2012-07-04 09:13:27

Wasifu wa Askofu mkuu Protas Rugambwa


Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania limepokea kwa moyo wa furaha na shukrani kuu habar iza uteuzi wa Askofu Protas Rugambwa aliyekuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Kigoma, kuwa Katibu mkuu msaidizi Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa pamoja na kumpandisha hadhi kuwa ni Askofu mkuu. RealAudioMP3

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linasema hizi ni dalili za kukua na kukomaa kwa Kanisa la Tanzania, tayari kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa katika ngazi ya kiulimwengu. Wanamshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa kutoa heshima hii kubwa kwa Kanisa la Tanzania.

Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu Protas Rugambwa alizaliwa kunako tarehe 31 Mei 1960, Bunena, Jimbo Katoliki la Bukoba. Alipata majiundo yake ya Kipadre kutoka katika Seminari ndogo za Katoke iliyoko Rulenge-Ngara na Itaga, Jimbo kuu la Tabora. Kwa masomo ya Falsafa alipelekwa Seminari kuu ya Kibosho iliyoko Jimbo Katoliki la Moshi na Masomo ya Taalimungu aliyapatia Seminari kuu ya Mtakatifu Karoli Lwanga, maarufu kama Segerea.

Baada ya masomo na majiundo yake ya Kipadre, alipadrishwa kunako tarehe 2 Septemba 1990, Jimbo kuu la Dar es Salaam wakati wa Hija ya Kichungaji ya Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili nchini Tanzania. Yeye alikuwa ni kwa ajili ya Jimbo Katoliki Rulenge kwa wakati huo. Baada ya Upadrisho alifanya utume Parokiani, Seminari Ndogo ya Katoke, Mwenyekiti wa Idara la Liturjia Jimbo Katoliki Rulenge na Mhudumu wa shughuli za kiroho Hospitali ya Biharamulo.

Kuanzia mwaka 1994 hadi 1999 alipelekwa mjini Roma kwa masomo kwa masomo ya juu katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano na kujipatia Shahada ya Uzalimivu katika shughuli za kichungaji. Baada ya kurudi Jimboni mwake Rulenge, alipangiwa kuwa Mwalimu na Mkurugenzi wa miito na Mkurugenzi wa shughuli za Kichungaji; Makamu Askofu.

Kunako mwaka 2002 hadi 2008 aliombwa kwenda kusaidia kutoa huduma za kichungaji kwenye Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu, utume ambao aliufanya kwa ufanisi mkubwa. Kunako tarehe 18 Januari 2008, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, akamteuwa kuwa ni Askofu wa Jimbo Katoliki Kigoma, Tanzania na kuwekwa wakfu hapo tarehe 13 Aprili 2008.

Baada ya Askofu Protas Rugambwa kuwafundisha, kuwaongoza na kuwatakatifuza Watu wa Mungu Jimbo Katoliki Kigoma, tarehe 16 Juni 2012, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, akamteua kuwa Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa.








All the contents on this site are copyrighted ©.