tangu Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ulipozinduliwa bila kusahau kumbu kumbu ya miaka ishirini tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, alipochapisha kwa mara ya kwanza Katekesimu Mpya ya Kanisa Katoliki, ni matukio muhimu sana katika kuamsha na kukoleza imani miongoni mwa waamini. RealAudioMP3

Hii ni changamoto ya kufanya tafakari ya kina, kuhusu maisha na utume wa Kanisa kwa takribani miaka hamsini iliyopita, bila kuukimbia ukweli na changamoto zinazoendelea kulikabili Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo; yaani tabia ya ukanimungu na watu kupenda mno malimwengu. Wakristo wanapaswa kusimama kidete kuifahamu, kuiungama, kuitetea na kuilinda imani yao. Matukio haya yalenge kukoleza imani kwa Kristo na Kanisa lake, kama njia ya kujipatia wokovu.

Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya Uinjilishaji mpya ni fursa kubwa kwa Mababa wa Sinodi kuweza kupembua changamoto, matatizo na matumaini ya Mama Kanisa katika ulimwengu mamboleo. Mababa wa Sinodi wanatafakari kwa kina, jinsi ambavyo Mama Kanisa anaweza kurithisha, kushirikisha na kuimwilisha imani hiyo katika uhalisia wa maisha ya watoto wake waliotawanyike sehemu mbali mbali za dunia. Ni fursa muhimu kwa Kanisa katika kupambanua njia na mikakati ya kichungaji itakayochukuliwa na Mama Kanisa katika maisha na utume wake kwa miaka ijayo kuanzia sasa.

Askofu mkuu Fisichella anasema, maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya Uinjilishaji mpya yanakwenda sanjari na Mwaka wa Imani, kwani kwa pamoja, matukio haya makuu, yanafumbatwa katika kauli mbiu inayoongoza maadhimisho ya Sinodi juu ya Uinjilishaji mpya, yaani Uinjilishaji mpya ni nyenzo ya utangazaji wa imani ya Kikristo.

Ni mwaka ambao Baba Mtakatifu anapania kuona kwamba, waamini wanaifahamu, iungama na kuishuhudia imani yao katika maisha na vipaumbele vyao, ili hatimaye, jirani zao waweze pia kuonja uzuri wa Injili unaojionesha katika maisha ya Wakristo. Ni mwaliko kwa waamini hawa kukuza na kuimarisha uhusiano wao wa dhati na Yesu Kristo Mkombozi wa dunia, kwa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, dhamana ambayo Mama Kanisa amejitwalia kwa takribani miaka elfu mbili iliyopita.

Mama Kanisa anadhamana endelevu ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, kama njia ya kushiriki ujumbe ambao Kristo mwenyewe aliupokea kutoka kwa Baba yake wa mbinguni. Uinjilishaji Mpya ni dhana inayopania kuwawezesha waamini kukabiliana na changamoto mbali mbali katika maisha na utume wao hapa duniani, katika ngazi ya mtu binafsi na jumuiya ya waamini, wanapojitahidi kumtangaza Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu, limbuko lao walio lala katika mauti.

Uinjilishaji mpya unapania kutoa fursa kwa waamini kuonesha imani yao katika maadhimisho ya Ibada na Liturujia mbali mbali zinazoandaliwa na Mama Kanisa, Ushuhuda wa imani hiyo katika uhalisia wa maisha ya waamini kwa njia ya Injili ya upendo.

Mababa wa Sinodi wametafakari kwa kina: matatizo, changamoto na fursa za Uinjilishaji mpya katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo kama vile: tabia ya ukanimungu, tatizo la wakimbizi, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, hali ya uchumi kimataifa, kumong’onyoka kwa misingi ya maadili na utu wema; njia za mawasiliano ya jamii na changamoto na fursa zake.

Yote haya yanaweza kupata ufanisi mkubwa kwa waamini wenye kujibidisha kumwilisha ndani mwao tunu msingi za maisha ya Kikristo na Mapokeo yake. Waamini hawana budi kutubu na kuongoka, kama njia ya kumkaribisha Kristo aweze kufanya hija ya maisha pamoja nao! Mama Kanisa hana budi kuendeleza juhudi za utamadunisho, changamoto iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ili kweli, imani iweze kumwilishwa.

Jambo la msingi anasema Askofu mkuu Fisichella ni toba na wongofu wa ndani; ushuhuda wa imani unaojionesha katika vipaumbele vya maisha ya mwamini, kwa kutambua kwamba, Mama Kanisa anawaalika kuishi kwa namna ya pekee, utume wao kama sehemu ya historia ya wokovu, daima wakijitahidi kusoma alama za nyakati.

Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, Mama Kanisa amefanikiwa kujenga mang’amuzi na uwezo mkubwa katika azma ya Uinjilishaji, umefika wakati sasa kuhakikisha kwamba, mang’amuzi haya yanafanyiwa kazi kwa ajili ya utume na ustawi wa Kanisa sehemu mbali mbali za dunia. Juhudi hizi zianzie kwa namna ya pekee, ndani ya mtu binafsi, familia, parokia na vyama vya kitume, kila mwamini apanie kuonesha ushuhuda wa imani yake, kwani kila mwamini kwa hakika ni mwinjilishaji, dhamana na wajibu aliojitwalia kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo.








All the contents on this site are copyrighted ©.