2012-10-29 07:34:14

Mababa wa Sinodi wameonesha unyenyekevu wa hali ya juu, daima wamejitahidi kusoma alama za nyakati, sasa ni kipindi cha kumwilisha changamoto hizi katika maisha na utume wa Kanisa!


Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya katika ujumbe wao kwa Watu wa Mungu sehemu mbali mbali za dunia, wanawahimiza waamini kwa namna ya pekee, kuhakikisha kwamba, wanauhisha imani yao ili isimezwe na malimwengu. Wajitahidi kutafuta fursa za kukutana na Mwenyezi Mungu anayejifunua kwa namna ya pekee, kama kielelezo cha upendo unaojidhihirisha ndani ya Kanisa kama Jumuiya inayosimikwa katika misingi ya Umoja na Mshikamano. RealAudioMP3

Kutokana na dhamana hii, Waamini wanaalikwa kutolea ushuhuda umoja uliopo kati yao. Mababa wa Sinodi wanabainisha kwamba, ili Wakristo waweze Kuinjilisha, kwanza kabisa hawana budi Kujiinjilisha wao wenyewe, ili ujumbe wao uweze kuwa na mvuto pamoja na mguso kwa wale watakaokutana nao katika hija ya maisha yao. Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, wanajikita katika toba na wongofu wa ndani unaowawezesha kuyaona, kukiri na hatimaye, kujiwekea mikakati ya maboresho katika mchakato mzima wa Uinjilishaji Mpya.

Askofu Salutaris Libena wa Jimbo Katoliki Ifakara, Tanzania alikuwa Mwakilishi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania waliokuwa wanahudhuria kwenye Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya. Anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumkirimia fursa hii ya kuweza kusali, kutafakari, kusikiliza na kushirikishana mang’amuzi, changamoto, fursa na matumaini ya Kanisa kwa sasa na kwa siku zijazo.

Askofu Libena anasema, jambo ambalo limemgusa kwa namna ya pekee, katika maadhimisho ya Sinodi ya Uinjilishaji Mpya kama njia ya kutangaza Imani ya Kikristo ni jinsi ambavyo Mababa wa Sinodi walivyoonesha unyenyekevu wa hali ya juu kabisa, kwa kusoma alama za nyakati, wakitambua kwamba, huu ndio muda muafaka wa kuamsha ari na mwamko katika azma ya Uinjilishaji Mpya; kwa kukazia toba, wongofu wa ndani na utakatifu wa maisha; kwa kujikosoa na kukosoa, ili kuibua mbinu mkakati unaopania maboresho ya Uinjilishaji Mpya, kama sehemu ya utekelezaji wa Agizo la Kristo la kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia.

Dhamana ya Uinjilishaji Mpya ni changamoto inayotakiwa kwanza kabisa kutekelezwa na Wainjilishaji mihimili ili waweze kuinjilisha kwa umakini mkubwa na kwamba, Uinjilishaji ni wajibu fungamanishi kwa Wafuasi wote wa Kristo.

Mababa wa Sinodi wamekiri kwa unyenyekevu kwamba, katika maeneo ambayo Kanisa halijafanya vyema sana ni katika maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa. Wakristo wanapaswa kujipanga vyema na kwa umakini mkubwa ili maadhimisho haya yaweze kuleta mvuto na mguso kwa makundi ya vijana na wanaume ambao mara nyingi wamekuwa wakisua sua katika kushiriki katika maisha na utume wa Kanisa. Mahubiri yaandaliwe kwa usafaha na maadhimisho ya Liturujia mbali mbali za Kanisa yamguse mwamini katika undani wa maisha yake: kiroho na kimwili.

Mababa wa Sinodi anasema Askofu Libena kwamba, wamekazia na kuwahimiza Waamini kujichotea utajiri unaobubujika kutoka katika Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, Mafundisho Jamii ya Kanisa na Nyaraka za Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican. Mwaka wa Imani uwe ni fursa ya kuimarisha Imani kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya ushuhuda makini.








All the contents on this site are copyrighted ©.