2012-10-08 14:52:21

Tatizo la ugumba na tamaa ya kupata watoto!


Ndugu msikiliza wa Radio Vatican, baada ya kusema kwa kirefu kuhusu uzazi kwa njia ya asili nakualika leo tugeukie upande mwingine tuwatazame wanandoa wasiojaliwa zawadi ya watoto. Tamaa au hamu ya kuwa na mtoto au watoto kwa wanandoa ni matokeo ya upendo kati yao.
Ni matokeo ya ahadi na matumaini wanayokuwa nayo wanandoa ya kujenga familia ambayo hutajirishwa na ujio wa mtoto au watoto. Katika vipindi vichache vijavyo tutazitazama jitihada za wanandoa kutafuta mtoto/watoto hasa pale ugumba unapodhihirika kuwa bayana.
Hamu ya kuwa na mtoto sio tu kwa ajili ya tamaa binafsi bali ni nafasi ya kupokea mtu mwingine, atakayeshiriki baadaye ya maisha pamoja na wazazi wake. Zawadi ya mtoto/watoto ni baraka toka kwa Mungu (Mwanzo 4:1) kwa wazazi. Naomba ndugu msiklizaji naomba turejee tena katika fikra za mwafrika kuhusu mzao. Lengo kuu la ndoa ni kuzaa mtoto au watoto hivyo kwa mwafrika maana ya ndoa hutoweka endapo hakuna mzao.
John Mbiti mwandishi mashuhuri kutoka Afrika anasema “Anayekufa bila mzao amezima moto wa maisha kwani hana wa kumkumbuka au kumtolea ubani.” Kukosa uzao barani Afrika kuliongeza uke wenza na mahusiano mengi ya kimapenzi nje ya ndoa.
Matokeo yake ni ongezeko la magonjwa na vifo kutokana na baadhi ya wanandoa kukosa uaminifu kwa wenzi wao wa ndoa kwa lengo la kutafuta mtoto kwa udi na uvumba. Hapa inabidi pia kukumbuka athari za nyumba ndogo katika mshikamano na mapenzi ya dhati ndani ya familia, kwani Yesu anasema huwezi kuwatumikia Mabwana wawili!
Leo hii maendeleo ya sayansi na teknolojia yamekuwa msaada mkubwa katika hili kwani wana-ndoa huweza kusaidiwa kupata mzao. Kwani matatizo mengine ya uzazi yanahitaji tiba ya kawaida ambayo haitenganishi tendo la ndoa na uzazi.
Kwa kawaida wanandoa wanapokamilisha ndoa yao hutegemea mzao na mara mtoto asipokuja mahangaiko huwajia. Jitihada zao huwasukuma kwenda kumwona daktari ambaye naye hufanya vipimo na kuona jinsi ya kuwasaidia. Wakati mwingine jitihada za wazazi huleta matunda mazuri wanaposaidia kupata uzao katika njia ya kawaida. Wakati mwingi hufikia mahali pa kuhuzunisha wanapoambiwa kwa uhakika kuwa sio rahisi kupata mtoto kwa njia ya kawaida na huku wakiendelea kudumisha uaminifu wa muungano wa kindoa kati yao.
Hiki ni kipindi kigumu sana kwa wanandoa kwani matumaini waliokuwa nayo ya kujenga mji wenye furaha pamoja na zawadi ya watoto wao hutoweka. Kweli hapa isipotumika busara ya kichungaji hata ndoa iliyo na tabia ya umoja usiogawanyika huingia hatarini. Na wakati mwingine huingia katika tamaa ya kutafuta mtoto hata kwa njia ya kumtengeneza katika maabara kwa ushirikiano na daktari ambalo tutalisema katika kipindi kijacho, jambo ambalo lina hatari kubwa.
Wakati mwingine, wanandoa kama hawa wanaweza kujikuta wamejiingiza katika vitendo vya kishirikina. Wanandoa wasipokuwa makini kwa jambo hili wanaweza kufilisika na hatimaye ndoa yao kubomoka kwa kuendekeza ushauri wa waganga wa kienyeji. Ni vyema ikiwa kama wanandoa watapata ushauri wa kina kutoka kwa wataalam wa masuala haya.
Kutoka Studio za Radio Vatican ni mimi Padre Raphel Mwanga, wa Jimbo Katoliki la Same, Taasisi ya Ndoa na Familia, Chuo Kikuu cha Kipapa Laterano- Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.