Benedikto XVI: dhana ya maisha mintarafu jamii za Kiafrika
Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, nakukaribisha tena kwa furaha kabisa tuendelee
na uchambuzi wetu wa Hati Dhamana ya Afrika: Africae Munus. Juma lililopita tulizungumzia
juu ya vijana na watoto. Tulichambua mambo
mengi mintarafu wao ni nani na nafasi yao katika jamii, wajibu wa jamii kwa makundi
hayo; na nini Kanisa linafundisha na kutenda juu ya vijana na watoto. Leo Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita, anatuongoza katika kutafakari kwa kina kuhusu mtazamo wa
Kiafrika juu ya maisha. Maisha kwa mtazamo wa Kiafrika ni zawadi kubwa kutoka kwa
Mungu. Maisha yanajumuisha viumbe vyote vilivyo hai na visivyo hai. Ni muunganiko
wa walio wazima na waliotangulia mbele ya haki, wanaozungumza na wasiozungumza, waliozaliwa
na ambao bado hawajazaliwa, wanaofikiri na wasiofikiri. Kimsingi tamaduni za Kiafrika
zinatoa nafasi na heshima kubwa kwa uhai. Kuna imani kubwa kwamba maumbile ya kiulimwengu
kama yalivyo, yapo ili kutunza, kulinda na kurutubisha uhai. Vizazi vilivyopo
havina budi kuheshimu vizazi vilivyo tangulia na vijavyo ndio maana kuna miungu na
mababu ambao wameabudiwa na kuheshimwa tangu mwanzo; na nyakati za shida huelekezewa
maombi ya msaada na jamii husika kama waombezi na waangalizi wa jamii. Urithi huu,
anasema Baba Mtakatifu ni nafasi nzuri kwa familia ya Mungu Barani Afrika kuelewa
ujumbe wa Kristo, kuthamini fumbo la Kanisa na kuendelea kuthamini maisha katika mtazamo
wa Kikristo. Mababa wa Sinodi katika uchambuzi wao kuhusu kutunza na kuthamini
uhai barani Afrika, walizingatia kwa makini jitihada mbali mbali zinazofanywa na jumuiya
ya Kimataifa. Hata hivyo waligundua utata kwa baadhi ya jitihada hizo hususan juu
ya majina yake na maana yake, ambazo kwa namna fulani zilionekana kupingana na mafundisho
na maadili ya Kikristo. Hata hivyo wao hawakusita kutoa mwelekeo sahihi juu ya maisha
kadiri ya mafundisho ya Kikristo. Walilaani kwa namna ya pekee matumizi ya njia za
kisasa za mpango wa uzazi na kupaaza sauti dhidi ya utoaji mimba. Baba Mtakatifu
alisisitiza kwamba wako watu, makundi, taasisi na hata mataifa ambayo yanapinga msimamo
wa Kanisa dhidi ya njia za kisasa za mpango wa uzazi. Lakini Kanisa lisiogope makundi,
taasisi na hata mataifa haya, bali lazima lisimamie ukweli daima ili kuhifadhi thamani
ya maisha na hadhi ya mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Muumba wake. Amewataka
Wanafamilia ya Mungu kuwepo duniani lakini wasijihusishe na mambo ya dunia hii. Aidha
Baba Mtakatifu anaendelea kubainisha mambo ambayo yanaendelea kutishia na kudhoofisha
maisha Barani Afrika, ambayo ni pamoja na umaskini, magonjwa na ujinga. Mambo haya
yanawatatiza sana watu wa Bara la Afrika, amabapo wengi wao wanaishia katika matatizo
na majanga makubwa kama njaa, vita vya wenyewe kwa wenyewe, biashara ya ukahaba, UKIMWI,
Kifua kikuu, Malaria, matumizi harem ya dawa za kulevya, utoaji mimba, ubakaji, na
imani potofu zinapolekea mauaji ya vikongwe, watu wenye ulemavu wa ngozi, biashara
haramu ya viungo vya binadamu na dhuluma nyingine za Kijamii. Analitaka Kanisa
kufanya tafakari ya kina kuhusu hali ya Bara la Afrika na kubuni mbinu mkakati ili
kusaidia kutatua na kurudisha nafuu ya maisha kwa watu wa Bara hili. Amezialika taasisi
za Kanisa Barani Afrika kuvalia njuga swala la Elimu ambayo anaamini yaweza kuwa ufunguo
kwa matatizo mengi. Elimu hii ilenge kumjenga Mwafrika, akatambue barabara mazingira
yake hivi kwamba kwa elimu hii aweze kubuni njia za kujijengea maisha pale alipo na
kwa rasilmali zinazopatikana karibu naye. Hii itasaidia kuondokana na fikra potofu
kwamba maendeleo ya Afrika lazima yatoke nje ya Afrika. Elimu hii imsaidie kujenga
fikra bora juu ya maisha binafsi, mtu mmoja mmoja aweze kutumia mwanga huu kuishi
maisha yanayolingana na wakati dunia ilipofikia. Sanjari na hilo anaialika Jumuiya
ya Kimataifa, taasisi na mataifa yenye nguvu kuzingatia na kutenda katika kweli kwani
kila mtu akimtazama mwingine kwa viwango anavyojitazama mweneywe vitendo vya kibinafsi
vinaweza kukomeshwa. Misaada inyotolewa kwa Bara hili itolewe kwa moyo wa upendo na
ilenge miradi ya kumnufaisha kwanza Mwafrika na sio kujenga mirija ya kulinyonya zaidi
bara hili. Yaangaliwe maeneo ambayo mwenyeji akielekezwa anaweza kwa msaada kidogo
kunyanyua maisha yake na wanajumuiya wenzake. Hadi hapo tumefikia mwisho wa tafakari
yetu kwa siku ya leo. Nakutakia heri na baraka toka kwa Mweneyezi Mungu na mfungo
mwema wa kwarema. Ni mimi mtayarishaji na msimulizi wako Padre George wa Bodyo.