Familia ya Mungu inawajibu wa kuwa chachu ya imani na matumaini kwa watu waliokata
tamaa na kukengeuka!
Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican karibu tena katika makala yetu ya Uinjilishaji
wa kina. Juma lililopita tulizungumzia juu ya maeneo muhimu yanayogusa Uinjilishaji
mpya kama unavyoletwa kwetu na Baba Mtakatifu Benedikto XVI katika hati ya Mwongozo
wa kutendea kazi juu ya Uinjilishaji mpya.
Juma hili
tuendelee kutembea pamoja na Baba Mtakatifu katika kushirikishana yale yanayojadiliwa
na Mababa wa Sinodi ya Uinjilishaji Mpya, kama njia ya kurithisha imani ya Kikristo.
Mpendwa msikilizaji wa radio Vatican, Baba Mtakatifu, anaendelea mbele kubainisha
mazingira halisi wanayojikuta Waumini katika mazingira ya leo ambayo yanabadilika
kwa kasi tena bila tahadhari. Wanafamilia ya Mungu sehemu mbali mbali duniani, wanakumbwa
na uoga na kuchanganyikiwa wanapotazama ulimwengu wa leo hususan juu ya utu, maadili
na maendeleo ya Binadamu kiroho na kimwili.
Katika mataifa yaliyoendelea wanafamilia
ya Mungu wanakosa rejea katika kujitafuta wao wenyewe kama viumbe wa Mungu katika
umilele. Hii inatokana na ukweli kwamba, ule mchafuko na mporomoko wa kifikra kumhusu
Mungu unaotokana na kuibuka kwa utandawazi ambao umegusa jamii nzima hata Kanisa.
Katika mazingira hayo anabainisha Baba Mtakatifu kuwa, watu wengi wamepoteza matumaini
ya maisha na hivyo kukata tamaa kabisa.
Baba Mtakatifu anawaasa Maaskofu katika
Sinodi hii kuona namna mbadala ya kurudisha tumaini hilo miongoni mwa Waamini na hivyo
kuimarisha utume wa Kanisa lakini hasa zaidi kuonesha kupitia Uinjilishaji Mpya maana
ya maisha kwa watu wa Mungu. Aidha Baba Mtakatifu anabainisha kwamba, kwa namna hiyo
Wanafamilia ya Mungu wataweza kuwa chachu ya matumaini kwa watu wote kupitia majadiliano
na kuwashirikisha wengine tumaini lile wanaloamini na kuliishi.
Katika ulimwengu
huu wenye dalili zote za kuporomoka kwa maadili na utu wema, kuna uhitaji mkubwa wa
kukaa pamoja na kupeana moyo. Wakristo wanaoishi katika tumaini la Kristo: aliyeteseka,
akafa na kufufuka wana wajibu wa kuwatumainisha wengine.
Njia pekee anasema
Baba Mtakatifu ya kuwarudishia Taifa la Mungu matumaini ni ile ya Wakristo kukaa pamoja
na kutathmini kwanza namna wanavyoishudia imani yao kwa wengine, kutathmini mazingira
jinsi yalivyo na hivyo kubuni mbinu mkakati wa kupambana na mazingira hayo.
Badala
ya kubaki tu kuhubiri Neno la Mungu Kanisani, katika vikundi vya sala; wakati umefika
ambapo lazima Kristo ajidhihirishe sasa katika mazingira halisi ya watu wake kama
Mponyaji wa wagonjwa, Anayejali walio pweke, wafungwa, wasio na sauti, wakimbizi,
wasio na chakula na mazingira yanayofanana na hayo. Hii inawaalika Wakristo kumleta
Kristo kwa walio wake katika matendo halisi katika mazingira halisi.
Kanisa
linaalikwa kuivalia njuga dhana nzima ya Mungu katika yale maeneo ambayo tuliona hapo
kwanza kuwa ni sababu ya kushuka kwa Uwepo wa Mungu katika maisha ya watu. Kanisa
kupitia waamini wake lazima kumleta Mungu katika historia ya ulimwengu na vyote viijazavyo
akiwapo Mwanadamu na karama zake.
Lazima watu wapambanue matendo ya Mungu
yanayoendelea kutendeka kupitia Mwanadamu na sio Mwanadamu kuwa chanzo na mwisho wa
mambo hayo. Wanafamilia ya Mungu kama Kanisa watafanikiwa iwapo watashiriki kikamilifu
katika maeneo hayo na kutoa mwelekeo halisi na maana ya mambo hayo. Wakristo wawasaidie
watu kuelewa mipaka ya tafiti za kibaolojia, madawa na lishe; wawasaidie watu kuelewa
kutumia vema vyombo vya mawasiliano, wanasiasa waelimishwe nafasi yao katika kuiunganisha
jamii kuishi kwa amani, haki na mapatano.
Watu waoneshwe kutumia vema rasilmali
za ulimwengu huu wakiwasaidia wale wanaoshindwa kujikomboa kutokana na mazingira yao
kujipatia mahitaji ya maisha kirahisi. Maana yake Wanafamilia ya Mungu wawe mashahidi
kwa maisha yao kujenga amani, upatanisho, haki, uwajibikaji, upendo na mshikamano
katika jamii.
Baba Mtakatifu Benedikto XVI anamalizia sehemu hii kwa kukazia
umoja, mshikamano, maisha ya amani na watu wenye imani tofauti na sisi, na ushuhuda
wa maisha yanayomstahili mwanadamu miongoni mwa Waumini ili kutoa mfano hai kwa mataifa.
Huku ndio kuangalia na kutasiri vizuri alama za nyakati ili kuweza kuutangaza vizuri
ujumbe wa Injili.
Mpendwa msikilizaji nakushukuru sana kuwa nami kwa wasaa
wote. Nakutakia Baraka tele toka kwa Mwenyezi Mungu unapojiandaa kutembea pamoja na
Maaskofu katika Sinodi juu ya uinjilishaji mpya. Kutoka studio za Radio Vatican ninayekakuaga
ni mimi Padre George wa Bodyo mtayarishaji na msimulizi wa kipindi hiki.