Kardinali Pengo asema "Kamwe msitumie kinzani, vurugu na misigano ya kidini kujinufaisha
kiuchumi, kisiasa, kijamii na kidini"
Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya inayoendelea hapa mjini Vatican
wanasema, kati ya mambo yanayoendelea kukwamisha mchakato wa majadiliano ya kidini
ni pamoja na misimamo mikali ya kiimani, watu kutoheshimu sheria za nchi kwa kutaka
kujichukulia sheria mikononi mwao pamoja na malumbano ya kidini yanayolenga kuvunja
misingi ya amani na mshikamano kati ya watu wa mataifa kwa malengo binafsi: kisiasa,
kiuchumi, kijamii na kidini.
Katika mahojiano
maalum na Radio Vatican, Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza
ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar anabainisha kwamba, choko choko, machafuko
na uharibifu wa mali kwa misingi ya kidini, zimeendelea kujionesha kwa namnaya pekee
nchini Nigeria na Tanzania. Hii ni kutokana na sababu kwamba, watu wanashindwa kuelewa
kwamba, kimsingi hakuna dini inayoshabikia mapigano wala machafuko ndani ya Jamii.
Kardinali
Pengo anasema kwamba, kuna watu ambao wanapenda kutumia tofauti za kidini kama njia
ya kujijenga: kisiasa, kiuchumi, kijamii na kidini, kiasi hata cha kuhatarisha amani,
usalama, utulivu na mshikamano wa kitaifa. Ni watu wanaogubikwa na ubinafsi, uchu
wa mali na kupenda mno madaraka. Watu wa namna hiyo hawataki kusikia ukweli mkamilifu
kuhusu masuala ya kidini, kwao jambo la msingi ni kufaidika na migogoro na kinzani
za kidini.
Kardinali Pengo anawaalika Waamini wa Dini ya Kiislam na Kikristo
kuendeleza moyo wa majadiliano ya kidini, kwa kuheshimiana, kuthaminiana na kujadiliana
masuala muhimu ya kidini kwa ajili ya mafao ya wengi na kamwe tofauti zao za kidini
zisiwe ni chanzo cha kinzani, vurugu, umwagaji wa damu ya watu wasiokuwa na hatia
na uharibifu wa mali ya watu.
Serikali na vyombo vya dola vitekeleze wajibu
wake kikamilifu kwa kuhakikisha kwamba, utawala wa sheria unashika mkondo wake. Anatoa
onyo kwa wanasiasa wanaotumia tofauti za kidini kama njia ya kujitafutia umaarufu,
ili hatimaye, kujijenga kiuchumi, kisiasa na kijamii, kuacha mara moja kwani wanaweza
kusababisha maafa makubwa kwa Jamii. "Kamwe hasiwepo mtu anayetumia dini kama ngao
yao katika medani mbali mbali za maisha".
Kardinali Pengo anawaomba watanzania
na watu wote wenye mapenzi mema kutambua kwamba, tofauti za kidini na kiimani zimekuwepo
nchini humo miaka nenda miaka rudi, lakini watu wakaheshimiana, kuthaminiana na kusaidiana.
Anajiuliza, kumetokea nini hata leo hii dini iwe ni chanzo cha kinzani, vurugu na
machafuko nchini Tanzania?
Anawakumbusha wote wanaotaka kuchochea vurugu,
vita na kinzani kwamba, amani ikitoweka, hakuna mtu atakayesamilika kwani matunda
ya kuvunjika kwa misingi ya haki kamwe hayawezi kudumu. Ni jukumu la kila mtu kutafuta,
kulinda na kudumisha misingi ya haki na amani na kamwe tofauti za kidini zisiwe ni
chanzo cha kinzani, vurugu na umwagaji damu.