Mwili wa Kardinali Laurean Rugambwa kuzikwa upya Bukoba
Mwili wa Mwadhama Laurean Kardinali Rugambwa , utazikwa rasmi katika Kanisa Kuu
la Jimbo Katoliki la Bukoba octoba 6 mwaka huu, wakati huo kesho yake th 7oktoba
kufanyika sherehe za kutabaruku kanisa katoliki baada ya kumalizika ukarabati mkubwa
uliochukua takribani miaka 17. Aidha sherehe za kutabaruku kanisa katoliki la Jimbo
la Bukoba linaenda sambamba na sherehe za kuadhimisha miaka 100 tangu kuzaliwa kwa
kiongozi huyo aliyekuwa Kardinali wa kwanza nchini Tanzania na afrika kwa ujumla.
Hili kuelewa zaidi juu ya Mwadhama Kardinali Rugambwa , ufasaha wa maisha yake, moyo
wake, kazi zake za kitume, upendo wake na mambo mengi turudi nyuma katika makala iliyoandikwa
na aliyekuwa wakati ule Padre Method Kilaini kwa magazeti mbalimbali mara baada ya
kifo cha mwadhama Desemba 1997. Padre Kilaini wakati huo alikuwa Katibu Mkuu wa Baraza
la Maaskofu Katoliki Tanzania. Katika makala hii itatupatia kina cha kujua historia
nzima ya huo mwadhama. Padre Methodius Kilaini sasa ni Askofu msaidizi wa Jimbo katoliki
la Bukoba ambaye alitumwa Roma na Mwadhama mwaka 1968 kusomea Upadre. Na hata baadaye
alikuwa karibu sana naye kiasi kwamba ndiye aliyemwachia kuwa msimamizi wa mirathi
yake. Naye Baba Kilaini aliandika makala hiyo kwamba; mwaka 1968 wakiwa Roma Kardinali
Rugambwa alikuja kikazi Roma, ikawa bahati ya kumsindikiza mjini Roma na Vatikani.
Kwa mara ya kwanza alielewa ukubwa wa kardinali na alipolinganisha na jinsi alivyotendewa
pale ndipo alitambua unyenyekevu wake. Huko nyumbani kwao Bukoba na Tanzania kwa
ujumla watu hawakujua wamwiteje ndipo wakatengeneza maneno ya 'Nyakutununta' kwa kihaya,
na Mwadhama kwa kiswahili. Kardinali katika Kanisa Katoliki lenye waumini zaidi
ya bilioni moja, alikuwa ni mmoja wa watu bawaba au wa msingi 130 katika kanisa hilo.
Kikanisa yeye alikuwa yuko juu ya maaskofu, maaskofu wakuu, balozi wa Baba mtakatifu
na wengine. Kidiplomatia hupokelewa kama Mwana Mfalme. Yeye alikuwa anashiriki katika
uchaguzi wa Baba Mtakatifu,hivyo (Rugambwa alishiriki kuwachagua Baba Watakatifu
watatu). Aliendelea kueleza kuwa anakumbuka mwaka 1992, Baba Mtakatifu Yohana
Paulo II akiwapokea maaskofu wa Tanzania alimwita mwana wa kwanza wa kanisa la Afrika.
Aliwaambia maaskofu kwamba anamheshimu sana kwa sababu alimtangulia kama Kardinali.
Rugambwa alikuwa mjumbe katika kamati na tume mbali mbali huko Vatikani ikiwemo ile
ya Liturujia na ile ya Uenezaji Injili. Kama Kardinali alipewa kanisa lake la kudumu
Roma, kanisa la zamani sana la Mtakatifu Fransisco wa Ripa. Mwaka 1992 akisherehekea
miaka 40 ya Uaskofu aliweza kuwaalika maaskofu wa Tanzania katika kanisa ambako walipokelewa
vizuri na waumini wake. Waumini hao walimpenda na kujivunia kuwa na kardinali wa kwanza
wa Afrika kama kardinali wao wa pekee. RUGAMBWA ALIKUWA HESHIMA YA WATU WEUSI Baada
ya kuteuliwa kuwa kardinali alipotembelea nchi za Ulaya na Marekani alipokelewa vizuri
sana na heshima zote za kiserikali. Ikumbukwe kwamba wakati huu ulikuwa bado wakati
wa ukoloni katika nchi karibu zote za Afrika. Kupitia kwake mtu mweusi aliheshimiwa
na kukubalika kwa wote. Ulaya hasa Italia, Ujerumani, Uholanzi, Ubelgiji na Austria
alipokelewa na viongozi wa juu wa serikali. Ujerumani alionana na Raisi, Waziri Mkuu
na kuiongelea Bundestag ambalo ndilo bunge la Ujerumani. Hii ilikuwa heshima kubwa
sana ambayo walikuwa hawapewi hata wakuu wa serikali. Huko Marekani alihutubia
katika vyuo vikuu vingi vilivyomtunuku shahada za juu za udaktari wa heshima. Alikutana
na vingozi wa marekani weusi ambao walijionea sifa sana kwake. Katika yeye walijivuna
kuwa weusi na kukumbuka kwamba wao ni watoto wa Afrika. Kwa mara ya kwanza wamarekani
weusi walimwona mwafrika aliyepata cheo kikubwa kama hicho, hata na wazungu wa marekani
ingawa waliwadharau watu weusi walimheshimu sana. Makardinali weupe wa Marekeni kama
Kardinali Cushing, walimkaribisha majimboni kwao kwa heshima kubwa. Hivyo wote walimwona
kama ishara ya uwezo wa mtu mweusi katika harakati zao za kupigania usawa huko marekani.
Walianza kujihusisha na kanisa la Afrika. RUGAMBWA ALIKUWA KIUNGO CHA UPATANISHI
KWA WOTE. Rugambwa alikuwa askofu wa tatu mwafrika na kardinali wa kwanza wa bara
la Afrika. Maaskofu wa Afrika walimtambua na kumkubali kama kiongozi wao. Wakati wa
Mtaguso Mkuu wa Vatikano II (1962-65) uliohudhuliwa na maaskofu zaidi ya 3,000 yeye
alikuwa askofu mwafrika pekee aliyepewa fursa ya kuhutubia maaskofu wote kwa pamoja
katika ukumbi mkuu katika miaka yote mitatu ya mkutano huo. Hata wazungu ni wachache
sana waliopewa fursa hiyo. Wakati wa mtaguso huo aliwaita pamoja maaskofu wote
kutoka Afrika (wengi wao wakiwa wamisionari wazungu) na yeye akiwa mwenyekiti wao
zilianza harakati za kuundwa umoja wa maaskofu wa Afrika, (SECAM). Vivyo hivyo Rugambwa
alikuwa kiuongo cha kusaidia kuunda umoja wa maaskofu wa Afrika ya Mashariki, zikiwemo
nchi za Eritrea, Ethiopia, Somalia, Sudan, Kenya, Uganda, Tanzania, Malawi na Zambia,
(AMECEA). Mpaka alipofariki alikuwa bado baba mlezi wa umoja huo. Kwa sababu hiyo
alikuwa mjumbe wa kudumu wa kamati tendaji, pamoja na kuwa vile vile baba mlezi wa
Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Afrika ya Mashariki ambacho kiko nchini Kenya. RUGAMBWA
NA BARAZA LA MAASKOFU KATOLIKI TANZANIA Rugambwa alikuwa ni mmoja wa waasisi wa
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania pamoja na Askofu Mkuu Marantha akiwa askofu mwafrika
pekee katika baraza hilo mwaka 1956. Yeye ndiye aliyewakaribisha maaskofu wengine
waafrika katika baraza hilo na kuwaelekeza. Baada ya kuwa kardinali mwaka 1960 wengi
wao aliwapa uaskofu au aliwasimika katika viti vyao vya uaskofu. Alijiona kama kiungo
chao. Hakutaka hata mara moja kukosa vikao vya baraza hili ikijulikana kwamba kwa
heshima alikuwa mwanachama wa kudumu katika kamati tendaji mpaka alipostaafu. “
Askofu Mathias Joseph Isuja akitoa rambi rambi zake alisema 'Rugambwa alikuwa nguzo
yetu na kiungo chetu. Kule kuwako kwake kulimfanya mtu kushika adabu. Kama mtu hakushika
adabu alimwita na kumwambia neno moja tu na lilitosha.” Kilaini anaendelea; Vile
vile kama alivyoeleza askofu huyo hakuzungumza sana katika vikao vya baraza lakini
ilipofika wakati, akaona kwamba maaskofu kidogo hawakubaliani alisema maneno machache
na ndio ulikuwa mwisho wamabishano. Alipenda sana umoja wa maaskofu na alitaka wawe
kitu kimoja. Mwaka 1967 alikuwa msitari wa mbele katika kuunganisha seminari kuu za
Tanzania ili kuleta umoja. Yeye aliitoa Seminari yake ya Ntungamo iwe kwa ajili ya
Baraza zima. Maaskofu walimpenda na kumheshimu sana. Yeye vile vile aliwapenda
sana. Mfano mmoja ni mwaka 1996 alipoona Askofu Castor Sekwa wa Shinyanga ameugua
sana na ukawa muda mrefu bila kumwona, alifunga safari mpaka Shinyanga kumtia nguvu
na kumpa moyo licha ya barabara mbaya ingawa yeye tayari alikuwa ameanza kuwa mnyonge
kiafya. Alibaki naye zaidi ya wiki moja wakati wa pasaka.
Mwezi wa saba akiwa
kitandani baada ya kutembelewa na maaskofu alimwambia Kilaini kuwa: 'Mwanangu najisikia
vizuri nikiwaona maaskofu'. Kwa kawaida Mwadhama alikuwa hataniani sana lakini alipokuwa
na maaskofu hasa kama Askofu Isuja wa Dodoma, Marehemu Askofu Sekwa wa Shinyanga,
Amedeus aliyekuwa wa Moshi na wakati huu ni askofu wa Mwanza, hata na maaskofu kama
Askofu Paul Ruzoka aliyekuwa wa kigoma na sasa Tabora na Marehemu Askofu Justin Samba
aliyekuwa wa Musoma na wengine alitaniana nao sana hata kusahau kama ni yeye ambaye
kikawaida alikuwa ni mtu mtulivu mwenye maneno machache. Alitafuta namna ya kuwafanya
wacheke na kujisikia vizuri naye.
Miaka 100 ya kuzaliwa Hayati Kardinali RUGAMBWA Makala
ya Askofu Methodi Kilaini aliyoiandika baadaya ya kifo cha Kardinali Rugambwa Desemba
1997 inaendelea. Hayati Rugambwa hakupenda ukabila. Askofu Mkuu Pengo akitoa buriani
kwa aliyemwita, Baba yetu Rugambwa, aliongelea juu ya uwezo wake wa kuwa juu ya makabila
na vikundi. Akiongelea juu ya kazi yake Dar es Salaam alisema aliweza kuwafanya waumini
wa jiji wajisikie wenye kanisa la Dar es Salaam bila kujali walitoka wapi. Aliwapata
mapadre wa Dar es Salaam, masista wa Dar es Salaam na waumini wa Dar es Salaam. Kardinali
kwao ni Bukoba na Bukoba aliipenda lakini hakupenda ukabila hata kidogo. Akiwa askofu
wa Bukoba baada ya kumaliza nyumba yake ya kiaskofu, aliwaalika masista wa Kilimanjaro
waje kumtunza na kuhudumia katika nyumba yake. Hivyo watawa waliokuwa karibu naye
kumhudumia kwa miaka 34 ya uongozi wake wengi walikuwa ni wachagga. Ni hao vile
vile aliowaleta katika seminari kuu ya Ntungamo na siyo shirika lake la Bukoba. Alifanya
juu chini kutuma wasichana katika shirika hilo la Kilimanjaro ili wapate upeo wa kitaifa.
Kwa moyo huo alipokuja Dar es Salaam alikaribisha mashirika mbali mbali ya watawa
kutoka sehemu zote za Tanzania na kuwaweka katika parokia mbali mbali ili kuwafanya
watanzania wote wajisike nyumbani jijini. RUGAMBWA NA UMOJA WA WAKRISTO NA UELEWANO
NA WAISLAMU Askofu mstaafu kwa sasa Elinaza Sendoro wa kanisa la Kiluteli Tanzania
akitoa rambi rambi zake naye alimtaja Kardinari Rugambwa kama baba wa umoja wa makanisa
Dar es Salaam. Pamoja na Askofu Sambano wa kanisa la Kianglikana walimkumbuka kama
mwanzilishi wa umoja huo na mwenyekiti wake kwa miaka 8. Alihimiza ujenzi wa makanisa
ya pamoja kama lile la hospitali ya Muhimbili. Wakati wa kuifungua aliomba waibariki
kwa pamoja. Huu ni moyo alioukuza katika uongozi wake wote. Kamachumu alikozaliwa
Mwadhama Laureani Kardinali Rugambwa palikuwepo madhehebu matatu yaliyoshindana. Wakatoliki
wakiwa na makao yao katika kilima cha Rutabo, Waluteli wakiwa Ndolage na Waislamu
wakiwa wafanyabiashara tajiri Kamachumu mjini. Kwanza alijitahidi kuelewana na kutoa
ugomvi kati ya wakristo na Waislamu. Aliwaonyesha upendo wake kwa kuwafanya watambue
kwamba analeta maendeleo, elimu na huduma kwa wote bila ubaguzi. Kwa hilo alifanikiwa
kiasi kwamba Waislamu wenye siasa kali walimwita Sheik Mkuu wa Bukoba mkristo asiyebatizwa
lakini yeye hakujali kwasababu ya uwezeo wake wa kuleta upendo na uelewano. Kama
baba wa Mtaguso Mkuu wa Vatikano II aliamini katika umoja wa wakristo. Alilelewa katika
moyo wa Papa Yohana XXIII aliyesema kila wakati 'tafuteni kile kinachowaunganisha
na si kile kinachowatenga' Katibu Mkuu wa Chama cha Biblia Tanzania, Mchungaji Albert
Mongi akituma rambi rambi za chama alikumbuka maneno ya Kardinali Rugambwa ' Jambo
hili (maana yake ya kueneza pamoja Biblia kati ya wakatoliki na waprotestanti) halihitaji
ushawishi. Ikiwa tutashindwa kushirikiana katika huduma ya kuwapa watu Biblia, basi
tutakuwa hatuna la kutuunganisha'. Rugambwa alitumia uwezo wake wote kuleta ushirikiano.
Akiwa Bukoba alishirikiana kwa karibu na Askofu wa Kiluteli, Marehemu Josias Kibira.
Kibira alipochaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kiluteli ulimwenguni, Kardinali
alifanya mpango wakaenda pamoja kumsalimu Papa Paulo VI huko Roma. Picha ya Kardinali
Rugambwa na Askofu huyu wa Kiluteli, Kibira, ilipochapishwa katika gazeti na kalenda
ya gazeti la jimbo la Rumuli, mmoja akiwa mkono wa kulia na mwingine wa kushoto wa
Baba Mtakatifu Paulo VI, iliamsha uelewano na ushirikiano mkubwa kati ya madhehebu
haya makubwa ya kikristo Bukoba. Moyo wake wa ushirikiano uliendelea vizuri hivyo
hata wakati wa sinodi ya Afrika, iliyofanyika Roma 1994, aliyekuwa mrithi wa marehemu
Askofu Kibira, Askofu Mushemba sasa msaatafu alialikwa na Baba Mtakatifu Yohana Paulo
II kuwakilisha kanisa la Kiluteli Afrika katika sinodi hiyo. Hata baada ya kustaafu
kama wakristu walikuwa na kitu chenye utata au walitaka kumwona Raisi wa Tanzania
kwa pamoja kutatua tatizo fulani walimwomba awe kiongozi wao. Yeye alikuwa juu ya
tofauti za kidhehebu au kikabila. RUGAMBWA NI MTU MWENYE UPEO MKUU KATIKA KUELIMISHA
WATU (USHUHUDA WA ASKOFU MSTAAFU NKALANGA) Kilaini aliendelea katika mala yake
; Jioni baada ya mapokezi makubwa ya Mwili wa marehemu Rugambwa Mwanza, alipata fursa
ya kuongea kwa faragha na Mhashamu Askofu Gervase Nkalanga, Askofu mstaafu wa Bukoba
ambaye sasa yuko katika monastri ya wa benediktini wa Hanga. Nkalanga alikuwa parokia
moja na Rugambwa alipotangazwa kuwa askofu, baada ya hapo alitumikia chini yake miaka
11, miaka sita kama katibu wa jimbo wa elimu na miaka mitano kama Askofu Msaidizi.
Kilaini alimuuliza swali moja kuwa Alimwonaje Mwadhama' alimwona uso wa Askofu
Nkalanga ukingara kwa tabasamu na alisema: 'Mwadhama alikuwa na upeo mkubwa ajabu,
hakukata tamaa katika shida'. Muda wote hasa baada ya kupewa jimbo jipya la Rutabo,
likiwa fukara, mwadhama alimwambia kwamba kuna ufunguo mmoja tu kwa shida hizi zote,
yaani kuwapa watu elimu na matatizo mengine wangeweza kuyatatua wao wenyewe. Askofu
Nkalanga aliendelea ; katika miaka kumi na moja aliyotumikia chini ya Mwadhama, ingawa
jimbo lilikuwa fukara hakuna hata siku moja alimwendea kumwomba fedha kwa ajili ya
elimu akamnyima. Nkalanga alisema kwamba hata mapadre wengine walipata hata kumchukia
wakiuliza kwa nini alipata fedha kwa ajili ya shule na wengine hawakupata kwa ajili
ya shughuli nyingine muhimu. Upeo wake wa elimu Kwa Kardinali Rugambwa ulikuwa
ni wa kumwelimisha mtu mzima, kijamii, kifamilia, na kitaifa. Kutimiza hilo alianza
umoja wa 'St. Augustine Social Guild' katika umoja huu aliwaweka pamoja vijana na
watu wazima wenye uwezo na kuwaendeleza kwa pamoja. Wale waliokuwa na akili zaidi
aliwatuma sehemu mbali mbali kwa masomo ya juu hata Ulaya na Marekani. Wengi waliporudi
walichukuliwa na serikali lakini aliendelea kuelimisha tu. Kwa watu wa kawaida
kijijini aliona kwamba hawawezi kuendelea kama hawajifunzi kuweka pesa zao na kupanga
maendeleo yao. Akitumia Marehemu Padre Robert Rweyemamu ambaye baadaaye alikuwa Katibu
Mkuu wa Baraza la Maaskofu, na Padre Peter Mutashobya, aliyewahi kuwa mhasibu wa
jimbo la Bukoba, alianzisha chama cha kukopa, (Credit union) Kilipofanikiwa katika
parokia moja ya Mwemage waliieneza katika jimbo zima na baadaye wakajaribu kulieneza
kitaifa. Watu wengi waliinuka kwa huduma hii. Alipenda kuwaelimisha viongozi akianzia
na mapadre, watawa na walei. Ni kweli ni wengi katika makundi hayo matatu aliowaelimisha
wanaosaidia taifa katika nyadhifa mbali mbali Askofu Nkalanga alisema kwamba mara
nyingi ilikuwa vigumu kuelewa malengo yake kwa sababu yalionekana magumu na ya juu
mno yasiyoweza kutekelezwa. Lakini mwadhama alisema kila mara kwamba itawezekana tu,
na kama kwa mwujiza iliwezekana. Mwishoni wale aliofanyakazi nao walipata imani kubwa
kwake na walitimiza kama Yesu alipowaambia wafuasi wake wawagawie umati wa watu elfu
tano vipande vitano vya mikate na wakafanya. Uhusiano wake na serikali ulikuwa
mzuri kwa sababu yeye alichotaka kwao ni kwamba wampe fursa ya kufanya mema, kujenga
hospitali, mashule na kupewa fursa za kutoa huduma kwa watu. Askofu Nkalanga aliendelea
kwamba; serikali ilipoanza kuzungumzia juu ya kutaifisha shule za kanisa alimwuliza
Kardinali kama angeendelea kujenga au kuacha , na kardinali alimjibu, 'endelee kujenga
ili wapate cha kutaifisha, si shule zitaendelea kuelimisha watu' Kutaifisha haikuwa
shida ya Kardinali mradi bado zinaendelea kulea watoto na vijana. Hii ndiyo sababu
hata baada ya kutaifisha mashule bado aliendelea kuwa karibu a shule zilizotaifishwa. RUGAMBWA
NA UJENZI WA SEMINARI Mwadhama kardinaliRugambwa aliamini kwamba uchungaji hauwezi
kufanikiwa kama hakuna wachungaji wenye akili, ucha Mungu na elimu ya kutosha. Hivyo
nguvu zake za kwanza zilikuwa kuwapata mapadre waliotayarishwa vizuri. Seminari
ndogo ya Rutabo: Alipoteuliwa kuliongoza jimbo changa la Kagera ya chini ambalo
baadaye lilitwa Rutabo alikuwa na mapadre 17 tu wote wa jimbo. Wakat huo kulikuwepo
seminari ndogo ya Bunena na seminari ya sekondari ya Rubya kwa ajili ya jimbo la Bukoba.
Mara alipewa idadi ya watoto ambao angeliweza kupeleka katika seminari hizo. Mara
moja aliona umuhimu wa kufungua seminari yake walau ile ndogo. Mwaka 1958 alifungua
seminari ndogo ya Rutabo iliyowapokea vijana kwa ajili ya darasa la tano. Seminari
hiyo ipo hadi leo na imekwisha elimisha vijana wengi na kutoa mapadre wengi sana.
Seminari Kuu ya Ntungamo Baada ya kuwa askofu wa Bukoba aliona umuhimu wa kuwa
na Seminari Kuu badala ya kuwatuma mafrateli Uganda. Aliomba msaada na kujenga seminari
Kuu ya Mtakatifu Antoni wa Padua pale Ntungamo nje kidogo ya Bukoba mjini. Seminari
hii ilipokea mafrateli wa kwanza wa jimbo la Bukoba na Rulenge mwaka 1964. Mwaka 1967
maaskofu wa tanzania walipomuomba iwe sehemu ya seminari ya taifa alikubali na hadi
leo ni Seminari Kuu ya Falsafa. Seminari Kuu ya Segerea Mwadhama Laureani Kardinali
Rugambwa alipohamishiwa jimbo Kuu la dar es Salaam mwaka 1969, jambo la kwanza aliliotambua
ni kuona changamoto za jiji ambazo zilihitaji mapadre ambao wamezoea kusuguana nazo.
Aliona vile vile kwamba kuwa na seminari Kuu jijini kutaongeza chachu siyo tu kwa
ajili ya jimbo Kuu la Dar es salaam bali kama kitovu cha nchi kutachangia katika kutatua
changamoto za kitaifa. Aliomba pesa na kujenga seminari Kuu ya Segerea ambayo ni sehemu
ya mfumo wa taifa ikiwa kwa ajili ya Tauhidi (Teologia). Sasa inaendelea kutoa matunda
yake. Seminari ya Visiga Juhudi za mwisho katika kuanzisha seminari zilikuwa
Dar es Salaam. Kwa miaka mingi alituma waseminari katika seminari ya Mtakatifu Petro,
Morogoro lakini alivyosema hakupata mapadre wengi. Hapo aliazimia kuanza seminari
ndogo ya Jimbo Kuu la Dar es Salaam ambapo angewafundisha vijana katika mazingira
watakayofanyia kazi. Alijenga seminari hiyo Visiga, nje ya mji wa Dar es Salaam
mkoa wa Pwani. Ilifunguliwa mwaka 1990 na alipostaafu mwaka 1992 vijana walikuwa katika
kidato cha pili. Kilichomfurahisha sana ni pale Umoja wa Wanawake Wakatoliki wa Dar
es Salaam ulipoipokea na kuikumbatia shule hiyo. Kabla hajafariki alipata habari kwamba
imekuwa shule ya nne kitaifa katika mitihani ya kidato cha nne, hii ilikuwa ni faraja
kubwa. Katika majimbo yote matatu aliyoyaongoza, alitayarisha walimu wa seminari
kwa kuwatuma mapadre kujifunza katika vyuo vikuu mbali mbali ndani na nje ya nchi.
MWADHAMA RUGAMBWA NA MAENDELEO YA ELIMU YA WANAWAKE Makala ya baba kilaini
inaendelea; Askofu Nkalanga alisema kwamba akiwa katibu wa jimbo wa elimu mwadhama
alimwambia kwamba asielimishe wavulana tu bali hasa wasichana. Kwani wanawake ndio
walimu wa binadamu. Alipopokea jimbo la Rutabo, wamisionari wote wa Afrika waume kwa
wake waliondoka akabaki na mapadre na watawa wafrika. Mpaka wakati huo watawa
waafrika wa Mtakatifu Tereza wa Mtoto Yesu walikuwa hawajapata elimu ya kutosha kuendeleza
elimu ya wanawake. Hapo ndipo alikwenda kuwatafuta masista wa Kanosa mwaka 1956 waje
kusadia. Walipofika Mugana aliwapa jukumu moja nalo ni kuendeleza wanawake katika
njia yote. Chini ya mama yao aliyekuwa Riveta waligawana kazi. Sr. Josephina
aliona watoto wana nguo zimechanika akaanza shule ya akina mama 300 akiwafundisha
kushona kwa kutumia sindano, kitu kidogo lakini kilileta tofauti sana katika maisha
ya watu, na baadaaye akaanza mambo mengine ya maendeleo ya akina mama, na mwishowe
shule ya maarifa ya nyumbani ya kwanza Bukoba, na baadaye wakaanza vile vile shule
ya kati ya wasichana,.Sr. Carolina akaanza na Sr. Victoria kliniki za akina mama ambayo
sasa imekua na kuwa hospitali kubwa ya Mugana, shule ya wakunga wasaidizi na fani
nyingine. Alivyofanya hapo Mugana ndivyo alivyoendelea kutafuta watawa wenye moyo
na ujuzi hasa kuwasaidia akina mama katika elimu, afya na maendeleo hadi alipostaaafu
Dar es Salaam. Aliwatafuta masista wa Breda Uholanzi kufungua hospitali ya Rubya,
sasa ni hospitali teule ya wilaya, Masista wa Familia takatifu kutoka Uholanzi kuanza
shule ya msingi ya pekee Rumuli na shule ya kati Mwemage, Masista wa Mtakatifu Paulo
kushika duka la vitabu la Mtakatifu Joseph Dar, wakamelitane - Changombe, Waivrea
- Kawe, nk. Kilaini aliendelea kuwa; anakumbuka alimsindikiza kwa masista wa
Kamelitane na Waivrea alipokuwa anaomba, kila mara aliweza kujieleza vizuri sana na
kuonyesha ulazima wa wao kuja kusaidia wanawake. Katika kupigania elimu ya wanawake
labda ya kukumbukwa kuliko zote ni ujenzi wa shule ya sekondari ya wasichana ya Rugambwa.
Wakati huo hata kiulimwengu haja ya kuwasaidia wanawake ilikuwa bado haijapata msisitizo.
Kwa hilo Askofu Nkalanga alisema alipomwambia kwamba wajenge shule ya wasichana hadi
kidato ch sita kidogo baada ya kuteuliwa kuwa kardinali, hakuamini masikio yake kuwa
sababu hatukuwa na chochote. Aliendelea kuwa; alikuwa akimwona kama nabii kwa
sababu aliposema kitafanyika kitu kilifanyika hivyo aliamini tu. Kwanza kupata ardhi
ilikuwa shida lakini hapo Mwadhama hakuogopa mtu awe nani hata wakubwa wengine wa
serikali walipoweka vipingamizi alipigana tu. Hapa alitumia hadhi yake kwa watu ambao
walimwuunga mkono. Kwa ajili ya ujenzi alikwenda Ujerumani; akisaidiwa na Misereor,
alionana na bunge zima la nchi hiyo akiwemo, Raisi na viongozi wengine ambao wote
aliwahubiri juu ya ulazima wa kumwelimisha msichana mama na mwalimu wa kesho.
Kote huko hakuomba kitu kingine ila hicho tu. Walimwamini na kumpa fedha za kujenga
shule nzuri sana yenye kupendeza. Ilipokuwa tayari serikali ilisema haina pesa za
kuanza wakati huo kuiendesha, lakini akisaidiana na wananchi hasa wakulima wa kahawa
wa Bukoba walikubali kukatwa hela kuendesha shule, aliifungua mwaka 1964. Kusimamia
na kufundisha katika shule hiyo aliwapata masista mashuhuri kwa kuendesha shule za
wasichana, Masista wa Maryknol. Hawa tayari waliendesha shule za wasichana za Marian
Morogoro na Rosary college Mwanza. Hapa siyo tu alijenga shule bali kwa kuwahusisha
wananchi kuchangia uendeshaji wa shule hiyo, aliifanya shule ya watu wanaothamini
elimu ya wasichana. Katika maisha yake alipenda kuendeleza elimu hasa ya wasichana
kama chaguo la kwanza. Hata mwishoni mwa utawala wake Dar es Salaam alitumainia bado
kujenga shule ya sekondari ya wasichana ya bweni aliyotaka kuita 'Omushumba' maanake
mchungaji. Kwa hilo alimaanisha kazi yake ya uchungaji ni hasa kuelimisha wasichana
kama namna ya pekee ya kuelimisha jamii. WATAWA:Shirika la Dada wadogo wa Mtakatifu
Fransisko wa Asizi: Katika uzee wake kitu kimoja alichojivunia lilikuwa ni shirika
hili la watawa wa Dar es Salaam. Alisumbuka sana kulianzisha hasa kuwapata walezi
wazuri na kuwapa mwongozo. Alisema kuwa walicheka kwa sababu kila walipokwenda
kumtembelea aliwaonyesha picha hizo bila kutambua kwamba alisha waonyesha picha hizo
mara nyingi. Alipokwenda Ulaya alikwenda na picha hizo za wajukuu wake kama walivyowaita
kwa utani. Kila mara alitoa picha hizo mkobani na kueleza jinsi anavyotaka dada hao
wadogo wawe watawa wa Jiji wenye kujiamini, elimu na mbinu mpya za uchungaji. Aliwashika
kama mboni ya jicho lake. Kadiri siku za kustaafu kwake zilivyokaribia ndivyo
alivyozidi kupata homa juu ya wajukuu wake hao. Aliogopa kuwaacha yatima. Alipostaafu
kwa wema wao hakuwaingilia ili wampokee askofu mkuu mpya na waweze kuendelea bila
yeye. Hata hivyo kila mara aliulizia kwa mbali jinsi wanavyoendelea. Alifurahi kuona
wanakua vizuri na kushika kasi nzuri chini ya uongozi wa Sr. Paulin Bommer na shirika
la ‘Divine Providence’ la Balddeg Uswizi aliokuwa amewakabidhi. Hospitali ya Ukonga:
Mradi mwingine wa misho ilikuwa hospitali ya ukonga. Aliweka nguvu nyingi sana
katika mradi huu, kuipata ardhi ilikuwa na mlolongo mrefu sana lakini hakukata tamaa.
Kwa sababu aliamini kwamba anataka kuwasaidia watu wa sehemu hiyo ambayo ilikuwa mbali
ma huduma za afya alitulia nguvu zote za wadhifa wake kuletaufanisi. Kazi nyingine
ilikuwa kuwapata wafadhili. Katika hayo yote alifanikiwa na kuanzisha kituo cha afya
cha Ukonga kikiwa na lengo la kuwa hospitali kamili. Aliwaomba masista wa shirika
la Mtakatifu Therezia wa Mtoto Yesu wa Bukoba wamsaidie kuiendesha. Misingi aliyoiweka
ilifnikisha kituo hicho ambacho sasa ni hospili. Tunashukuru uongozi wa jimbo Kuu
la dar es salaam ambao walitambua juhudi hizo na kuiita jina lake. Pamoja na Ukonga
aliyaalika mashirika mengine kufungua zahanati katika sehemu mbali mbali za jiji
ikiwemo, Tegeta, Kawe na Kibiti. SIRI YA UFANISI WA RUGAMBWA Kilaini aliendela
kuandika katika mala kuwa Baada ya ibada ya misa ya kumwombea marehemu Rugambwa alimwendea
Padre Jovin Bakekera na kumwuliza amwambie siri ya mafanikio ya Kardinali Rugambwa.
Padre Jovin alikuwa katibu wake katika miaka tisa ya mwisho. Alifanya kazi naye katika
ofisi na aliishi naye nyumbani hadi alipokata roho. Baada ya kufikiri kidogo Bakekera
alisema 'sitaki mimi nimwite mtakatifu; lakini katika uamuzi wa kibinadamu alikuwa
mkamilifu, hii ilikuwa hoja kubwa na hivyo akamwomba maelezo yake ,naye alisema kufuatana
na cheo chake, heshima yake ya kifalme na unyamavu wake watu wengi walimwogopa, lakini
kusema ukweli alivyokaa naye miaka hiyo yote Rugambwa alikuwa na moyo mzuri ajabu,pamoja
na misimamo thabiti lakini hakupenda kumwudhi au kumwonea mtu. Kama alifanya kitu
na akaona emekuudhi hata ukiwa mdogo uliona alifanya juu chini mwenyewe kukuonyesha
kwamba anasikitika na alikuwa wa kwanza kuja kwako. Pia Kilaini aliuliza swali
hilo kwa Askofu Nkalanga, na kumjibu kwa kiingreza 'He had a golden heart' alikuwa
na moyo wa dhahabu. Alisema watu waliongelea sana juu ya unyenyekevu wake lakini alidhanizaidi
ya unyenyekevu yeye alikuwa na upendo mkubwa kwa watu. Yeye alijinyima vitu vingi
hata kukuta nguo zake nyingine zimechakaa lakini kila alichopata alitaka kiende kwa
watu wenye shida. Kilaini aliendelea; hata yeye vile vile alimjua kwa miaka 30;
hasa katika miaka ya 80 alipoanza kuugua alikuja Roma kwa matibabu akiwa mwanafunzi,
kitu kikubwa ambacho wote walijua ni kwamba hakutaka hata mara moja kusumbua watu
hata kama aliumwa, alitaka watu wafanye mambo yao wamalize kabla ya kumhudumia.
Siri yake nyingine ni kwamba alijua kutumia vipaji vya watu. Alipokuwa na kazi alimpa
mtu aliyeamini ataifanya vizuri lakini vile vile alifuatilia na alitaka ripoti kamili
za mara kwa mara. Mwadhama alijali sana uwezo katika kutoa kazi au madaraka,mtu akifanya
vibaya awe nani atamnyanganya kazi au madaraka. Alichukia kama kitu kilifanywa vibaya.
Watu wengine walichukia kwa sababu alitaka ripoti. Lakini jambo hilo liliwafurahisha
wafadhili kwa sababu alikuwa mkali sana katika matumizi ya fedha na kutoa ripoti.
Kwa sababu hiyo wafadhili wengi walimsaidia wakijua kwamba fedha zitatumika vizuri
kama zilivyokusudiwa. PUMZIKA KWA AMANI RUGAMBWA Apumzike kwa amani Rugambwa
kwa kazi yake kubwa alioifanya. Alivyotaniwa kila wakati na Askofu Isuja wa Dodoma,
yeye alikuwa namba one, katika upadre kijijini mwake, katika uaskofu Tanzania, Ukardinali
Afrika, na Askofu Mkuu wa kwanza Mtanzania Dar es Salaam. Sasa yuko kwa Mungu kama
Mwobezi wetu. Mungu amweke mahala pema mbinguni na sisi tufuate katika nyayo zake.
AMINA Ni makala ya Baba Askofu Kilaini msaidizi wa jimbo la Bukoba aliyoiandika
desembe 1997 baada ya kifo cha Hayati Kardinali Laurean Rugambwa – Imeandaliwa na
Angela Rwezaula.