2012-10-27 14:11:35

Papa afanya mabadiliko makubwa: Seminari za Kanisa Katoliki kusimamiwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri: Katekesi itakuwa chini ya Baraza la Kipapa la Uinjilishaji Mpya!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati akishiriki katika maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya, Jumamosi tarehe 27 Oktoba, 2012 amewashukuru na kuwapongeza Mababa wa Sinodi kwa kazi kubwa waliyoifanya kama sehemu ya mchakato unaopania kutangaza Imani ya Kikristo. Maadhimisho haya yamekuwa ni fursa makini kwa Mama Kanisa kutafakari kwa kina kuhusu nafasi na dhamana ya Seminari na Vyuo vya Katekesi.

Baada ya Sala na Tafakari ya kina, Baba Mtakatifu anasema, ameamua kwamba, dhamana ya kuangalia Seminari zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki zilizokuwa chini ya Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki kwa sasa zitasimamiwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri. Idara ya Katekesi iliyokuwa chini ya Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makleri sasa inahamishiwa kwenye Baraza la Kipapa la Uinjilishaji Mpya.

Mabadiliko haya yataanza kutekelezwa baada ya kuchapishwa hati maalum kutoka kwa Baba Mtakatifu mwenyewe. Anawaalika Mababa wa Sinodi pamoja na waamini kwa ujumla, kuendelea kusali kwa ajili ya kuombea Mabaraza haya ili yaweze kutekeleza utume huu muhimu kwa moyo wa ushirikiano kwa ajili ya mafao ya Kanisa zima.

Baba Mtakatifu ametumia fursa hii pia kuwatakia kheri na baraka Makardinali Wateule, kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya, unaoonesha ile sura ya Kanisa la Kiulimwengu, mahali ambapo watu kutoka katika kila kabila, lugha na jamaa wanaozungumza lugha ya Pentekosti Mpya ya Kanisa badala ya kujikita katika mwelekeo wa Kanisa la Kibara. Pentekoste Mpya ni mwelekeo ambao umejionesha kwa namna ya pekee, wakati wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya.

Kanisa la Kiulimwengu linaendelea kujionesha katika: madhulumu, hatari, furaha na matumaini yanayoonesha uwepo endelevu wa Kristo miongoni mwa Wafuasi wake, hata katika hali ngumu zaidi. Huu ndio ushuhuda uliotolewa na Mababa wa Sinodi kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Kanisa linaendelea pia kushuhudia uwepo wa Roho Mtakatifu anayelionesha mwanga na dira inayopaswa kufuatwa kama Kanisa Katoliki.

Baba Mtakatifu kwa mara nyingine tena, amewapongeza Mababa wa Sinodi na wadau mbali mbali waliohusika ili kufanikisha tukio hili muhimu katika maisha na utume wa Kanisa, wakiwa na ari ya kutaka kutangaza Injili ya Kristo. Anasema, mapendekezo hamsini na nane yaliyotolewa na Mababa wa Sinodi ni Waraka unaobubujika kutoka katika undani wa maisha unaopania kuzaa maisha mapya kwa Kanisa katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya.







All the contents on this site are copyrighted ©.