2012-10-09 09:31:50

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika barua yake ya kichungaji “Porta Fidei” ametangaza maadhimisho ya Mwaka wa Imani utakaofunguliwa rasmi hapo tarehe 11 Oktoba 2012, kumbu kumbu ya Jubilee ya miaka hamsini tangu Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ulipofunguliwa. Mwaka wa imani utahitimishwa rasmi katika maadhimisho ya Siku kuu ya Kristo Mfalme wa Ulimwengu hapo tarehe 24 Novemba, 2013. tarehe 11 Oktoba 2012 ni kumbu kumbu ya miaka ishirini tangu Katekesimu Mpya ya Kanisa Katoliki ilipochapishwa kwa mara ya kwanza, chini ya uongozi wa Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, akipania kuwaonesha waamini nguvu na uzuri wa imani. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu anasema, mlango wa imani daima uko wazi na unaendelea kutoa mwaliko kwa waamini kujenga uhusiano na Mwenyezi Mungu kwa njia ya Kanisa. Inawezekana kabisa kujenga uhusiano huu ikiwa kama Neno la Mungu linahubiriwa na mioyo ya waamini inaruhusu Neno hili kuleta mabadiliko ya ndani katika maisha kwa njia ya neema.

Tangu mwanzo Baba Mtakatifu anasema, amekuwa anawahimiza waamini kugundua hija ya imani itakayowawezesha kuona mwanga wa furaha ari mpya ya kukutana na Yesu Kristo. Miaka iliyopita ilikuwa ni rahisi kwa jambo hili kutokana na mwelekeo wa kitamaduni uliokuwepo na kukubalika mintarafu miongoz ya imani na tunu msingi za maisha ya kiroho. Lakini, kwa sasa hali imebadilika sana kutokana na mmong’onyoko wa tunu msingi za maisha ya kiimani, kiutu na kimaadili ambao umewakumba watu wengi duniani.

Itakumbukwa kwamba, Mwezi Oktoba, 2012, kutakuwepo na Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu Uinjilishaji Mpya, inayoongozwa na kauli mbiu “Uinjilishaji mpya kama njia ya kurithisha imani ya Kikristo”. Hiki kitakuwa ni kipindi muafaka kwa Mama Kanisa kufanya tafakari ya kina pamoja na kuendelea kutambua umuhimu wa imani, kama sehemu ya mwendelezo wa Mwaka wa Imani uliotangazwa na Papa Paulo wa sita, kunako Mwaka 1967; mwaka ambao ulihitimishwa kwa kuchapisha “Kanuni ya imani ya Watu wa Mungu”, ili kuonesha maudhui ya imani ambayo yamekuwa ni urithi wa Mama Kanisa kwa miaka mingi; imani ambayo haina budi kudumishwa, kufahamika na kufanyiwa tafakari ya kina kila wakati, ili hatimaye, waamini waweze kuitolea ushuhuda mintarafu mazingira ya kihistoria, pengine tofauti kabisa na hali ilivyokuwa kwa miaka iliyopita.

Baba Mtakatifu anasema, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani yamekuja wakati muafaka kabisa, Mama Kanisa anapoadhimisha Jubilee ya Miaka Hamsini tangu Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ulipofunguliwa, mwaliko kwa waamini kutafakari kwa makini urithi mkubwa unaofumbatwa katika hati mbali mbali zilizotolewa na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, nguvu na ari mpya katika maisha na utume wa Kanisa.

Mama Kanisa anaendelea kushuhudia mabadiliko kutokana na ushuhuda unaotolewa kwa njia ya maisha ya watoto wake; uwepo wao duniani na kwamba, Wakristo wanaalikwa kuonesha nuru ya mwanga wa ukweli, walioachiwa na Yesu Kristo mwenyewe. Mama Kanisa anatambua kwamba, miongoni mwa watoto wake kuna wadhambi, lakini ni Takatifu na daima linahitaji kujitakasa.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anasema, Mwaka wa Imani unalenga kuleta mwamko mpya katika wongofu wa ndani kwa Yesu Kristo Mkombozi wa Ulimwengu. Kwa njia ya Fumbo la Pasaka amedhihirisha Pendo linalookoa na hivyo, huu ni mwaliko wa kuongoka kwa njia msamaha wa dhambi, ili kuweza kukumbatia maisha mapya yanayojikita katika imani, inayomletea mwamini mabadiliko ya ndani na ukweli mpya kwa njia ya Ufufuko. Hii ni imani inayotenda kwa njia ya upendo, kigezo kipya cha uelewa na matendo yanayoleta mabadiliko katika maisha ya mwanadamu.


SEHEMU YA PILI: MLANGO WA IMANI

Kwa njia ya upendo wake wa dhati, Yesu Kristo aliweza kuwavuta watu wa nyakati zote; kwa njia ya Kanisa lake, anaendelea kuwaalika wengine pamoja na kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, changamoto ambayo daima ni endelevu. Kanisa linakabiliwa na changamoto ya Uinjilishaji ili kuwawezesha waamini kutambua ile furaha ya kuamini na kushirikisha imani yao. Waamini wanapaswa kugundua upendo wa Kristo kila siku ya maisha yao; kwa kujitoa kwa ajili ya kazi za kimissionari, ili iweze kusonga mbele. Imani inakuwa pale tu inapomwilishwa kwa njia ya mang’amuzi ya upendo unaopokelewa kwa dhati na kuwashirikisha wengine kama mang’amuzi ya neema na furaha.

Kwa kuamini anasema Baba Mtakatifu, imani inakuwa na kuimarika zaidi, kiasi kwamba, inakuwa ni vigumu kwa mwamini kuipatia kisogo, kwani hata upendo kwa Mwenyezi Mungu utakuwa unaimarika zaidi, kwani Yeye ndiye chemchemi ya upendo huo. Mama Kanisa anapenda kuadhimisha Mwaka wa Imani kwa ari kubwa zaidi, ili uweze kuzaa matunda yanayokusudiwa. Tafakari kuhusu imani haina budi kuimarishwa zaidi, ili kuwawezesha waamini kumfahamu Kristo zaidi na kujishikamanisha na Injili, hasa wakati huu ambapo mwanadamu anashuhudia mabadiliko makubwa katika maisha yake.

Ni kipindi cha kuungama imani kwa Kristo Mfufuka, ili kila mwamini aweze kuifahamu vyema, ili hatimaye, kuirithisha kwa kizazi cha sasa. Jumuiya, Parokia na Vyama vya Kitume vinachangamotishwa kutafuta njia ambayo itawawezesha kuungama imani yao hadharani katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Mama Kanisa anapenda kuona watoto wake wakiungama imani yao katika ukamilifu wake, kwa mwamko na ari mpya zaidi, kwa kujiamini pamoja na kuwa na matumaini makubwa zaidi. Iwe ni fursa ya kuimarisha imani katika Liturjia na kwa namna ya pekee katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, kiini na kilele cha maisha na utume wa Kanisa. Ni changamoto kwa waamini kutoa ushuhuda unaoaminika. Waamini watambue maudhui yaliyomo kwenye Kanuni ya Imani wanayoungama, wanayoadhimisha, ishi na kusali; mintarafu imani inayomwilishwa katika maisha ya kila mwamini.

MLANGO WA IMANI SEHEMU YA TATU

Imani si jambo binafsi anasema Baba Mtakatifu, bali inapaswa kushuhudiwa katika maisha ya hadhara. Hili ni tendo huru linalohitaji uwajibikaji na utendaji wa maisha ya kijamii kwa mtu anaye amini. Imani ni jambo binafsi linalofumbata pia maisha ya Kijumuiya. Imani ni urithi wa Kanisa, ni urithi wa Jumuiya ya waamini na kwa kila Mbatizwa anayo alama isiyofutika inayomshirikisha katika kundi la watu wanaoamini ili kupata uzima wa milele.

Maudhui ya Imani ni jambo la msingi, ili kumwezesha mwamini kuikiri kwa akili na utashi wake, kile ambacho Kanisa linafundisha. Ufahamu wa kiimani unamfungulia mwamini uelewa mpana wa Fumbo la Ukombozi lililofunuliwa na Mwenyezi Mungu. Mwamini anapokubali kwa akili na utashi wake inamaana kwamba, anakubali kimsingi Fumbo la Imani, kwani Mungu ndiye anyemhakikishia ukweli wake na kumpatia fursa ya kuonja pendo lake.

Baba Mtakatifu anasema, imani haina budi kuzingatia pia tunu msingi za maisha ya kitamaduni, kwani hata kama kuna umati mkubwa wa watu ambao hawana imani, lakini, wako katika hija ya kutafuta ukweli kuhusu maisha yao hapa duniani. Hija hii ya imani inawaongoza katika kulifahamu Fumbo la Mungu. Daima akili inatafuta kile kilichochema na kinachodumu; kwani haya ni mambo ambayo yamepigwa chapa katika moyo wa mwanadamu na yanapata utimilifu wake katika Mungu mmoja. Imani inatoa mwanya kwa waamini kuuona utimilifu wake.

Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki ni nyenzo msingi katika kuifahamu imani ya Kanisa kwa muhtsari. Haya ni matunda makuu ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, changamoto katika maadhimisho ya Jubilee ya miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, kugundua tena na tena ile misingi ya imani, kama inavyopembuliwa kwa kina na mapana katika Katekesimu Mpya ya Kanisa Katoliki na jinsi ambavyo waamini wanaweza kuimwilisha imani hii, baada ya kushiriki katika tafakari ya kina iliyofanywa na Mama Kanisa. Ni nyenzo muhimu katika majiundo endelevu kwa waamini mintarafu tamaduni za watu husika. Kanisa linaandaa mwongozo maalum utakaowawezesha waamini kuadhimisha kikamilifu Mwaka wa Imani, mintarafu azma ya Uinjilishaji.

Baba Mtakatifu anasema, kuliko ilivyokuwa miaka kadhaa iliyopita, waamini leo hii wanakabiliana na maswali magumu katika hija ya maisha yao kutokana na mabadiliko ya mwono; maendeleo ya sayansi na teknolojia yanayokuja kwa kasi katika Ulimwengu wa Utandwazi. Kanisa daima linapenda kuonesha kwamba, hakuna kinzani kati ya Sayansi na Imani, kwani njia zote hizi zinapania kuufikia ukweli.

Mwaka wa Imani, uwe ni muda wa kufanya hija ya historia ya imani ya Kanisa, inayofumbata utakatifu wa maisha na uwepo wa dhambi. Kuna maelfu ya watoto wa Kanisa ambao wamejitoa kimaso maso katika mchakato wa kumletea mwanadamu maendeleo endelevu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao. Kwa wale ambao wanaogelea katika lindi la dhambi na mauti, ni mwaliko wa kutubu na kuongoka, ili kuonja kwa mara nyingine tena huruma ya Mungu katika maisha yao.

Baba Mtakatifu anasema, Mwaka wa Imani kiwe ni kipindi cha kutolea ushuhuda matendo ya huruma, kwani imani inamwilishwa katika matendo. Watoto wa Kanisa wamekuwa na utamaduni wa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili huduma ya upendo kwa jirani zao; hasa kwa wale wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii, wapweke, wasiopendwa wala kuthaminiwa na jamii inayowazunguka; Wote hawa kwa namna moja au nyingine wanaonesha ile sura ya Kristo. Kwa njia ya imani, waamini wanaweza kuitambua Sura ya Kristo Mfufuka anayeomba kuonjeshwa upendo wa dhati.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuwa na imani thabiti katika hija ya maisha yao ya kiimani na kamwe wasikumbwe na uvivu. Imani inapaswa kuandamana na waamini wenyewe katika maisha yao, daima wakijitahidi kuiuisha kwa ari na nguvu zaidi, kama kielelezo cha matendo makuu ya Mungu katika maisha ya mwanadamu. Ni mwaliko wa kusoma alama za nyakati na kwamba, imani inamchangamotisha mwamini kuwa ni alama hai ya uwepo wa Kristo Mfufuka ulimwenguni.

Baba Mtakatifu anasema, ulimwengu wa leo unahitaji kuona mashahidi amini wanaojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani zao, ili kuweza kuzima kiu ya watu wanaomtafuta Mungu katika maisha, ili hatimaye, waweze kupata maisha yenye uzima wa milele.








All the contents on this site are copyrighted ©.