2012-10-12 11:12:43

Maeneo maalum ya Uinjilishaji Mpya!


Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, karibu tena katika mfululizo wa vipindi vyetu vya uinjilishaji wa kina. Juma lililopita tulizungumzia dhana ya uinjilishaji mpya katika ulimwengu wa leo mintarafu maana yake na umuhimu wake. Leo tuendelee mbele kuungana na Baba Mtakatifu Benedikto XVI, anapobainisha maeneo muhimu yanayoguswa moja kwa moja na Uinjilishaji Mpya.

Unijilishaji mpya anasema Baba Mtakatifu ni ile hali ya kuwa na ari na moyo mpya wa kiutendaji ambapo Kanisa hutafsiri alama za nyakati na kubainisha mazingira mapya anayoishi Mwanadamu na hivyo kubuni mbinu mkakati za kumpeleka Kristo kuangaza mazingira haya ambayo kimsingi yanagusa Nyanja zote za maisha ya Mwanadamu: kisiasa, kiutamaduni, kiuchumi na kidini.

Utamaduni ni eneo la kwanza kabisa kuguswa na uinjilishaji mpya. Utamaduni wa leo umekumbwa zaidi na mtazamo wa kidunia zaidi kuliko wa kiroho miongoni mwa wanajamii. Uchaji na hofu ya Mungu vimetoweka kabisa na watu wala hawatoi tena kipaumbele kwa mambo ya dini au mambo ya Mungu. Katika nchi za magharibi hali hii imeongezeka sana kiasi kwamba Mungu taratibu anatoweka katika fikra za watu na badala yake watu wamezama katika kuhangaika na mambo ya kiulimwengu tu mintarafu mali, nguvu na umaarufu. Badala ya kuhangaikia wokovu war oho watu wanahangaika na kutafuta pesa zaidi, kutafuta kukuza jina kwa karama fulani na kuonekana zaidi kuliko wengine.

Utamaduni huu wa kidunia umejikita zaidi katika maisha ya mtu binafsi na uhuru wake hivi kwamba haukatai moja kwa moja uwepo wa Mungu bali unakuza na kuweka mbele mambo ya dunia hivi kwamba mtu hana muda wa kufikiria tena mambo ya Mungu. Aidha mtazamo huu wa kidunia hukuza zaidi hisia tepetevu katika mambo muhimu ya maisha ya mtu na kurahisisha kila kitu kuonekana cha kawaida. Katika mazingira haya watu wengi wameathirika kifikra na kimtazamo na kuona kila kitu sawa na haki, hivyo kukuza hisia za kipenda roho hula nyama mbichi au uzuri uko kwa jicho la mtazamaji. Kila kitu huwa halali ili mradi mtu havunji sheria ya nchi. Hali hii imepelekea malumbano makali ndani ya wanafamilia, kuongezeka kwa biashara ya ukahaba, dawa za kulevya na ndoa za jinsia moja.

Sekta ya jamii ni eneo jingine muhimu linahitaji uinjilishaji mpya. Mchangamano wa watu unaotokana na kuibuka kwa wimbi kubwa la uhamiaji katika kigezo cha utandawazi umechangia sana katika kuporomoka kwa mila na desturi nyingi zilizokuwa zinajenga jamii fulani. Leo hii kutokana na kukua kwa mawasiliano na ugumu wa maisha watu wengi wanahamia maeneo ya miji, nchi fulani au bara fulani kwa kigezo cha kutafuta maisha bora. Hali hii imegeuza kabisa sura za miji mingi na hata nchi fulani. Hali hii hupelekea kuporomoka kwa utambulisho wa jamii fulani, kuzuka kwa mila na desturi za wastani ambazo basi kila mtu anaishi kadiri ananvyoweza.

Njia za mawasiliano ni eneo jingine nyeti linalohitaji uinjilishaji mpya. Njia bora za mawasiliano zimewesha upatikanaji haraka wa habari, elimu na kukuza biashara. Njia za mawasiliano pia zimewezesha kuunganisha watu kutoka pembe zote za dunia na kushirikiana iwe katika mawazo, maafa na mambo mengine. Lakini lazima pia kuona hatari inayotokana na urahisi huo wa mawasiliano kati ya watu. Mtandao kwa mfano unatoa changamoto kubwa sana kwa watu wa marika yote pale unapotumika kudhalilisha ubinadamu, kuunganisha magendo, kupanga njama za kigaidi, kusambaratisha ndoa n.k. Hivyo ni lazima kwa wanafamilia ya Mungu kuelimishwa namna bora ya matumizi ya mtandao.

Mpendwa msikilizaji, wakati ukuta. Kufikia hapa tumefikia mwisho wa kipindi chetu kwa siku ya leo. Mungu akubariki katika yote, akuzidishie imani, matumaini na mapendo. Nikikuaga kutoka studio za Radio Vatican ni mimi mtayarishaji na msimulizi wako Padre George wa Bodyo.










All the contents on this site are copyrighted ©.