2012-10-12 11:03:00

Huu ni muda muafaka wa kujikita katika Uinjilishaji wa kina!


Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, baada ya kuwa pamoja katika tafakari ya Hati ya Baba Mtakatifu Benedikto XVI, Africae Munus, nakukaribisha tena katika mfululizo wa vipindi vyetu vya uinjilishaji wa kina. Katika juma hili, tukizingatia kuanza kwa Sinodi ya Maaskofu juu ya uinjilishaji mpya hivi karibuni, basi tuangalie japo kwa ufupi nini Mama Kanisa anawaongoza Maaskofu kujadili ili kuboresha na kuimarisha utume wa Kanisa kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi wa Yesu.

Katikati ya mwezi wa Tisa mwaka huu, Baba Mtakatifu Benedikto XVI alitoa hati (linieamenta) ambayo ni kama chombo cha kufanyia kazi na Maaskofu wa Sinodi juu ya uinjilishaji mpya. Katika hati hii Baba Mtakatifu anaanza kwa kufanunua dhana nzima juu ya uinjilishaji mpya hususan nini maana ya uinjilishaji mpya na uhitaji wake leo katika Kanisa. Dhana ya uinjilishaji mpya ilianza na Mwenye heri Yohane Paulo wa Pili, alipotembelea Poland na baadaye dhana hii ilipata mvuto zaidi alipotembelea Amerika ya Kusini.

Mwenye Heri Yohane Paulo wa Pili, akiwa Amerika ya Kusini, aliitumia dhana ya Uinjilishaji mpya akitaka kuamusha tena miongoni mwa wanafamilia ya Mungu Amerika ya Kusini ile nguvu, ari na kasi mpya ya uinjilishaji barani Amerika ya kusini baada ya uinjilishaji wa awali kufanyika. Kumbe uinjilishaji mpya unabeba pamoja na mambo mengine ari, kasi na nguvu mpya ya uinjilishaji kwa kutumia mbinu mpya na njia mpya za uinjilishaji katika mazingira ya mapya yenye muonekano, mahitaji, matatizo na mtazamo mpya kuhusu maisha na jamii.

Tunapozungumzia uinjilishaji mpya haimaanishi kuwabatiza watu upya au kubadilisha Injili, bali kumpeleka Kristu ndani kabisa katika maisha ya mtu ya kila siku mahali pale alipo. Uinjilishaji mpya hauishii kutangaza tu Imani ya Kristu bali kuwafanya waumini kumwelewa zaidi Kristu na ujumbe wake ndani kabisa ya maisha yao ya kila siku.

Uinjilishaji Mpya unalenga kumuwezesha muumini kuiishi imani yake kwa kujiamini zaidi kwani kwayo anaona njia ya kufuata, anapata ukweli kuhusu maswali mengi ya maisha na hatimaye uzima utokanao na ushuhuda wa maisha ya Imani aliyoipokea na kuiamini tangu alipobatizwa. Katika ujumla wake uinjilishaji mpya unalenga kutangaza ufalme wa Mungu katika mazingira mapya katika maana kwamba Binadamu ameongezeka kimo na akili katika kuutawala ulimwengu wake.

Maendeleo ya sayansi na teknologia ambayo yamepelekea kuongezeka kwa ustawi wa jamii, utandawazi ambao umepelekea dunia kuwa ndogo kama kijiji, kuongezeka kwa ushirikiano miongoni mwa mataifa kwa upande mmoja; na ongezeko la watu, kupungua kwa kasi kwa rasilmali za dunia, migogoro ya kisiasa nyuma ya tofauti za kiimani, ugumu wa maisha kwa watu wengi, kuyumba kwa uchumi wa kimataifa, na kuongeza kwa biashara haramu ya dawa za kulevya na watoto ni miongoni mwa mambo ambayo yaipa sura mpya dunia ya leo ambamo Kanisa linaishi na kuendeleza utume wake.

Katika mazingira hayo Kanisa linawajibika bado kuendeleza utume wake wa awali kumpeleka Kristo kule ambako bado hajafika lakini zaidi kuwaimarisha wale walikwishakumpokea Kristo tayari. Ili kufanya vizuri katika utume wake Kanisa halina budi kuwaimarisha watoto wake nyumbani ili waweze kuwavuta watoto wenzao huko barabarani na kuwaleta nyumbani. Changamoto za maisha ya dunia ya leo hazijaliacha Kanisa salama. Wanafamilia ya Mungu wanapambana na changamoto hizi kumbe wanahitaji majibu sahihi kukidhi changamoto hizi.

Leo hii ambapo Makanisa mengi mahali pengi yamegeuzwa kuwa kumbi za starehe, kupungua kwa miito ya Upadre na Utawa, kusambaratika kwa thamani ya ndoa na familia miongoni mwa vijana ni mambo ambayo Kanisa lazima litulie na kubuni mbinu mkakati za kuweza kurudisha tena Imani ya Kanisa miongoni mwa watu.

Mpendwa msikilizaji kwa kifupi huo ndio uinjilishaji mpya. Naomba nikutakia Baraka tele toka kwa Mwenyezi Mungu na kukushukuru sana kwa kuwa nami kwa muda wote huu. Tuonane tena juma lijalo wakati na wasaa kama huu. Kutoka studio za Radio Vatican ni mimi mtayarishaji na msimulizi wako Padre George wa Bodyo.








All the contents on this site are copyrighted ©.