Jitajirishe na mchango wa Mababa wa Sinodi juu ya Uinjilishaji mpya kama njia ya kurithisha
imani ya Kikristo!
Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji mpya wanaendelea kuadhimisha Sinodi
hii inayoongozwa na kauli mbiu Uinjilishaji mpya ni kutangaza imani ya Kikristo. Kwa
namna ya pekee, Mababa wa Sinodi wameguswa na ushuhuda wa imani iliyooneshwa na wafiadini
ndani ya Kanisa kwa nyakati mbali mbali. Hawa ni watu walioguswa kwa namna ya pekee
na upendo wa Yesu na Mafundisho yake, hata wakawa tayari kuyamimina maisha yao.
Hata
leo hii, kuna Wakristo bado wanaendelea kudhulumiwa na kunyanyaswa kutokana na imani
yao kwa Kristo na Kanisa lake. Mababa wa Sinodi wanasema, waamini hawa wanapaswa kuheshimiwa
na kuthaminiwa kutokana na ushuhuda wa imani yao, kwani kimsingi imani ni jambo la
hadhara na wala si kitu cha kuficha, bali inapaswa kutolewa ushuhuda wenye kuleta
mvuto na mguso katika maisha ya watu.
Wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi
maalum ni kundi linaloteseka na kuonja hadha ya maisha. Ni watu wanaotafuta maana
ya maisha yao hapa ulimwenguni. Mababa wa Sinodi wanasema, hili ni kundi ambalo ni
chemchemi mpya ya Uinjilishaji unaopaswa kufanywa na Mama Kanisa katika mapambazuko
ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Wahamiaji na wakimbizi hawa, wakishainjilishwa nao
pia wanageuka na kuwa ni vyombo vya Uinjilishaji kwa wale wanaowazunguka. Ili kufanikisha
azma hii, haki zao msingi hazina budi kuheshimiwa na kuthaminiwa na Jumuiya ya Kimataifa.
Kanisa
linapaswa kutambua kwamba, Injili ya Upendo ni ushuhuda makini kabisa wa Uinjilishaji.
Waamini wajikite zaidi na zaidi katika kumwilisha Injili ya upendo kwa maskini na
wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili wao pia waonje huruma na upendo wa Kristo
unaojionesha kwa namna ya pekee kwa njia ya Kanisa. Uinjilishaji mpya uwe ni mwendelezo
unaopania kuonesha uwepo wa Kristo kati ya wafuasi wake.
Familia ni Kanisa
dogo la nyumbani, linalopaswa kuwa kweli ni shule ya utakatifu, haki na amani; hii
ni chemchemi ya Uinjilishaji mpya. Pale ambapo mikakati ya kichungaji imeshindwa kutekelezwa
ni kwa vile Kanisa limeshindwa kujitambua kuwa ni Familia ya Mungu inayowajibika na
badala yake dhana ya Kanisa kama Taasisi imekuzwa na kupewa kipaumbele cha kwanza,
kiasi hata cha kusahau changamoto iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa
Vatican.
Mababa wa Sinodi wanasema, Kanisa kamwe halitaweza kukaa kimya na
kufumbia macho mmong'onyoko wa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, unaofanywa
kwa makusudi mazima na baadhi ya wanasiasa, ambao sera na mikakati yao inalenga kubomoa
misingi bora ya kifamilia. Hii ni changamoto kubwa kwa Mama Kanisa hasa katika nchi
za Ulaya zinazokabiliwa na ukanimungu wa kutisha. Kanisa linaposimama kidete kulinda
na kutetea tunu msingi za kifamilia mintarafu Mafundisho ya Kristo na utu wema, wanandoa
wanajikuta wakiwa na dhamana ya kukuza na kudumisha uaminifu wao kama kielelezo makini
cha imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.
Mababa wa Sinodi wanasema, Parokia
zinapaswa kutekeleza wajibu wake katika maisha na utume wa Kanisa kwa kukuza na kuendeleza
Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo, shule ya majadiliano ya kidini na waamini wa dini
mbali mbali. Majadiliano haya yanapaswa kuwa ni sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji
mpya, changamoto iliyotolewa kwa mara ya kwanza na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili
wa Vatican, takribani miaka hamsini iliyopita.
Juhudi hizi hazina budi kwenda
sanjari na utamaduni wa kusikilizana, kuheshimiana, kuthaminiana na kushirikishana
mang'amuzi na tunu msingi za maisha ya kidini, daima mafao ya wengi yakipewa kipaumbele
cha kwanza. Mababa wa Sinodi wanakiri kabisa kwamba, vitendo vya kigaidi, misimamo
mikali ya kiimani na tabia ya baadhi ya watu kutozingatia na kuheshimu sheria ni mambo
yanayokwamisha jitihada za Mama Kanisa katika mchakato mzima wa majadiliano ya kidini
sehemu mbali mbali za dunia. Lakini matukio yote haya yasiwakatishe moyo waamini kujikita
katika majadiliano ya kidini.
Tema nyingine iliyojitokeza ni umuhimu wa utamadunisho
kama njia ya Uinjilishaji mpya, ili Injili iweze kuota mizizi na kushika hatamu katika
maisha na vipaumbele vya waamini, wakiwa tayari kuitolea ushuhuda imani yao kwa Kristo
na wakiendelea kubaki na utambulisho wao wa mahali wanapotoka.
Kashfa ya utengano
kati wafuasi wa Kristo ni mada ambayo pengine haijapewa msukumo wa pekee, lakini Mama
Kanisa anachangamo kuhakikisha kwamba, anawajengea waamini wake moyo na ari ya kutaka
kukuza na kudumisha majadiliano ya kiekumene miongoni mwa wafuasi wa Kristo, ili siku
moja kadiri ya mapenzi ya Mungu, umoja huu uweze kuonekana kama kielelezo makini cha
imani ya Kanisa.
Juhudi hizi ziyahusishe Makanisa na Madhehebu mbali mbali
ya Kikristo, ili wote wawe ni wamoja kama Kristo anavyotaka Kanisa lake liwe. Lengo
ni Wakristo katika umoja wao, kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza
katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Umoja na mshikamano
wa Kikristo unapaswa pia kujionesha kwa namna ya pekee, wanaposhiriki katika "kuumega
mkate", wanaposoma na kulitafakari kwa pamoja Neno la Mungu, tayari kulitolea ushuhuda
katika uhalisia wa maisha yao.
Uinjilishaji mpya unajikita wanasema Mababa
wa Sinodi katika utangazaji wa Neno la Mungu kwa umakini na umahiri mkubwa, ili hatimaye,
Neno hili liwe ni kichocheo cha tafakari ya kina inayolenga kuzima kiu ya uwepo wa
Mungu miongoni mwa binadamu. Uinjilishaji mpya ni mchakato wa ndani ya mtu unaolenga
kwa namna ya pekee kumletea wongofu wa ndani, utakatifu na hatimaye, maisha ya uzima
wa milele. Imani kwa Kristo na Kanisa lake inadai utii na upendo mkamilifu.
Mababa
wa Sinodi wanaona umuhimu wa kuwainjilisha vijana wanaoendelea kukumbana na changamoto
mbali mbali katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia ili
waweze kumfahamu, kumpenda na htimaye, kujitoa bila ya kujibakiza kumtumikia Kristo
katika maisha ya Kipadre na Kitawa. Uinjilishaji mpya kwa vijana unapaswa kwenda sanjari
na jitihada za Mama Kanisa katika maboresho ya sekta ya elimu na umakini katika majiundo
ya vijana, ili waweze kutambua wajibu na dhamana yao ndani ya Kanisa, tayari kuitolea
ushuhuda imani hii katika mazingira na changamoto za maisha yao ya ujana.
Utume
wa Kanisa miongoni mwa vijana ni jambo linalopaswa kupewa msukumo wa pekee kwa kuhakikisha
kwamba, wahudumu wakuu wanaandaliwa kwa umakini mkubwa, ili kuwamegea vijana hawa
tunu msingi za maisha ya Kikristo na kweli za Kiinjili, kwa njia ya ushuhuda wa maisha
na mafundisho yao.
Uinjilishaji mpya ujenge mahusiano mema na ya dhati miongoni
mwa watu wa Mataifa. Uhusiano huu kwanza kabisa ujioneshe katika maisha ya Kifamilia,
Jumuiya Ndogo ndogo za Kikristo, Vyama vya Kitume na Jamii katika ujumla wake. Kila
mtu aguswe kwa namna ya pekee na uwepo wa jirani yake. Mshikamano huu wa upendo ujioneshe
hasa kwa wagonjwa, maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Watu
washikamane kwa pamoja ili kukabiliana na changamoto za hali ngumu ya maisha na mmong'onyoko
wa maadili na utu wema. Hakuna muujiza unaoweza kufanywa wa kupata mali au kumaliza
matatizo bila ya kufanya kazi kwa bidii, juhudi na maarifa.
Waamini watambue
kwamba, Mwenyezi Mungu anaendelea kutenda miujiza ya uponyaji kwa kushirikiana na
madaktari na kamwe wasipuuze huduma za afya wakitarajia miujiza katika maisha yao,
matokeo yake, watajikuta wakitangatanga katika madhehebu na dini mbali mbali, kielelezo
cha myumbo wa imani.
Mababa wa Sinodi wanatambua na kuheshimu mchango wa waamini
walei katika maisha na utume wa Kanisa. Wanaalikwa kuyatakatifuza malimwengu kwa njia
ya ushuhuda wa utakatifu wao binafsi, maadili na utu wema, bila kusahau mchango na
ushiriki wao katika Jumuiya ndogo ndogo za kikristo. Maadhimisho ya Mwaka wa Imani
yatoe changamoto ya pekee kwa wanaume na vijana kushiriki kikamilifu katika utume
wa Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo kama chemchemi ya Uinjilishaji mpya. Ile ni shule
ya Neno la Mungu na umwilishaji wa Injili ya upendo.