2012-10-25 08:37:26

Huduma za Upasuaji kwa Watoto wanaotibiwa Hospitali ya Mt. Gaspar Itigi kuboreshwa zaidi baada kuweka mkataba na Hospitali ya Bambino Gesù


Hospitali ya Bambino Gesù inayomilikiwa na kuendeshwa na Vatican imetiliana mkataba wa Ushirikiano na Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Kanda ya Italia, unaopania kuboresha huduma za upasuaji zinazotolewa na Hospitali ya Mtakatifu Gaspar iliyoko Itigi, Singida, Tanzania.

Maboresho haya yanalenga zaidi kwenye Kitengo cha Watoto wanaohudumiwa na Hospitali ya Mtakatifu Gaspar, Itigi, ambacho kwa miaka mingi, kimekuwa mstari wa mbele katika jitihada za kuokoa maisha ya watoto wanaotoka katika Mikoa ya Kanda ya Kati nchini Tanzania.

Mkataba huo umetiwa sahihi na Professa Giuseppe Profiti Rais wa Hospitali ya Bambino Gesù kwa niaba ya Uongozi wa Hospitali ya Bambino Gesù pamoja na Mheshimiwa Padre Oliviero Magnone, Mkuu wa Kanda ya Italia, Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu kwa niaba ya Shirika na kuhudhuriwa na wafanyakazi wa Hospitali ya Bambino Gesù pamoja na baadhi ya Wamissionari wa Damu ya Azizi ya Yesu.

Kuanzia mwaka 2013, Kitengo cha Huduma kwa Watoto Hospitali ya Itigi kitakuwa sasa ni Kituo cha Huduma ya Upasuaji cha Hospitali ya Bambino Gesù na kitaendeshwa kwa ushirikiano kati ya Hospitali ya Bambino Gesù na Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu.

Itakumbukwa kwamba, kwa miaka kadhaa, kumekuwepo na ushirikiano mkubwa kati ya Hospitali ya Mtakatifu Gaspar na Bambino Gesù katika huduma kwa watoto waliokuwa na matatizo ya moyo, ambao walilazimika kila mwaka kusafirishwa hadi Roma, Italia kwa ajili ya kupata huduma ya upasuaji wa moyo, sasa huduma hii itaanza kutolewa Hospitali ya Mtakatifu Gaspar, Itigi, kwa lengo la kuokoa maisha ya watoto wengi ambao wanapoteza maisha yao kutokana na ukosefu wa huduma makini ya afya.

Hospitali ya Mtakatifu Gaspar, Itigi, inayoongozwa na kauli mbiu: tibu, fariji na elimisha ilifunguliwa rasmi kunako mwaka 1989 na Rais Ali Hassan Mwinyi. Tangu wakati huo, Hospitali imeendelea kupanua huduma zake hadi kufikia hatua ya kupandishwa hadhi na kuwa ni Hospitali ya Rufaa kunako mwaka 2010.

Itakumbukwa kwamba, kutokana na ongezeko la vifo vya watoto chini ya umri wa miaka kumi kwenye mikoa ya kanda ya Kati, Hospitali ya Mtakatifu Gaspar, iliamua kupanua huduma kwa watoto kutoka vitanda arobaini na tano hadi kufikia vitanda mia moja hamsini, tukio lililomshangaza Rais Benjamin William Mkapa alipokuwa anafungua Wodi za Watoto hapo tarehe 23 Novemba 2003.

Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu wanasema, zote hizi ni juhudi za Mama Kanisa katika kumhudumia mtu: kiroho na kimwili na kwa namna ya pekee kuendeleza ile kazi iliyoanzishwa na Yesu mwenyewe kwa kuwatibu watu magonjwa yao kimwili na kiroho kwa kuwaondolea dhambi zao.







All the contents on this site are copyrighted ©.