2012-10-18 08:18:36

Dhamana ya Wakristo katika mchakato mzima wa Uinjilishaji Mpya katika ulimwengu mamboleo!


Mababa wa Sinodi ya Maaskofu kuhusu Uinjilishaji Mpya wanaendelea kuwahimiza Wakristo kutoogopa kamwe kutokana na vitisho na changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza katika dhamana ya Uinjilishaji Mpya kwani, Kanisa lina mtandao mpana unaojikita katika: Majimbo, Parokia na Vigango. Fursa zote hizi zinaweza kutumiwa na Mama Kanisa ili kufanikisha dhamana ya Uinjilishaji Mpya unaofanyiwa kazi kwa sasa.

Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, Wakristo wanahamasishwa kujitoa bila ya kujibakiza, wakisukumwa na ari, moyo na ukarimu wa Kiinjili, kushiriki katika mikakati ya kichungaji kwa ajili ya maisha na Utume wa Kanisa. Majukumu haya yanaweza kutekelezwa kwa njia za kawaida, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa ajili ya huduma kwa wagonjwa, majiundo makini ya wanafunzi shuleni na vyuoni, njia za mawasiliano ya jamii; uwanja wa sanaa, utamaduni na michezo pamoja na kusimama kidete na wafanyakazi na wakulima, ili kukabiliana na changamoto zao kwa moyo wa Kiinjili.

Vyama vya kitume vinapaswa kuwezeshwa, ili kutekeleza wajibu wao, kwa kutambua kwamba, vinashiriki pia katika Unabii wa Kanisa. Waamini wanapaswa kujitambulisha kwa njia ya utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu; ushuhuda kwa njia ya Injili ya Upendo; ushiriki mkamilifu katika maadhimisho mbali mbali ya liturjia ya Kanisa; ili matukio yote haya yawawezeshe waamini kuweza kukutana na Yesu anayefanya hija katika maisha yao ya kiimani.

Mababa wa Sinodi wanasema, ukanimungu, mawazo mepesi mepesi na uhuru usiokuwa na mipaka ni mambo yenye madhara makubwa katika: imani, maisha adili, mahusiano katika familia na jamii katika ujumla wake na matokeo yake ni watu kugubikwa na ubinafsi. Lakini ikumbukwe kuwa, wanadamu wanategemeana na hakuna mtu anayeweza kujigamba kwamba, anajitosheleza, lakini zaidi, mwanadamu anamtegemea na kumhitaji Mungu katika maisha yake.

Kumbe waamini washirikishwe kwa ukamilifu katika kubuni, kupanga, kutekeleza na kutathimini mikakati mbali mbali inayopania kukoleza ari na moyo wa Uinjilishaji Mpya miongoni mwa Jamii. Lengo ni kuwajengea waamini uwezo wa kujisomea, kulitafakari na kuliishi Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha yao na kwamba, Wakristo wanapaswa kuona fahari ya kushirikishana utajiri unaofumbatwa katika Neno la Mungu.

Mababa wa Sinodi kwa namna ya pekee, wanawashukuru na kuwapongeza wanawake wanaojitoa bila ya kujibakiza katika maisha na utume wa Makanisa mahalia, katika malezi na makuzi ya watoto na vijana; katika huduma kwa wagonjwa, wazee na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Ni jukumu la Kanisa kuwawezesha wanawake ili waweze kuchangia zaidi katika maisha, utume na ustawi wa Kanisa katika ujumla wake.

Waamini wanapaswa kufundishwa namna ya kusali ili waweze kusali vyema wakiwa na amani na utulivu wa ndani; daima wakitamani kuyafahamu mapenzi ya Mungu katika maisha yao. Watambue dhana na uwepo wa dhambi inayoharibu uhusiano kati yao na Mungu pamoja na jirani zao. Wajitahidi kukimbilia huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya Sakramenti za Kanisa, ili hatimaye, waweze kupata maisha mapya. Waamini wawezeshwe kikamilifu, ili washiriki katika azma ya Uinjilishaji, kwani hawa ni nguvu kazi ambayo ikitumiwa barabara inaweza kulisaidia Kanisa katika mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu.

Vijana ni kundi jingine linalopaswa kuwekewa mikakati makini ya Uinjilishaji Mpya, ili katika harakati zao za kutafuta ukweli na maana ya maisha, waweze kukutana na Yesu Kristo Mkombozi wa dunia. Ni jukumu la Kanisa kuwasaidia vijana hawa kutambua maana ya maisha kwa kujichotea utajiri unaofumbatwa katika Kweli za Kiinjili.

Vijana watambue wazi kwamba, wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuwainjilisha vijana wenzao wanapokutana katika "vijiwe" vyao. Vyama vya utume kwa vijana viendelee kupewa msukumo wa pekee, ili hatimaye, kwa pamoja waweze kujenga Jumuiya ya Waamini wanaoshiriki kikamilifu Fumbo la Ekaristi Takatifu.

Uinjilishaji Mpya upanie kukoleza majadiliano na wasiomwamini Kristo, ili katika hija ya maisha yao, waonje na kuguswa na uwepo wa Mungu aliyewaumba, anayewapenda na kuwathamini na anataka kuwakomboa kwa njia ya Mwanaye Mpendwa Yesu Kristo. Wasioamini waguswe na mifano na ushuhuda wa mitume, watakatifu na waamini ambao wamekuwa mstari wa mbele kumwilisha Injili ya Kristo katika uhalisia wa maisha yao.

Miaka hamsini imekwisha gota, tangu Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican walipoonesha dira na mwongozo wa kufuata katika harakati za kukoleza ari na moyo wa majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Wakristo. Vikwazo vingi vimeweza kuvukwa hadi wakati huu, changamoto kwa Wakristo wote katika umoja wao kushuhudia kweli za Kiiinjili kwa njia ya huduma ya upendo. Kanisa linatambua kwamba, lipo kwa ajili ya Kuinjilisha.

Jukumu hili linapaswa kupata pia chapa ya Kiekumene kwa kukazia utakatifu wa maisha, ili kwa pamoja waweze kuungama Imani inayojikita katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, Biblia Takatifu na Mapokeo. Matunda ya Uinjilishaji Mpya ni neema ya Mungu inayojionesha miongoni mwa waamini wenye dhamana ya Kuinjilisha. Ni lazima liwe ni Kanisa linalochota utajiri wake kutoka katika Heri za Mlimani, ambazo kimsingi ni muhtasari wa Mafundisho Makuu ya Yesu. Waamini waundwe kikamilifu ili hatimaye, waweze kufikia ukomavu katika Ibada, maisha ya kijumuiya na utume wao ulimwenguni.

Jumuiya za Kikristo zijibidishe kuhakikisha kwamba, Injili ya Kristo inamgusa mwanadamu: kiroho na kimwili; na kwamba, utangazaji wa Habari Njema, ufanyike kwa njia ya Liturjia ya Kanisa na Huduma ya Upendo. Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, yawe ni kiini na hitimisho la maisha na utume wa Kanisa. Waamini wajichotee nguvu na neema kutoka katika Fumbo la Ekaristi Takatifu. Liturjia ina umuhimu wa pekee, katika mchakato mzima wa Uinjilishaji Mpya.







All the contents on this site are copyrighted ©.