2012-10-12 09:21:25

Wito: Imarisheni juhudi za kuwahudumia wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi duniani


Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi, mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Ofisi za Umoja wa Mataifa zilizoko mjini Geneva, akichangia hoja kwenye mkutano wa sitini na tatu wa kamati tendaji ya Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa, ameitaka kwa namna ya pekee, Jumuiya ya Kimataifa kujenga na kuimarisha mshikamano sanjari na kuwalinda wakimbizi.
Kinzani na migogoro inayoendelea kufuka sehemu mbali mbali za dunia, imekuwa ni chanzo cha kuibuka kwa wimbi kubwa la wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi maalum.
Jambo la kusikitisha ni kuona kwamba, hata baadhi ya vyombo vya habari vinaendelea kufumbia macho tatizo hili kwa kuandika na kutangaza maeneo ambayo yanagusa masilahi yao binafsi, kiasi cha kuwaacha wakimbizi na wahamiaji kutangatanga, hali inayohatarisha usalama na maisha ya watu hawa.
Ujumbe wa Vatican kwenye mkutano huu umetoa shukrani za dhati kwa Mataifa na Jumuiya za Kimataifa zinazoendelea kutoa hifadhi na msaada kwa ajili ya wakimbizi na wahamiaji, wanaokimbia nchi zao kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao. Wanatoa mwaliko wa pekee, kwa Jumuiya ya Kimataifa kuzisaidia nchi kama hizi ili kubeba walay gharama za kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji wanaoendelea kuongezeka maradufu kila siku ya maisha.
Wajumbe hao wamelitaka Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa, kuhakikisha kwamba, linatoa ulinzi na usalama kwa wakimbizi kwa kuzingatia sheria na kanuni za Umoja wa Mataifa. Ni jukumu la Shirika hili kuongeza juhudi kwa kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji kwa kushirikiana kwa karibu zaidi na Mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa, alisema, Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi.








All the contents on this site are copyrighted ©.