Msijaribu kuubinafsisha mchakato wa Mtumishi wa Mungu Julius K. Nyerere kutangazwa
kuwa Mwenyeheri! Ni Hatari!
Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika
na Madagascar ambaye pia ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, anawaalika
waamini na watu wenye mapenzi mema kutoka Barani Afrika kuhakikisha kwamba, wanatafuta
zaidi mafao ya wengi kwa njia ya kujitoa bila ya kujibakiza na kamwe wasigubikwe na
tamaa ya kutafuta utajiri, sifa na masilahi yao binafsi kiasi cha kusahau wajibu na
dhamana waliyokabidhiwa na Kanisa pamoja na Jamii kwa ujumla wake.
Kardinali
Pengo amewaonya baadhi ya watu wanaotaka kubinafsisha mchakato wa kumtangaza Mwalimu
Julius K. Nyerere kwa ajili ya sifa na utukufu wao binafsi kuwa mwelekeo wa namna
hii unaojionesha hata ndani ya Kanisa na miongoni mwa wanasiasa ni hatari katika zoezi
zima la mchakato wa Mwalimu Nyerere kutangazwa kuwa Mwenyeheri, hatua ambayo kwa sasa
iko katika ngazi ya Kijimbo. Mwalimu Nyerere awe ni mfano bora wa kuigwa kwa majitoleo
yake kwa ajili ya mafao ya wengi, ukuu na utakatifu wake, viwe ni sifa kwa Mwenyezi
Mungu aliyetenda makuu katika maisha ya Mwalimu.
Kardinali Pengo ameyasema
hayo wakati akitoa salam kwa watanzania na watu wenye mapenzi mema, waliohudhuria
katika Ibada ya Misa Takatifu, kama sehemu ya kumbu kumbu ya miaka kumi na mitatu,
tangu Mtumishi wa Mungu Mwalimu Julius K. Nyerere alipofariki dunia, Ibada ya Misa
iliyoongozwa na Askofu Mkuu Protas Rugambwa, Katibu mkuu Msaidizi wa Baraza la Kipapa
la Uinjilishaji wa Watu na Rais wa Mashirika ya Kipapa ya Kimissionari.
Zifuatazo
ni salam na matashi mema kwa watanzania kutoka kwa Kardinali Polycarp Pengo, Askofu
mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam.