Padre Theodorus Johaness Slaat wa Jimbo Katoliki Mbeya afariki dunia!
Simanzi na majonzi makubwa yamemkumba Askofu Evarist Chengula(IMC) wa Jimbo Katoliki
la Mbeya, mapadre,watawa wa kike na kiume pamoja na waamini wote baada ya kumpoteza
aliyekuwa Katibu wa Askofu na mshauri wa Jimbo aliyefariki tarehe 4 Oktoba 2012 majira
ya saa saba kasorobo nyumbani kwake uaskofuni.
Wingu la vilio na simanzi limetanda
wakati mwili wa Paroko wa Kanisa la Roho Mtakatifu,Parokia ya Ruanda, Padre Theodorus
Johannes Slaats kupokelewa tarehe 8 Oktoba, 2012 na mapadre,watawa na waumini wa
Jimbo la Mbeya waliokuwepo kanisa la Ruanda kuupokea mwili wake kutoka katika chumba
cha kuhifadhia miili ya marehemu katika Hospitali ya Meta Rufaa,Mbeya majira ya saa
9.00 mchana kwa ajili ya misa na mkesha hadi tarehe 9 Oktoba, 2012 anapokwenda kuhifadhiwa
katika nyumba yake ya milele.
Akizungumzia wasifu wake,Paroko msaidizi wa Parokia
ya Roho Mtakatifu,Padre Deus Tarimo alisema marehemu padre Slaats aliyefariki akiwa
na umri wa miaka 82 alizaliwa huko Eindhoven,Uholanzi Novemba, 3 mwaka 1930 akiwa
ni mtoto wa saba katika familia ya watoto 12 na kubatizwa siku hiyo hiyo katika Kanisa
la Mt.Theresia Trudo huko Uholanzi.
Padre Tarimo alisema marehemu alipata
sakramenti ya kipaimara mei,17,1939, elimu ya msingi katika shule ya Msingi ya Mt.Theresia
mwaka 1937 hadi 1940 na baadaye alihamia katika shule ya msingi Jan Smitslaan mwaka
1940 hadi mwaka 1943 huko Eindhoven na baadaye kujiunga na seminari ndogo ya shirika
la Roho Mtakatifu, Weert mwaka 1943 hadi 1950.
Alisema baadaye aliendelea
na malezi ya Novisiati katika Shirika hilo huko Gennep Uholanzi mwaka 1950 na kuweka
nadhiri zake za kwanza Sept,7,1951 hadi mwaka 1952 alifanya masomo ya falsafa katika
seminari kuu ya Shirika hilo huko Gemert,Uholanzi, masomo ya Taalilimungu katika
chuo kikuu cha Gregoriana, Roma, Italia (1953-1957), nadhiri za daima(1954) huko Gemert,
Uholanzi, daraja takatifu la ushemasi katika kanisa la Mt. Marcelli, Roma, Italia
(1956).
Padre Tarimo alisema padre Slaats alipata daraja takatifu la upadre
mwaka 1956 ambapo mwaka 1957 alitumwa kufanyakazi za umisionari nchini Tanzania na
utume wake ulianzia Parokia ya Kisanga,jimbo Katoliki la Morogoro, mwaka 1958 alihudumu
Parokia ya Matombo Morogoro na mwaka 1962 hadi 1964 alikuwa mratibu Taaluma na mwalimu
katika seminari kuu ya Mt.Thomas, Morogoro huku akifundisha dini katika chuo cha
ualimu kigurunyembe,Sekondari ya Mzumbe na Chuo cha Marian kwa sasa ni Sekondari
ya Kilakala.
Alisema marehemu Padre Slaats alihudumu kama Mkurugenzi wa Idara
ya Katekesi na afya Jimbo Katoliki la Morogoro,mwaka 1971 aliombwa na Mhashamu Askofu
James Sangu wa Jimbo Katoliki la Mbeya kufanyakazi ya Ukatibu na Paroko wa Parokia
ya Mwanjelwa hadi mwaka 1983.
Enzi za uhai wake Padre Slaats amewahi kuwa Mkuu
wa chuo cha ufundi cha Ruanda (1985-1996), mwaka 1997 baada ya kusimikwa Askofu mpya
wa Jimbo Katoliki la Mbeya, Askofu Evarist Chengula, aliteuliwa kuendelea na kazi
ya Ukatibu na chancela wa Jimbo na baadaye aliomba kuanzisha Parokia mpya ya Ruanda
ambapo Askofu Chengula alimsimika kuwa Paroko mwaka 2003.
Alisema Padre Slaats
aligundulika kuwa na ugonjwa wa Saratani kunako mwaka 2004 na kwa nyakati tofauti
alikuwa akipata matibabu katika Hospitali mbalimbali ndani na nje ya Nchi na lakini
aliendelea kujitoa na kuchapa kazi katika nafasi zote hadi alipokwenda nchini Uholanzi
kwa matibabu mwezi januari,mwaka huu na kurudi mwezi juni na afya yake iliendelea
kudhoofika huku akihudumiwa katika Hospitali ya Rufaa Mbeya.