"Angalieni Fumbo la Kifo kwa jicho la imani na matumaini kwa Mungu aliyewaumba na
kuwakomboa"
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumamosi tarehe 3 Novemba 2012 ameadhimisha
Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea Marehemu Makardinali
na Maaskofu waliofariki dunia kuanzia mwezi Novemba 2011 hadi Oktoba 2012, kutoka
sehemu mbali mbali za dunia.
Liturujia ya kuwaombea wafu pamoja na kutembelea
makaburi, imekuwa ni fursa kwa waamini kuweza kuonesha ule uhusiano uliopo kati yao
na marehemu wao. Makaburi ya marehemu ni kioo cha maisha yao hapa duniani, mwaliko
wa kuendeleza majadiliano kuhusu kifo ambacho kimeendelea kuleta mahangaiko makubwa
katika maisha ya mwanadamu.
Makaburi anasema Baba Mtakatifu ni mahali ambapo
watu wanakutana na marehemu ndugu zao, ili kuendeleza umoja ambao kifo kamwe hakiwezi
kuutenganisha. Mjini Roma kwa namna ya pekee, kuna Makaburi ya zamani yanayoonesha
kwa namna ya pekee, uhusiano endelevu uliopo na Ukristo tangu awali.
Mtu anapotembelea
makaburi inakuwa kana kwamba, anaendeleza mawasiliano na wale ambao wametangulia mbele
ya haki; watu ambao walionja furaha, huzuni, kushindwa na matumaini, kwani kifo kinamgusa
kila mtu na makali yake yanabaki vile vile hata baada ya miaka nenda miaka rudi.
Baba
Mtakatifu anawaalika waamini kuliangalia Fumbo la Kifo kwa Jicho la Imani na Matumaini
kwa Mwenyezi; matumaini ambayo yanabubujika kutokana na kifo na ufufuko wa Yesu Kristo,
kiasi cha kumfungulia mwamini mlango wa maisha ya uzima wa milele ili kujenga umoja
na Mwenyezi Mungu aliye hai pamoja na jirani aliowaumba na kuwakomboa. Hili ni jibu
makini la matumaini kwa upendo wa Mungu unaong'ara juu ya Msalaba wa Kristo; mwaliko
wa kujiunga naye ili kupata uzima wa milele.
Katika imani na sala, Baba Mtakatifu
amewakumbuka na kuwaombea Marehemu Makardinali kumi na Maaskofu mia moja na arobaini
na tatu waliofariki dunia katika kipindi cha mwaka 2011 hadi Oktoba 2012. Amewaombea
marehemu wote hawa ili waweze kupata tuzo ambalo Mwenyezi Mungu amewaahidia Wahudumu
wa Injili. Hawa ni watu waliojivika kwa dhati kabisa kheri za mlimani, muhtasari wa
mafundisho makuu ya Yesu.
Ni viongozi waliolihudumia Kanisa kwa uaminifu na
upole hata wakati mwingine walikabiliana na magumu katika maisha na utume wao, lakini
wakasimama kidete kuwalinda na kuwatetea Wanakondoo waliokabidhiwa kwao na Mama Kanisa.
Ni viongozi waliojitahidi kukesha, wakijitoa kimasomaso kwa ajili ya ujenzi wa Ufalme
wa Mungu; ni watu ambao wamekuwa na mchango mkubwa wa mabadiliko ndani ya Kanisa mintarafu
Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.
Baba Mtakatifu anaendelea kusema kwamba, hawa
ni viongozi ambao daima walishiriki Karamu ya Bwana na kwa sasa wanashiriki Karamu
ya Yerusalemu ya Mbinguni. Sala ya Kanisa inalenga kuwaombea viongozi wote hawa ili
kweli waweze kushiriki katika uzima wa milele, kielelezo cha ushindi wa Kristo dhidi
ya nguvu ya kifo, kama alivyojionesha mwenyewe Siku ile ya Kwanza ya Juma, alipofufuka
kutoka katika wafu.
Kwa njia ya Ubatizo, waamini wanakufa na Kristo na wana
matumaini kwamba, wataweza kuishi pamoja naye, kama alivyowaahidia; hili ni tumaini
linalobubujika kutoka katika upendo wa Kristo; ni tumaini ambalo kamwe haliwezi kudanganya.
Mwenyezi Mungu mwingi wa huruma kwa njia ya kifo cha Mwanaye mpendwa aliweza kuwapatanisha
naye wakati walipokuwa wangali dhambini. Wanahesabiwa haki kutokana na imani yao kwa
Yesu Kristo, Mtu mwenyehaki aliyetangazwa katika Maandiko Mataktifu na kwa njia ya
Fumbo la Pasaka, waamini wanaweza kumwona Mwenyezi Mungu na hivyo kuuutafakari uso
wake.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, viongozi hawa wa Kanisa walipendwa kwa
namna ya pekee na Bikira Maria, aliyewaonjesha upendo wa Kimama. Baba Mtakatifu anatumia
fursa hii kumkabidhi roho za viongozi hao marehemu, ili aweze kuwaelekeza kwenye Ufalme
wa Mungu, ambao waliufanyia kazi walipokuwa hapa duniani.