2012-10-12 09:42:29

Imarisheni huduma za afya kuzuia ugonjwa wa upofu duniani!


Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka ifikapo tarehe 11 Oktoba, inaadhimisha Siku ya Vipofu Duniani. Taarifa za Shirika la Afya Duniani zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya wagonjwa wenye tatizo la macho wapatao millioni mia mbili na themanini na tano duniani na kati yao kuna watu millioni thelathini na tisa ni vipofu kabisa. Tatizo la upofu linaendelea kukua na kuongezeka kwa kasi Barani Afrika, Asia na Amerika ya Kusini na katika baadhi ya nchi za Ulaya.
Takwimu za Shirika la Afya Duniani zinaonesha kwamba, kuna jumla ya watoto millioni sita ambao wanakabiliwa na upofu, kati yao kuna watoto millioni nne ambao ikiwa kama wangepata huduma bora ya afya na tiba wangeweza kusalimisha uwezo wao wa kuona, lakini kwa vile wanaishi vijijini ambako mara nyingi huduma za afya bado ni duni, wamejikuta wanakabiliwa na upofu.
Kutokana na changamoto hii, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa, Serikali na watu binafsi kuongeza jitihada za kuboresha tiba kwa kukazia kwa namna ya pekee, kinga dhidi ya magonjwa yote yanayoweza kupelekea upofu kwa watu. Jitihada hizi hazina budi kutekelezwa tangu watoto wakiwa wachanga. Ni changamoto pia kwa Jamii kujenga utamaduni wa kuwaheshimu, kuwathamini na kuwasaidia vipofu katika shida na mahangaiko yao, ili waweze kujisikia kuwa hata wao ni sehemu ya Jamii inayowazunguka licha ya matatizo wanayokabiliana nayo.
Utu na heshima yao kama binadamu vinapaswa kuzingatiwa na pale inapowezekana, basi wajengewe uwezo wa kujitegemea wao wenyewe. Inasikitisha kuona kwamba, vipofu wamekuwa ni kero katika mitaa ya miji mingi duniani, watu ambao wanatangatanga barabarani ili kupata riziki yao, huku wakisaidiwa na watoto wadogo ambao kimsingi walipaswa kuwa shuleni wakisoma, matokeo yake, hata watoto hawa wanajikuta wakitumbukia katika mzunguko wa umaskini kwa kukosa elimu ambayo ni msingi na mkombozi mkuu wa mwanadamu.








All the contents on this site are copyrighted ©.