2012-10-29 10:00:38

Familia za Kikristo na Parokia ni wadau wakuu katika azma ya Uinjilishaji Mpya katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo!


Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya katika ujumbe wao kwa Watu wa Mungu wanakazia kwa namna ya pekee, Familia kama kitovu cha mchakato wa Uinjilishaji Mpya, jitihada ambazo zinapaswa kuungwa mkono na Mama Kanisa, Wanasiasa na Jamii katika ujumla wake. Ndani ya Familia, Mababa wa Sinodi wanatambua na kuheshimu mchango na dhamana ya wanawake katika maisha na utume wa Kanisa.

Familia ni shule ya utakatifu, haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli. Lakini Familia katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, zinakabiliwa na vikwazo mbali mbali vinavyolenga kufifisha juhudi za Familia katika utekelezaji wa dhamana yake ya Uinjilishaji Mpya. Familia zikiwezeshwa kikamilifu, ziwatafute hata wale ambao wanalega lega katika imani katika Parokia zao, kwani Familia na Parokia ni wadau wakuu wa Uinjilishaji Mpya.

Wanasikitishwa na hali ngumu wanayokabiliana nayo wanawake kutokana na nyanyaso za kijinsia, mfumo dume pamoja na talaka zinazowafanya kuchechemea katika ushiriki wao wa maisha ya Kisakramenti ndani ya Kanisa. Lakini, wanawake wanapaswa kukumbuka kwamba, licha ya matatizo na changamoto wanazokabiliana nazo katika maisha na utume wao ndani ya Kanisa, kamwe Yesu Kristo, Mkombozi wa Dunia hajawasahau, changamoto kwao kugundua njia mpya za kuweza kumkaribia Yesu katika hija ya maisha yao kama waamini.

Akihojiwa na Radio Vatican, Askofu mkuu Nikola Etrovic, Katibu mkuu wa Sinodi ya Maaskofu anabainisha kwamba, Mababa wa Sinodi wamekazia kwa namna ya pekee, umuhimu wa kuziwezesha Familia na Parokia kutambua, kuthamini na kutekeleza wito na dhamana yao katika mchakato mzima wa Uinjilishaji Mpya. Mababa wengi wa Sinodi wameguswa na ushahidi unaotolewa na Wanawake Wakatoliki sehemu mbali mbali za dunia kutokana na nafasi na dhamana waliyo nayo katika maisha na utume wa Kanisa.

Maadhimisho haya yamechangia kwa namna ya pekee kuamsha tena changamoto iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican unaolitaka Kanisa kujikita katika majadiliano ya Kidini na Kiekumene. Wawakilishi kutoka Makanisa na Madhehebu mbali mbali ya Kikristo yameshiriki kwa kutambua kwamba, Wakristo wote wanayo dhamana ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, licha ya matatizo, changamoto na fursa zilizopo.

Askofu mkuu Nikola Etrovic anakiri kwamba, licha ya idadi kubwa ya Mababa wa Sinodi waliokuwa wanahudhuria kutoa tafakari, mawazo, mchango na changamoto zao, kazi kubwa imekuwa ni kuhariri na kuratibu mawazo yote haya katika hatua mbali mbali hadi kufikia hitimisho la Maadhimisho ya Sinodi yenyewe. Ni kazi ambayo imefanyika katika hali ya ukimya, sala, tafakari na majitoleo ya hali ya juu kutoka katika Sekretarieti ya Sinodi ya Maaskofu.

Hii si kazi haba, kwani jumla kulikuwa na washiriki mia nne na hamsini, kila mtu alikuwa na nafasi na mchango wake katika maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya kama mchakato unaopania kurithisha Imani ya Kikristo katika ulimwengu mamboleo. Anawashukuru na kuwapongeza wadau mbali mbali waliojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kufanikisha maadhimisho ya Sinodi juu ya Uinjilishaji Mpya.

Kazi kubwa sasa ni kwa Mababa wa Sinodi, Viongozi wa Makanisa Mahalia na Taifa la Mungu katika ujumla wake, kutekeleza kwa umakini mkubwa mawazo na changamoto zilizotolewa na Mababa wa Sinodi, kila mtu akijitahdi kusoma alama za nyakati.







All the contents on this site are copyrighted ©.