2012-09-12 14:13:05

Tanzia: Askofu Paschal William Kikoti amefariki dunia


Kwa masikitiko , tunatoa habari za kifo cha Askofu wa kwanza wa Jimbo Katoliki la Mpanda, Mkoani Katavi Tanzania , Mhashamu Askofu Paschal William Kikoti, aliyefariki dunia siku ya Jumanne kwa ugonjwa wa shinikizo la damu , akiwa katika hospitali ya Rufaa ya Bugando jijini Mwanza.
Padre Patrick Kasomo, Vika wa Askofu Jimbo la Mpanda, alitangaza msiba huo Jumanne mbele ya mamia ya waumini walikusanyika katika Kanisa Kuu la Mpanda baada ya kupata taarifa hizo.
Kwa mujibu wa Padre Kasomo, Askofu Kikoti alipatwa na shinikizo la damu Jumapili iliyopita majira ya asubuhi wakati akioga na kuanguka chini ghafla na kupoteza fahamu. Na Mapadre na Watawa waliofika nyumbani kwake baada ya Ibada ya Misa ya kwanza ya majira ya saa mbili na nusu za asubuhi, walimkuta katika hali hiyo ya kutojitambua.
Na mara walitoa taarifa kwa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), ambalo lilitafuta usafiri wa ndege na kumsafirisha hadi hospitali ya Rufaa Bugando Mwanza , ambako alianza kupatiwa matibabu hadi alipofariki siku ya Jumanne.
Marehemu Askofu Kikoti , alizaliwa parokiani Nyabula , mkoani Iringa mwaka 1957 na kupewa daraja la Upadre June 29 , 1988 mkoani Iringa.
Aliteuliwa kuwa Askofu wa kwanza wa Jimbo la Mpanda na Papa Yohane Paulo 11 0ctoba 2000, na kusimikwa January 24, 2001.
Marehemu Askofu Kikoti atazikwa siku ya Jumamosi, Mosi Septemba 2012, katika Kanisa Kuu la Mpanda.
Tunamwombea pumuziko la amani peponi.







All the contents on this site are copyrighted ©.