Kumbukumbu ya Mwl. J. K. Nyerere, miaka 13 baada ya Kifo chake!
Imekwisha gota miaka kumi na tatu tangu Watanzania walipogubikwa na majonzi ya kuondokewa
na Mwalimu Julius kambarage Nyerere, kiongozi mashuhuri duniani aliyejitoa bila ya
kujibakiza kwa ajili ya kupigania misingi ya haki, usawa, maendeleo na ustawi wa wengi.
Kama dira na mwongozo wake, alikazia kwa namna ya pekee, umoja na mshikamano wa kitaifa,
uhuru na kujitegemea, utu na heshima ya binadamu vikipewa kipaumbele cha pekee.
Mwalimu
Nyerere ni mtu aliyekerwa sana na mambo ya: rushwa, ukabila, udini na umajimbo, mambo
ambayo ni sumu kali sana kwa mafao ya watanzania na ustawi wao kama nchi.
Leo
katika Studio za Radio Vatican, tumebahatika kuwa na Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo
Katoliki Dodoma anayebainisha jinsi ambavyo Mwalimu Nyerere alivyotumia karama na
vipaji vyake kwa ajili ya mafao ya wengi, tangu wakati wa kupigania uhuru hadi mauti
yalipomfika. Kama binadamu alikuwa na mapungufu yake.
Watanzania na Jumuiya
ya Kimataifa inapomkumbuka Mwalimu Nyerere inapaswa kuenzi yale aliyopenda na kuyathamini
si tu kwa maneno, bali kwa njia ya uhalisia wa maisha.