2012-11-02 07:58:46

Nia za Papa kwa Mwezi Novemba 2012


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika nia zake za jumla kwa Mwezi Novemba, anayaelekeza mawazo yake kwa mihimili na wahudumu wakuu wa Injili ambao ni Maaskofu na Mapadre kuwa na ujasiri kiasi cha kutolea ushuhuda makini na aminifu kwa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka. Kutujuvya zaidi ni Sr. Gisela Upendo Msuya. RealAudioMP3

Katika nia zake za Kimissionari anawaalika waamini kuliombea Kanisa linalosafiri hapa duniani liweze kung’ara miongoni mwa Mataifa, ili hatimaye, Mataifa yaweze kutembea katika mwanga wake.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika barua yake kwa Majandokasisi wakati wa kufunga Mwaka wa Mapadre, anasema kwamba, licha ya magumu, changamoto, matatizo na fursa mbali mbali zilizojitokeza katika maisha na utume wa Kanisa, lakini bado kuna haja ya kuwa na Makleri wanaojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya: Kutangaza Injili ya Kristo na Kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa.

Hii ni kutokana na ukweli kwamba, hata katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknlojia, bado watu wataendelea kuwa na kiu ya uwepo wa Mungu katika maisha yao. Pale ambapo watu wanadhani kwamba, hawamhitaji Mungu, hapo kuna utupu na ubatili na matokeo yake ni kinzani na vurugu za maisha ambazo zinaathari kubwa kwa maisha, ustawi na maendeleo ya vijana. Baba Mtakatifu anasema Mungu ni hai na amemuumba na anamfahamu kila mtu. Hata leo hii bado anaendelea kuita Mapadre watakaojitoa kimasomaso kutangaza Injili ya Kristo hadi ukamilifu wa dahali.

Katika miaka ya hivi karibuni, Kanisa limeshuhudia baadhi ya viongozi wake wakikumbwa na kashfa ya unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya watoto wadogo; ni vitendo vya aibu na vilivyolipaka matope Kanisa, kiasi cha baadhi ya watu kuhoji umuhimu wa useja na usafi wa moyo katika maisha ya Kanisa. Licha ya vitendo vyote hivi anasema Baba Mtakatifu, bado wito na utume wa Kipadre unahitajika. Hawa ni viongozi wenye imani hai inayoonesha ukomavu wao wa kiutu hasa katika useja na usafi wa moyo. Ni changamoto ya kuwa makini kutambua na kuishi wito wa maisha ya kipadre.

Makleri ni wahudumu wa Mafumbo ya Kanisa wanaopaswa kutolea ushuhuda wa Imani yao kwa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Sakramenti ya Daraja Takatifu ni kielelezo makini cha uwepo endelevu wa Kristo kati ya wafuasi wake. Ni Kristo mwingine, changamoto ya kuhakikisha kwamba, matendo na maisha yao yanamfanana Kristo, kwani kinyume chake ni ubatili mtupu!

Kutokana na changamoto zote hizi, ndiyo maana Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anawaalika waamini kuungana pamoja naye kusali kwa ajili ya kuwaombea Makleri, ili kweli waweze kuwa ni wahudumu amini, wenye ujasiri wa kutolea ushuhuda wa kweli kuhusiana na maisha na wito wao wa Kipadre, daima wakiwa waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika nia zake za Kimissionari kwa Mwezi Novemba, 2012, anawaalika waamini kuliombea Kanisa linalosafiri hapa duniani ili liweze kuwa ni mwanga wa mataifa ili yaweze kutembea katika mwanga huu na hatimaye, kufikia utimilifu wa maisha, kwa kuonesha umoja na mshikamano kama Familia ya Mungu. Kanisa katika hija yake hapa duniani, linapania kuwaonesha watu njia inayokwenda kwa Kristo, Mkombozi wa Ulimwengu. Kanisa linapania kuwa ni mhudumu wa kweli kwa binadamu, lakini zaidi kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Kila mtu anaalikwa kuupokea mwaliko wa ukombozi na kwamba, kinzani na magumu yote yataponywa na hatimaye kupata ukamilifu wake kwa kujipatanaisha na Kristo aliyemwaga damu yake Msalabani, ili kumkirimia mwanadamu maisha yenye uzima wa milele. Ndiyo maana hata leo hii, Kristo anaendelea kuita na kuwatuma watu kutangaza Ufalme wa Mungu, ili Mataifa yaweze kuwa kweli ni Watu wa Mungu. Kwa Kanisa kutangaza Habari Njema ya Wokovu ni dhamana nyeti na endelevu kama ilivyokuwa kwa Mtakatifu Paulo, Mwalimu wa Mataifa.

Kanisa linalosafiri hapa duniani ni mbegu ya matumaini na mwendelezo wa huduma ya Kristo kwa Walimwengu, ili waweze kufikia uzima wa milele; wakiendelea kusimama kidete kulinda na kutetea haki, amani, uhuru, utu na heshima ya kila binadamu. Mama Kanisa anapania kutangaza Injili ya Upendo hadi miisho ya dunia, ili mwanga wa Injili uweze kuleta mabadiliko yanayokusudiwa kwa njia ya huduma na utume.

Mama Kanisa anaendelea kuwaalika watu wote waweze kushiriki katika hija ya Wokovu iliyoanzishwa na Mwenyezi Mungu kwa njia ya Neno wa Mungu aliyefanyika Mwili. Ndiyo maana Kanisa bado linaendelea kujikita katika Uinjilishaji wa Awali, miongoni mwa watu ambao bado hawajasikia Habari Njema ya Wokovu, hadi pale kila kitu kitakapopata utimilifu wake ndani na kwa njia ya Kristo Yesu.

Hii ni changamoto kwa Waamini kuendelea kutolea ushuhuda wa Imani yao hata ikibidi kuyamimina maisha yao kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Waamini kwa namna ya pekee, wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuwa kweli ni chumvi na mwanga wa mataifa kwa kutambua kwamba, Uinjilishaji bado ni kati ya vipaumbele vya Mama Kanisa.








All the contents on this site are copyrighted ©.