Tumieni utajiri wenu kujenga utamaduni wa upendo na mshikamano ili mjipatie utimilifu
wa maisha na uzima wa milele!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana kwenye
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican alitafakari kuhusu dhana ya
utajiri mintarafu Ibada ya Neno la Mungu, Jumapili ya ishirini na nane ya Kipindi
cha Mwaka wa Kanisa.
Anasema, ni vigumu kwa matajiri kuingia katika ufalme
wa Mungu, lakini si jambo ambalo haliwezekani kabisa, ikiwa kama utajiri na mali hii
itatumika kujenga na kuimarisha mshikamano na Injili ya upendo. Kwa njia hii, waamini
na watu wenye mapenzi mema, watakuwa wanatembea katika njia ya maisha wakijitahidi
kumfuasa Kristo ambaye licha ya kuwa tajiri, lakini alijinyenyekesha na kuwa maskini,
ili kutokana na umaskini wake, wengi waweze kuwa ni matajiri.
Baba Mtakatifu
anasema, Injili inamwonesha Kijana aliyekuwa na utajiri mkubwa, alikuwa ni Mchamungu
na alijitahidi kumwilisha Amri za Mungu katika maisha yake, lakini kwa bahati mbaya
alikuwa hajaonja maishani mwake furaha ya kweli, ndiyo maana anajitaabisha kumtafuta
Yesu ili aweze kuzima kiu yake ya kupata furaha ya kweli na utimilifu wa maisha.
Yesu
kwa jicho la Kimungu anamwangalia na kumpenda, lakini anatambua udhaifu wa kijana
huyu kuwa ni kung'ang'ania mno mali, ndiyo maana anamchangamotisha kutoa mali yake
yote kwa ajili ya maskini, kisha amfuate! Wazo hili hlikupokelewa kwa mikono miwili
na badala yake, likajenga majonzi moyoni mwa kijana yule, kwani alishindwa kujinasua
kutoka kwenye mali aliyokuwa anaimiliki, ambayo ilikuwa ni kikwazo kikubwa cha furaha
na maisha ya uzima wa milele.
Ndiyo maana Yesu anawakumbusha Wafuasi wake,
jinsi ambavyo ni vigumu kwa tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu, maneno ambayo yaliwaaacha
Mitume wakiwa wameshika tama! Anakazia kwamba, kile ambacho ni vigumu kwa binadamu,
lakini kinawezekana mbele ya Mwenyezi Mungu. Hii ni changamoto kwa watu wenye utajiri
kuhakikisha kwamba, wanatumia utajiri wao kwa ajili ya kujipata maisha ya uzima wa
milele.
Ndani ya Kanisa kuna mifano mingi ya watu waliotumia utajiri wa mali
yao mintarafu kweli za Kiinjili, kiasi hata cha kufikia utakatifu wa maisha. Hawa
ndio akina Francisco wa Assis, Mtakatifu Elizabeth wa Hungaria na Mtakatifu Charles
Borromoe, kwa kutaja wachache!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anawaalika
waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kumwomba Bikira Maria, Kikao cha Hekima aweze
kuwasaidia kupokea mwaliko wa Kristo kwa moyo wa furaha, ili waweze kupata utimilifu
wa maisha.