Baba Mtakatifu atembelea na kusali kwenye Makaburi ya Mapapa chini ya Kanisa kuu la
Mtakatifu Petro, mjini Vatican
Katika maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Marehemu wote, hapo tarehe 2 Novemba, 2012, majira
ya jioni, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, alikwenda kutembelea na kusali
kwa kitambo kwenye makaburi ya Mababa Watakatifu yaliyoko chini ya Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro, mjini Vatican.
Baba Mtakatifu aliwaalika wale waliokuwa wameandamana
naye wakati wa kutembelea makaburi hayo kuwaombea viongozi hawa wa Kanisa huruma na
upendo wa Mungu, wakati huu wakiwa wamelala katika usingizi wa amani, wakiwa na tumaini
la ufufuko wa uzima wa milelle. Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu aliwakumbuka Mapapa
ambao walijitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kuiongoza Familia ya Mungu, ili waweze
kushiriki liturujia ya mbinguni.
Siku ya kuwakumbuka na kuwaombea Marehemu
Wote imetumiwa na waamini sehemu mbali mbali za dunia, kutembelea, kusali pamoja na
kusafisha makaburi, kama njia ya kuwaenzi waamini hao ambao wametangulia mbele ya
haki wakiwa na tumaini la uzima wa milele.