2012-10-31 09:07:12

Wakenya: salini ili kuombea uchaguzi mkuu, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa!


Askofu Salesius Mugambi wa Jimbo Katoliki Meru, Kenya, Jumapili iliyopita, tarehe 28 Oktoba 2012, wakati wa maadhimisho ya Ekaristi Takatifu, aliwaalika waamini na wananchi wa Kenya katika ujumla wao, kuombea uchaguzi nchini humo, unaotarajiwa kufanyika hapo tarehe 4 Marchi 2013, ili uweze kuwa: huru, wa haki, amani na utulivu sanjari na kuombea maboresho ya ulinzi na usalama nchini Kenya.

Jumapili iliyopita ilikuwa ni Siku ya kusali kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa ajili ya Vikosi vya Ulinzi na Usalama na Familia zao nchini Kenya na imeongozwa na kauli mbiu "Ili wote wawe wamoja". Askofu Mugambi ambaye amewataka Wanajeshi wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama kutekeleza wajibu wao kwa umakini na uchaji mkubwa, daima wakimtegemea Mwenyezi Mungu katika maisha yao ya kila siku.

Kwa njia hii, Kenya inaweza kugeuka na kuwa kweli ni nchi ya Wachamungu, changamoto inayopaswa kufanyiwa kazi kuanzia kwenye Familia na katika maeneo mbali mbali ya kazi, lengo ni kuyatakatifuza malimwengu.

Itakumbukwa kwamba, kabla ya mabadiliko yaliyofanyika kwenye Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, mshauri wa kiroho kwa Wanajeshi wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama nchini Kenya, alikuwa ni Askofu Philip Anyolo, ambaye hivi karibuni alichaguliwa kuwa ni Makamu wa Rais Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya. Yeye alifanya utume huu kwa takribani miaka kumi na minne na kwa hakika anastahili kupewa pongezi za dhati.

Kwa upande wake, Askofu Anyolo amemtakia ufanisi, tija na mafanikio mema katika utumishi wake huu mpya kwa ajili ya vikosi vya ulinzi na usalama na anawaalika wanajeshi kuunga mkono juhudi za Kanisa katika kulinda, kutetea na kuimarisha: haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa miongoni mwa wananchi wa Kenya.

Akizungumza katika maadhimisho haya, Rais Mwai Kibaki, Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama nchini Kenya, amelishukuru Kanisa kwa huduma ya maisha ya kiroho wanayoitoa katika vikosi vya ulinzi na usalama. Amekazia zaidi nidhamu na umakini kwa wanajeshi; daima wakijitahidi kujenga na kuimarisha mshikamano na umoja wa kitaifa ambao kwa miaka ya hivi karibuni ulitikiswa vibaya sana, lakini zaidi, wakati huu, Kenya inapojiandaa kwa ajili ya uchaguzi mkuu.

Ni matumaini ya Rais Kibaki kwamba, Kanisa nchini Kenya, litaendelea kuchangia kwa hali na mali katika kukuza na kuimarisha amani, umoja na mshikamano wa kitaifa. Kwa wanajeshi wanaalikwa kwa namna ya pekee kuwa makini na watu wanaotaka kuwagawa Wakenya kwa masilahi yao binafsi.







All the contents on this site are copyrighted ©.