2012-10-27 13:22:21

Hija za maisha ya kiroho ziendelee kuimarisha na kukuza Imani na Injili ya Upendo na Mshikamano kati ya watu!


Hija mbali mbali zinazofanyika wakati huu wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita hivi karibuni, zinapania kwa namna ya pekee kuimarisha imani ya waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia na kama kielelezo makini cha umoja, upendo na mshikamano wa dhati na Makanisa mahalia.

Kutokana na msukumo huu wa kiimani, Wanachama elfu tatu wa Chama cha Kitume cha Kaburi Takatifu la Yerusalem, wanatarajiwa kutembelea maeneo ya kihistoria na kiimani yaliyoko mjini Roma kuanzia tarehe 13 hadi tarehe 15 Septemba 2013. Tukio hili linakwenda sanjari na maadhimisho ya Mkutano mkuu wa Chama hiki cha Kitume, unaotarajiwa kuhitimishwa kwa Ibada ya Misa Takatifu itakayoongozwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita.

Hayo yamebainishwa na Kardinali Edwin Fredrick O'Brien, Rais wa Chama hiki cha Kitume, wakati wa mkutano wao wa Mwaka uliokuwa unafanyika hapa mjini Roma, mwishoni mwa Juma. Viongozi wa Kanisa kutoka Mashariki ya Kati wameainisha mipango na mikakati ya shughuli za kichungaji katika sekta ya elimu inayopania kuwanufaisha wanafunzi elfu kumi na nane kutoka: Israeli, Palestina na Yordani. Wanafunzi hao wanapata elimu kutoka katika shule za Msingi na Sekondari arobaini na mbili zinazofadhiliwa na Chama hiki cha Kitume.

Viongozi mbali mbali wa kidini kutoka Mashariki ya Kati wameonesha hofu na wasi wasi wao kutokana na kuongezeka kwa vitendo vinavyoashiria misimamo mikali ya kidini pamoja na kinzani na migogoro ya kisiasa na kijamii. Viongozi hao wakuu wamebainisha kwamba, Nchi Takatifu bado ina utajiri mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa kama ilivyojionesha wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Familia Kimataifa, iliyokazia umuhimu wa Waamini kuiga mfano kutoka katika Familia Takatifu ya Nazaeti katika hija ya maisha yao hapa duniani.

Umoja na mshikamano uliojionesha wakati wa Karamu ya Mwisho na wakati ule Mitume walipokuwa wanangojea zawadi ya Roho Mtakatifu ni tema zilizopembuliwa kwa mapana wakati wa Maadhimisho ya Kongamano la Hamsini la Ekaaristi Takatifu Kimataifa lililofanyika huko mjini Dublin, Ireland mwaka 2012.







All the contents on this site are copyrighted ©.