JK: achonga na kusema "Naridhishwa na Kazi ya Tume ya Katiba"
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa anaridhishwa
na mwenendo mzima wa kazi ya Tume ya Kukusanya na Kuratibu Maoni ya Wananchi Kuhusu
Katiba. Aidha, Rais Kikwete amewataka wajumbe wa Tume hiyo kuwakumbusha wananchi kutokutoa
maoni kwa kutumwa na watu wengine bali watoe maoni yao wenyewe kwa kadri wanavyotaka
Katiba yao mpya iwe.
Rais Kikwete ameyasema hayo Jumanne, Oktoba 30, 2012,
kwenye Ikulu Ndogo mjini Mwanga, Mkoa wa Kilimanjaro wakati alipokutana na kuzungumza
kwa muda mfupi na baadhi ya wajumbe wa Tume hiyo wakiongozwa na Profesa Baregu Mwesiga
ambao walikwenda kumjulia hali Rais. Rais Kikwete yuko katika ziara ya siku tatu katika
Mkoa wa Kilimanjaro.
Wajumbe hao wanne ambao walikutana na Rais Kikwete ni
sehemu ya wajumbe wa Tume ambao wako mkoani Kilimanjaro kukusanya na kuratibu maoni
ya wananchi wa mkoa huo kuhusu Katiba. Watakuwa Kilimanjaro hadi tarehe 6 Novemba,
2012.
Rais Kikwete amewaambia wajumbe hao: “ Kwa maoni yangu nadhani kazi ya
Tume inakwenda vizuri na mimi nawatakia kila heri katika shughuli hii muhimu kwa mustakabali
wa taifa letu. Zitakuwepo changamoto, lakini hizo hazikosi katika shughuli yoyote
ya binadamu.”
Aliongeza Rais Kikwete: “Nawaomba tu muendelee kuwaelimisha wananchi
kuwa ni vizuri kwao kutoa maoni yao wenyewe siyo kwa kutumwa na watu wengine. Wahasishwe
wasiwe kaseti za kucheza maoni ya watu wengine.”
Profesa Baregu amemwambia
Rais Kikwete kuwa kazi ya Tume hiyo inakwenda vizuri na wajumbe wa Tume wanayo matumaini
makubwa kuwa kazi hiyo itakamilishwa katika kipindi kilichokubaliwa. “Tunaweza kusema
kuwa tunakaribia kumaliza robo tatu ya kazi ya kukusanya maoni ya wananchi.”
Profesa
pia amemwambia Rais Kikwete kuwa ni kweli wajumbe wa Tume hiyo wanakumbana na watu
ambao wanatumika kama kaseti za watu wengine. “Ni kweli wapo. Mwanzoni walikuwa wengi
lakini sasa tunaona kuwa wanaanza kupungua.”