2012-09-19 16:29:25

Parokia ya Bunena Bukoba yatimiza miaka mia, na Maziko mapya ya Kardinali Rugambwa.


Mamia ya waamini Jumapili walimiminika katika Ibada iliyoongozwa na Askofu Nestorius Timanywa wa Jimbo la Bukoba kuadhimisha sherehe ya Jubilee ya miaka mia tangu parokia ya Bunena , ilipoanzishwa na Wamisionari wa Afrika (White Fathers), mwaka 1912.
Katika homilia yake Askofu Timanywa aliwaasa waamini kwamba, Jubilee hii ya miaka mia, uwe ni wakati wa kuwaweka karibu zaidi na Mungu, na katika mshikamano na umoja wa kufanikisha maendeleo na ustawi wao kimaisha pia. Wafanye kazi kwa bidii na mshikamano zaidi, huku wakitakatifusha matendo yao na kukataa maovu na vishawishi vya shetani, kama tabia za ulevi, utoaji wa mimba, ufuska na kupambana kikamilifu na virus vya HIV/ UKIMWI.
Pia Askofu Timanywa alitangaza uwepo wa tukio jingine muhimu la kihistoria hivi karibuni ambamo Mtumishi wa Mungu , Marehemu Kardinali Laurian Rugambwa , atazikwa upya katika Kanisa Kuu la mjini Bukoba hapo tarehe 6 Octoba mwaka huu. Na alieleza sababu zilizochelewesha maziko hayo kwamba, ilitokana na ukarabati mkubwa uliohitajika kukamilishwa katika kanisa Kuu la Bukoba Mjini.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa, Mwili wa Marehemu Kardinali Laurian Rugambwa,tarehe Octoba 6, utasafirishwa kutoka kanisa la Kashozi na kuzikwa siku inayofuatia katika Kanisa kuu la Bukoba Mjini.
Marehemu Kardinali Laurian Rugambwa, ni mwafrika wa kwanza kupata daraja la Kardinali katika Kanisa Katoliki la Ulimwengu. Aliifariki dunia akiwa na Umri wa miaka 85, Desemba 8 1997, jijini Dar es salaam na kupewa maziko ya muda katika Kanisa la Kashozi Bukoba.
Kuteuliwa kwake kuingia katika Decania ya Makadinali , kulionyesha alama ya utambuzi kwamba, Kanisa la Roma si kanisa la Magharibi, bali ni kanisa la Ulimwengu. Na hivyo kuonyesha umuhimu wa mpanuko wa mashirika ya kanisa sehemu mbalimbali za dunia, ikifuta muono wa nyuma wa kutawaliwa na wamisionari kutoka mataifa ya Magharibi.
Kardinali Rugambwa anakumbukwa kwa mchango wake mkubwa alioutoa wakati wa Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatican, ambamo alihimza umuhimu wa jumuiya za walei, kujihusisha katika kazi na utume wa kanisa. Alisistiza, utendaji wa kazi za missioni kwamba hauwezi kutenganishwa utendaji wa maisha ya kila siku ya muumini. Na aliwataka Wakatoliki, kuwa tayari kushirikiana na wasiokuwa Wakatoliki, kutembea pamoja katika hija ya maisha ya hapa duniani. Alisisitiza Kanisa lipaswa kuwa mwalimu wa maisha. Kati ya urithi ulioachwa nae ni Hospitali ya Rubya na Mugana , pia seminari ya Ntungamo na Shule ya Wasichana ya Rugambwa , vyote vikiwa mkoani Kagera.








All the contents on this site are copyrighted ©.